Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Songwe

Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imeanza ujenzi wa Barabara ya Kiwira–Landani kwa kiwango cha lami yenye urefu wa Km 5 pamoja na daraja lenye urefu wa mita 40 kwa gharama ya shilingi bilioni 5.7 Wilayani Ileje ili kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi.

Hayo yameelezwa na Meneja wa TARURA Mkoa wa Songwe, Mhandisi Kilian Haule ambapo ameeleza kuwa barabara hiyo ni muhimu kwa Mkoa wa Songwe kwani inaunganisha eneo la kiwanda pamoja na sehemu ambayo makaa ya mawe yanachimbwa na itapunguza umbali wa magari kuzunguka umbali wa Km 40 katika usafirishaji wa makaa hayo.

‘’Mradi huu ni muhimu kwa Mkoa wa Songwe hasa katika Wilaya ya Ileje na kwa wananchi wa Kijiji cha Kapeta pamoja na Kitongoji cha Landani kwani itaongeza mapato katika Mkoa kupitia magari makubwa ya usafirishaji wa makaa ya mawe tofauti na hapo awali’’, alisema.

Aliongeza kuwa mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi Ira JV Global Link na kusimamiwa na Mhandisi Mshauri wa mradi Luptan Company Ltd na utekelezaji wake umeanza Machi 2023 ambapo unatarajiwa kukamilika ifikapo Februari 2024 na kwasasa mradi umefikia asilimia 40 kukamilika na Mkandarasi yupo eneo la kazi anaendelea na utekelezaji wa mradi.

Pia Mhandisi Kilian alieleza kuwa TARURA Mkoa wa Songwe inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi wa miundombinu ya barabara kupitia bajeti iliyoidhinishwa ya shilingi bilioni 17 kwa mwaka huu wa fedha 2023/24 ili kuendelea kuwafikisha wananchi kufika kusikofikika.

Naye Bw. Octavius Wangu Mkazi wa Kitongoji cha Landani alisema Barabara ya Kiwira –Landani imekuja wakati sahihi kwani itawasaidia kuwaunganisha wakazi wa kijiji cha Kapeta na Kitongoji cha Landani kufanya shughuli zao za kiuchumi.

“Tunaishukuru Serikali kupitia TARURA kwa jitihada za kuhakikisha barabara hii inakamilika na kutuwezesha wananchi kuwasiliana kwa urahisi pamoja na kufika katika mgodi wa mawe (Kiwila Cool Mine) ili kuendelea na shughuli zetu za uzalishaj tofauti na hapo awali ambapo ilitulazimu kuzunguka umbali wa Km 40 kufika katika shughuli zetu za kiuchumii”, alisema Bw. Octavius.

Sh

By Jamhuri