Benki Kuu ya Tanzania inapenda kuukumbusha umma kwamba Serikali ilishatoa  Tamko kuhusu katazo la matumizi ya fedha za kigeni kwa wakaazi wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania katika kulipia bidhaa na huduma nchini. Tamko la kwanza  lilitolewa mwezi Agosti 2007 na la pili mwezi Desemba 2017. Hata hivyo, katika siku  za karibuni imebainika kuwepo kwa ukiukwaji wa Tamko hilo. Hivyo, Benki Kuu  inapenda kuukumbusha umma kwamba maagizo yaliyotolewa hapo awali kuhusu  matumizi ya fedha za kigeni yanapaswa kuendelea kuzingatiwa kama ifuatavyo: 

  1. Bei zote hapa nchini zitangazwe kwa shilingi ya Tanzania. Bei hizi zinajumuisha  kodi za kupangisha ardhi, nyumba na ofisi; gharama za elimu; huduma za afya,  vifaa tiba na vitendanishi; gharama za usafiri, lojistiki na bandari; vifaa vya  kielektroniki na huduma za mitandao ya mawasiliano, n.k.  
  2. Bei ambazo walengwa wake wakuu ni watalii au wateja wasio wakaazi  zinaweza kutangazwa kwa fedha za kigeni na malipo yake yanaweza kufanyika  kwa fedha za kigeni. Bei hizi zinajumuisha gharama za hoteli, usafiri, gharama  za viwanja vya ndege na viza kwa wageni, usafirishaji kwenda nchi za nje  kupitia Tanzania na gharama za mizigo bandarini. Walipaji wanaotumia fedha  za kigeni watambuliwe kwa vitambulisho vyao kama pasi za kusafiria na  nyaraka za usajili kwa makampuni.  

iii. Viwango vya kubadilisha fedha vitakavyotumika katika kuweka bei hizo viwekwe wazi na visizidi vile vya soko. Ifahamike wazi kuwa ni benki na maduka  ya kubadilisha fedha za kigeni pekee yanayoruhusiwa kupanga viwango vya  kubadilisha fedha kutokana na ushindani katika soko la fedha za kigeni.  

  1. Mkaazi yeyote wa Tanzania anapaswa kufanya malipo kwa kutumia shilingi ya  Tanzania pekee na hivyo asilazimishwe kulipia bidhaa au huduma yoyote hapa  nchini kwa kutumia fedha za kigeni.  

Benki Kuu inapenda pia kuukumbusha umma kuwa kifungu cha 26 cha Sheria ya  Benki Kuu ya Tanzania ya mwaka 2006 kinaelekeza kuwa shilingi ya Tanzania ndiyo  fedha pekee ambayo inaruhusiwa kutumika nchini, hivyo hakuna mtu au kampuni  yoyote inayoruhusiwa kuikataa kwa malipo yoyote halali (legal tender). Kitendo cha  kukataa malipo kwa shilingi ya Tanzania ni kuvunja Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania  ya mwaka 2006. 

GAVANA 

BENKI KUU YA TANZANIA