pg 1Tuhuma za wabunge kuchukua au kuomba rushwa kutoka katika mashirika na taasisi wanazozisimamia, zimechukua sura mpya baada ya kubainika mkakati unaosukwa na wabunge wafanyabiashara ya mafuta kuiangamiza Mamlaka ya Nishati na Maji (EWURA), waweze kurejesha uchakachuaji wa mafuta.

Mbali na hilo, kuna mbunge aliyeomba kiasi cha Sh milioni 100 kutoka taasisi inayosimamiwa na kamati yake, huku mwingine akiomba walipe posho badala ya kupewa chai na chakula, uchunguzi wa JAMHURI umebaini.

“Spika hakufanya uamuzi wa kuvunja Kamati kutokana na habari zilizochapishwa magazetini, bali kwa muda mrefu vyombo vya dola vimekuwa vikifuatilia mienendo ya wabunge hawa na wengi wameonekana kukiuka mienendo na taratibu za kibunge.

“Upo ushahidi wa sauti kabisa, ambapo mbunge huyu anaomba posho, mwingine anaomba milioni 100. Watumishi wa hilo shirika wakamuuliza, ‘hivi tukikupa hizo milioni 100 sisi tutazitoleaje taarifa katika mizania ya hesabu?’ Akawaambia atawapa njia jinsi ya kufanya. Ndipo wakaripoti kwenye vyombo vya dola, likaanza kufanyiwa kazi… watu wameona matokeo tu, wabunge wanafuatiliwa nyendo zao,” kilisema chanzo cha habari kwa JAMHURI.

 

Kamati ya Nishati na Madini

Uchunguzi uliofanywa na JAMHURI umebaini kuwa wabunge wafanyabiashara ya mafuta walianzisha zengwe kwenye kikao cha Kamati ya Nishati na Madini kama harakati za kuivunja Ewura.

Katika kikao cha Kamati hiyo cha Februari 10, 2016, Ewura ilipofika mbele ya Kamati walijitahidi kuonesha kuwa taasisi hiyo haifanyi kazi yoyote zaidi ya kuvuna fedha za wananchi kupitia tozo inazopata kwenye mafuta.

Wabunge 14 kati ya 16 waliochangia hoja, walijenga hoja kuwa kazi zinazofanywa na Ewura sasa zinastahili kufanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kwani tayari kama ni magari yanayopeleka mafuta nje ya nchi yanawekewa lakiri, hivyo yakithubutu kushusha mafuta yanayopelekwa nje ya nchi, basi yatabainika na kukamatwa.

Hoja nyingine waliyojenga wabunge hao ni kuwa Ewura badala ya kuweka vinasaba kwenye mafuta yanayouzwa katika soko la ndani, iweke vinasaba kwenye mafuta yanayouzwa nje ya nchi kwani vinasaba hivyo havina maana yoyote. Hoja nyingine iliyojengwa ni kuwa Ewura wanalipwa mishahara mikubwa na wanalipwa kwa dola.

 

Catherine Magige

Mbunge wa Viti Maalum (CCMkashililah-feb17-2014), Catherine Magige, alihoji Ewura inasaidiaje kuwaletea maendeleo wananchi na kupunguza ukali wa maisha, huku akiongeza kuwa zipo taarifa kuwa wanalipwa mishahara kwa dola za Marekani.

Hoja hii ilijibiwa kuwa Ewura inachangia maendeleo nchini kwa kudhibiti na kushusha bei za mafuta, kisha kuongeza mapato ya Serikali kwa kuwadhibiti wakwepaji kodi. Walitaja pia udhibiti wa ubora wa mafuta wanaofanya kuepusha mitambo na vyombo vya moto kuchakaa haraka kutokana na uchakachuaji uliokuwa unafanywa awali.

Taarifa zilizoifikia JAMHURI zinasema Catherine aliamua kuwasulubu Ewura baada ya kuwa ameombwa na Mbunge mfanyabiashara ya mafuta, Ahmed Shabby, ‘asaidie’ kusukuma ajenda ya kuhakikisha Ewura inafutwa au inafuta mpango wa kuweka vinasaba kwenye mafuta.

Akizungumza na JAMHURI, Catherine amesema Shabby hoja ya kupinga vinasaba amekuwa akimwambia kila mbunge na kwamba siku moja Dodoma alitaka kumpa hoja hiyo, ila akamshauri awape Ally Mohamed Kessy wa Nkasi au aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati, Martha Mlata. 

“Situmiwi na Shabby wala mbunge yeyote, haya yalikuwa mawazo ya Kamati yote,” anasema Catherine.

Anasema Kamati haikuridhishwa na majibu ya Ewura, hivyo wao walitaka kuwaita kwa mara ya pili waweze kufafanua zaidi tuhuma zinazoelekezwa kwao ikiwamo hizi za vinasaba. 

“Sioni tabu ni nini, hawa tulitaka waje mbele ya Kamati wajieleze, lakini inavyoonekana kuna mtu anawatisha na kuwapa taarifa zisizo sahihi na ndiyo maana jambo hili limekuzwa kiasi hiki,” anaongeza Catherine.

 

Deogratius Ngalawa

Mbunge wa Ludewa (CCM), Deogratius Ngalawa, alihoji fedha zinazokusanywa na Ewura kutoka kwenye mafuta zinatumiwaje na zinakwenda kwenye taasisi ipi.

Walimjibu kuwa fedha hizo hutolewa kwa kampuni zinazoshiriki mnyororo wa kuagiza na kusambaza mafuta nchini ambazo ni Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), TBS, Wakala wa Vipimo (WMA), Mamlaka ya Kodi (TRA), Tipper, Wakaguzi wa Mafuta Bandarini, Ewura, Wasambazaji wa Mafuta na Wasafirishaji wa mafuta.

 

Katani Ahmed Katani

Mbunge huyu alijenga hoja kwa nini Ewura asilimia 80 ya kazi zake zinahusiana na Wizara ya Nishati na Madini, lakini inaripoti kwa Waziri mwenye dhamana na masuala ya maji na si wizara mama. Huyu walimjibu kuwa suala hilo limefanyika kwa kufuata misingi ya udhibiti.

JAMHURI imewasiliana na mwanasheria aliyeomba asitajwe kwa maelezo kuwa hataki kujiingiza kwenye siasa, anayesema: “Misingi ya udhibiti inataka taasisi inayodhibiti wizara au vitengo vilivyopo chini ya wizara husika isiwajibike kwa wizara inayoidhibiti kuepuka mdhibiti kama Ewura kupewa maelekezo au kufutwa kirahisi.”

 

Joyce Bitta Sokombi

Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Bitta Sokombi, alihoji inakuwaje bei za mafuta hazishuki. Majibu yaliyotolewa na Ewura yamefumua upupu. Ewura walijibu kuwa bei ya mafuta ya Desemba, 2015 na Januari na Februari, 2016 hazikushuka kwa kiasi kilichotarajiwa kutokana na kosa lililofanywa katika miezi ya Septemba, Oktoba na Novemba 2015 baada ya Serikali kuagiza mafuta bila kufuata utaratibu wa zabuni.

Uchunguzi uliofanywa na JAMHURI umebaini kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa), George Simbachawene, wakati huo akiwa Waziri wa Nishati na Madini aliruhusu zabuni namba 37, 38 na 39 kukiuka utaratibu za zabuni ya ununuzi wa mafuta kwa pamoja, hali iliyoongeza gharama.

“Unafuu mkubwa ungeonekana katika miezi ya Disemba, 2015, Januari na Februari 2016 kwa nchi kunufaika na punguzo la premium (malipo) ya dola milioni 19.8 (Sh bilioni 43.5). Uingizaji mafuta katika kipindi hicho ulikuwa nje ya utaratibu wa ushindani ambapo wastani wake wa gharama ulipanda hadi kufikia dola milioni 60.6 (Sh 133,320), kwa tani badala ya dola 42.7 (Sh 93,940) au chini ya hapo wakati mafuta yakipatikana kwa ushindani.”

Hii ina maana zabuni hizo zilizoagizwa na Wizara ya Nishati na Madini chini ya Simbachawene, Sh bilioni 43.5 zilizoongezwa kama ‘cha juu’ ziliingia kwenye mfuko usiofahamika ni wa nani. JAMHURI imemtafuta Simbachawene kwa udi na uvumba ajibu swali hili, lakini hadi tunakwenda mitamboni hakupatikana.

 

Mulla, Kess, Mathayo wapinga vinasaba

Wabunge Haroon Mulla Pirmohamed (CCM) wa Mbarali, Vedasto Mathayo Manyinyi wa CCM (Musoma Mjini) na Ally Mohamed Kessy wa Nkasi (CCM), walieleza nia yao ya kupinga vinasaba katika mafuta yanayouzwa ndani ya nchi.

Hoja yao ni kuwa vinasaba viwekwe katika mafuta ya kuuzwa nje ya nchi kwani havina faida yoyote zaidi ya kuongeza gharama. Pia Mathayo alituhumu kuwa vinasaba vinapatikana mitaani.

Uchunguzi wa JAMHURI kwanza umebaini kuwa Mathayo ni muuzaji wa mafuta, lakini si hilo tu, kituo chake cha mafuta kilichopo Musoma ni moja kati ya vituo vilivyokutwa vinauza mafuta yasiyo na vinasaba vikapigwa faini ya Sh milioni 7.

Mbali na kuwapo mgongano wa maslahi kuwa Mathayo anafanya biashara ya mafuta na bado yumo kwenye Kamati ya Nishati na Madini, Sheria ya Ewura inasema wazi kuwa muuza mafuta au kituo chake kikipigwa faini mara ya kwanza kinatozwa kati ya Sh milioni 5 na 7. Kikirudia mara ya pili kinatozwa faini ya Sh milioni 25 na kikikutwa mara ya tatu kinauza mafuta yasiyo na vinasaba kinafutiwa leseni.

Kati ya vituo vilivyotajwa na Ewura kuwa vinauza mafuta yaliyopaswa kusafirishwa nje ya nchi, ni pamoja na kituo kinachomilikiwa na Mbunge wa Gairo, Ahmed Shabby, na cha Manyinyi. Hii ya wabunge Manyinyi na Shabby kutajwa kati ya vituo vinavyouza mafuta yaliyokwepa ushuru na yasiyo na vinasaba, inatajwa kuwa iliwakera wabunge na wakaona waanze juhudi za kuisambaratisha Ewura. Shabby amekwishapigwa faini ya Sh milioni 25 akalipa, hivyo akikutwa mara ya tatu atafutiwa leseni.

Vituo walivyovitaja kwenye Kamati ni Bweri Petro Station Musoma (Lake Oil), Bunda Filling Station, Bunda (Mhe. Vedasto Mathayo), New Gapco Bukoba Service Station (Numi Investments), Olympic Energy Kashozi Rd. Bukoba (Hamid Noorani), Ahmed M. S. Shabby Petro Station – Makole Dodoma, Lake Oil Limited – Msamvu (Lake Oil), Lake Oil Limited Nanenane Morogoro (Lake Oil), Govidet Negelo & Co. Ltd (Selestine B. Mhagama) na Kifaru Oil Co. Ltd – Misugusugu Kibaha (Rajabu Varisanga).

Kwa mwaka 2011 hadi 2015 zilichukuliwa sampuli kutoka kwenye vituo 2,130, ambapo vituo 300 vilikutwa na vinasaba chini ya kiwango. Katika mwezi Januari 2016, Ewura imekagua vituo 125 katika baadhi ya mikoa ya Kanda ya Ziwa, Dodoma, Morogoro na Pwani. Kati ya vituo hivyo, vituo 9, sawa na asilimia 7.2 vilikutwa na mafuta yasiyo na vinasaba vya kutosha. Vituo hivyo vimetajwa hapo juu.

Kiujumla, wabunge wajumbe wa Kamati hiyo walionekana kuwa na mshikamano kutaka kuisulubu Ewura, hali iliyomfanya Mwenyekiti wa Kamati aliyeondolewa, Martha Mlata, kuamua kupingana na wabunge hao akiamini kuwa wanachotaka kufanya ni kuirejesha nchi katika enzi za uchakachuaji wa mafuta.

Ally Kessy anasema kuwa lengo la kuwekwa vinasaba katika mafuta ilikuwa ni kuondokana na tatizo la uchakachuaji wa mafuta, lakini hivi sasa uchakachuaji uliokuwa ukifanywa na baadhi ya wafanyabiashara wa vituo vya kuuzia mafuta ambao walikuwa wakichanganya petroli na mafuta ya taa umekwisha.

Kessy anasema uwekaji vinasaba katika mafuta haukubaliki, ni wizi wa wazi ambao lazima ukomeshwe na wale wenye uchungu na nchi ya Tanzania.

“Kwani wewe hauna uchungu na nchi wewe? Hawa wanaojiita waweka vinasaba wanalipwa kiasi kikubwa mno cha fedha ambacho kinapotea bure. Haiwezekani tuendelee kuona kampuni za nje kuja kutuibia. Wanalipwa shilingi 12.50 kwa kila lita moja, hebu piga hesabu uone mara lita 300,000 ni shilingi ngapi zinapotea kwa kumlipa mtu yuko Dubai, sijui wapi,” anasema Kessy.

Alipoulizwa kuhusiana na taarifa za yeye kusambaza ujumbe mfupi wa maandishi kuwashawishi wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini kuiweka kiti moto Ewura kwa mara ya pili, anasema ni kweli anawashawishi kuiita kwa mara ya pili kuihoji. “Ni kweli kabisa nafanya hivyo ili tuweze kukutana nao tena.”

Anasema pamoja na utaratibu huo mbovu wa vinasaba, wapo baadhi ya watu wanafanya biashara ya kuuza vinasaba mitaani, lakini hakuwa tayari kueleza ni sehemu gani na kwa kiasi gani vinauzwa.

Kwa upande wa Mbunge wa Gairo, Ahmed Shabby, akizungumzia  kupigwa faini mara mbili kutokana na uuzaji wa mafuta yasiyo na vinasaba, anasema kinachofanywa na maafisa wa Ewura ni uhuni kwani hajawahi kukiuka sheria na taratibu za biashara ya mafuta na kuwa maafisa hao wamekuwa wakifanya hujuma kwa wafanyabiashara.

Shabby anasema yeye binafsi anashangazwa na taarifa za ukwepaji kodi kwa kuuza mafuta yanayotakiwa kusafirishwa nje ya nchi kwani yeye hununua mafuta jijini Dar es Salaam na kuyasafirisha ambapo maafisa wa Ewura huweka vinasaba katika mafuta yakiwa kwenye gari kabla ya kusafirishwa na kumpatia nyaraka zilizogongwa mihuri dereva wa gari husika kuanza safari.

“Vinasaba vinawekwa huko huko Dar es Salaam, na wakishaweka hivyo vinasaba vyao mafuta hayabadiliki rangi yanabaki na rangi yake ile ile. Dereva hana ujuzi wa kugundua anachowekewa kwenye mafuta kama ni juisi, dawa au nini. Wao wanaweka vinasaba vyao mafuta yakishafika tu kituoni na kushushwa baada ya siku mbili watu wa Ewura wanakuja kufanya ukaguzi na kudai kuwa hakuna vinasaba, huu ni uhuni na njama za hovyo,” anasema Shabby.

Anasema yeye binafsi hana mashine za kupimia vinasaba, hivyo ni vigumu kufahamu kama mafuta yaliyoletwa kwake yamewekewa vinasaba au la.

Alipoulizwa iwapo kuna hujuma zinazofanywa na maafisa wa Ewura na kupigwa faini mara mbili zenye thamani ya milioni 32, kwanini alikubali kulipa, akasema alilazimika kulipa faini hizo kutokana na sheria ngumu za Ewura ambazo zinambana mfanyabiashara kiasi cha kushindwa kwenda kufungua mashtaka mahakamani.

Shabby anasema tayari amefikisha malalamiko yake kwa Waziri  Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa, na Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo, ambao wote waliahidi kutafuta ufumbuzi wa suala hilo.

“Nilipopigwa faini nilisema wacha nilipe tu, ili biashara zangu ziendelee wakati nikitafuta mwafaka, maana mabasi yangu yote yanajaza mafuta katika kituo changu, ila tayari nimewasiliana na mwanasheria wangu ili niweze kuwashtaki Ewura warudishe pesa zangu,” anasema Shabby.

Anaeleza kuwa vinasaba vimekuwa vikiuzwa mtaani kwa gharama ya Sh milioni 2 kwa lita moja na kwamba wauzaji wa vinasaba hivyo ni miongoni mwa maafisa  wa uwekaji vinasaba katika mafuta yanayosimamiwa na Ewura na wateja wao wakubwa ni wafanyabiashara wakubwa wa mafuta ambao wana maghala makubwa ya kuhifadhia mafuta.

Kuhusiana na yeye kupeleka habari katika magazeti ili kumng’oa Martha Mlata katika nafasi ya uenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, anasema katika chombo hicho cha habari ambacho anatuhumiwa kupeleka habari hana mawasiliano na mwandishi yeyote wa habari na hana urafiki nao.

“Kama Mlata alikula rushwa, hilo ni juu yake atafute tu jinsi ya kujinasua si kutapatapa. Mimi simjui mwandishi yeyote wa habari huko, na wala sijawahi kuongea na mwandishi wa huko,” anasema Shabby.

 

Martha Mlata

Wajumbe wenzake wa Kamati wanamtuhumu kuwa mara kadhaa alionekana akiwa karibu na viongozi wa Ewura na hata walipokuwa kwenye vikao alikuwa akizuia hoja sawili za wabunge walipotaka kuibana Ewura. Kwa mantiki hiyo, wakasema wanahofu alikuwa akifanya kazi kwa niaba ya Ewura.

Uchunguzi unaonesha kuwa Martha alichukua msimamo huo, baada ya kupata taarifa za kina kuwa baadhi ya wabunge kutokana na maslahi binafsi wameamua kuisulubu Ewura ikiwezekana ivunjwe, au vinasaba viache kuwekwa kwenye mafuta wao wazidi kuuza mafuta ya kwenda nje ya nchi kwenye soko la ndani.

Kosa alilofanya Martha, taarifa za kina zinaonesha kuwa hakupata kuujulisha uongozi wa juu wa Bunge kuwa amepata tuhuma hizo, na katika hali ya kawaida kuonekana anakutana na viongozi wa Ewura katika maeneo kama hoteli kuliwatia wasiwasi si wenzake tu, bali hata uongozi wa Bunge na hivyo kumtuhumu.

JAMHURI imemtafuta Martha kuzungumza naye, ila mara zote alisema yuko katika maandalizi ya kwenda kanisani, na hadi tunakwenda mitamboni hatukufanikiwa kuzungumza naye.

 

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam

 Ripoti ya utafiti iliyofanywa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam inaonesha kuwa tangu mwaka 2011 Ewura ilipoanza kuweka vinasaba kwenye mafuta, kiwango cha kodi kinachokusanywa kimeongezeka kwa Sh bilioni 468.50.

“Ewura hususan katika udhibiti wa uchakachuaji na uuzaji wa mafuta ya transit bila kulipiwa kodi ilikuwa imeleta mafanikio kifedha ya jumla ya TZS 468.50 bilioni (TZS 146.5b, TZS 129.8b na TZS 192.2b mwaka 2010/11, 2011/12 na 2012/13 sawia.

“Kwa ujumla, uwekaji wa vinasaba umeendelea kuleta manufaa yafuatayo: Kuongezeka kwa mapato ya Serikali, kujenga mazingira ya usawa wa ushindani kibiashara miongoni mwa wafanyabiashara ya mafuta, mteja ananufaika kwa kupata bidhaa ya mafuta yenye ubora unaostahili na hivyo kupunguza uharibifu wa mara kwa mara wa mitambo ya magari hususan injector pumps na uwekaji wa vinasaba umefanikisha upatikanaji wa takwimu sahihi za kiwango cha matumzi ya mafuta nchini kwa ajili ya mipango ya maendeleo ya Taifa,” inasema Ripoti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ya mwaka 2014.

 

Chegeni anena

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii inayotaniwa kuwa ni gereza la wafungwa wa kisiasa la Guantanamo, kwani ilikusanya wabunge machachari wengi, Raphael Chegeni anayetuhumiwa kuomba Mfumo wa Bima ya Afya uwapatie wabunge posho badala ya chakula na chai, amezungumza na JAMHURI na kusema hakukuwa na kitu cha namna hiyo.

“Hakuwa na mazingira yoyote ya rushwa. Sasa kama ni rushwa, labda ni chai, maanake tulipewa chai pale. Suala hilo halikuwapo na wala halipo. Na hatuwezi kufanya kitu cha namna hiyo maana tunajua maadili ya kazi yetu… katika hali ya kawaida, haya mambo ni ya kawaida sana sana. Sisi tulikuwa tunakaa pale LAPF, walikuwa wanatupa chai, basi ni kitu cha kawaida. Na hii inakuwa ni arrangement kati ya Bunge na, Kamati zake,” anasema.

Alipohojiwa kwa nini suala hili litokee sasa, wakati Kamati zimekuwa zikifanya kazi bila kushutumiwa miaka yote, akasema asingependa kulisemea kwa undani kwani tayari walikaa kama viongozi wakalijadili kwa kina na wakaelezana ukweli, ila inafahamika tangu mwanzo kuwa wapo wabunge waliokuwa hawataki kujiunga katika kamati hii.

Wabunge wanaotajwa kuwa hawakutaka kupangwa katika kamati hiyo ni pamoja na Zitto Kabwe (ACT) na Hussein Bashe (CCM). Wabunge waliokuwa wajumbe wa hiyo kamati wamehoji imekuwaje Zitto na Bashe wajiuzulu kwa wakati mmoja na barua zao za kujiuzulu ziwe na maneno yanayofanana, kisha wakasema labda walitumia njia ya kuituhumu Kamati wasiyoipenda waweze kujiondoa.

Walihoji mbona Zitto amekwishatuhumiwa mara kadhaa ikiwamo la Escrow na hakujiuzulu, lakini zamu hii wametuhumiwa wengine akaishia kujiuzulu yeye. “Kumbuka ile Kamati yetu ilikuwa ni gereza la Guantanamo. Wale wahalifu wote wa kivita wanafungwa kwenye gereza hilo.

“Sasa wanatokaje kwenye gereza hilo? Sasa lazima watafute mkakati wa tufanyeje, wa kutoka. Aidha, wa kuua wenzao, ili waruke wakimbie au kwa kuweza kutoboa matundu au whatever. Kwa hiyo ni mkakati tukisema kwamba Kamati nzima imetuhumiwa, basi Spika atavunja ile kamati, hivyo unapata nafasi ya kutoka waweze kwenda kwenye Kamati nyingine,” anasema mmoja wa wabunge aliyeomba asitajwe.

 

Zitto ajibu

 Akizungumza na JAMHURI, Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT), Zitto Kabwe, alisema yeye alijiuzulu ujumbe wa Kamati kushinikiza uchunguzi ufanyike na kwa kuwa uchunguzi umefanyika anarejea kwenye Kamati hiyo kuchapa kazi.

Amesema maneno yanayoenezwa kuwa safari zilizopita alituhumiwa hakujiuzulu na kwa nini amejiuzulu awamu hii, anasema ameomba uchunguzi mara tatu Spika wa Bunge akikataa na zamu hii alipochukua hatua ya kujiuzulu kwenye kamati uchunguzi ukafanyika, hivyo hilo limetimiza lengo lake. Zitto anasema Kamati hii inasimamia asilimia 30 ya bajeti ya nchi, hivyo ni lazima aendelee kuwamo.

“Sasa hivi nimesema akaaa, naresign, na wanachunguza,” anasema Zitto. 

Amewataka Watanzania kuepuka kitu alichokiita propaganda zisizo na tija na kusema nchi haiwezi kuendelea kwa utaratibu wa wabunge na watu kuvizia mapato yasiyo halali.

“Nimewaambia wenzangu kwenye kamati juzi. Niliwaambia hata kama mtu una njaa, lazima uangalie, zama zimebadilika. Hizi siyo zama zile, ni zama mpya, lazima uwe makini. Usiendekeze njaa, lazima uwe makini, zama zimebadilika. I told my colleagues (niliwaambia marafiki zangu),” anasema Zitto.

Anasema wakati Rais John Magufuli anapambana kubana matumizi suala la wabunge kuendelea kupokea posho ya Sh 330,000 kwa siku ni kutomsaidia Rais. Anasema tangu wameanza kazi za Kamati kutokana na maelekezo maalumu ya Serikali wabunge hawapokei posho zaidi ya malipo yanayotolewa na Bunge.

 

Bashe anena

 Alipotafutwa na JAMHURI kujibu tuhuma hizo, Bashe amesema: “Sijawahi kuandika barua… Nimeteuliwa kuwa mjumbe wa Kamati ya Maendeleo na Huduma za Jamii, sijawahi kuandika barua ya kuomba kuhamishwa kwenye Kamati. Na nimesema wazi, ninachodemand mimi ni uchunguzi, kuliko hii style tuliyozoea wana-CCM ya funika kombe mwanaharamu apite. Zinakuwapo tuhuma zinaachwa hewani hazifanyiwi uchunguzi.

“Mimi nilichodemand ni Spika kutumia vyombo vya ulinzi na usalama kufanya uchunguzi kama kuna mjumbe yeyote ndani ya Kamati yetu au nje ya Kamati, hata kama ni mimi, hatua za kinidhamu na kisheria zichukuliwe ili kulijengea Bunge heshima. “Na msimamo wangu juu ya suala la kupewapewa viposho hivi, umekuwa wazi hata kwenye Kamati. Tuliwahi kuombwa na CWT wakatuma ujumbe ili wakutane na sisi siku ya wikiendi watulipe posho, mimi nilikuwa wa kwanza kumwomba Makamu Mwenyekiti tusikubali waje ndani ya siku za kazi tunazolipwa na Bunge. Wajumbe waliniunga mkono.

“Nademand uchungzui na sihitaji kuhamishwa Kamati. Kamati hii ni moja kati ya Kamati ambazo zinabeba ajenda muhimu za nchi hii. Inasimamia elimu na afya. Sina mpango wa kuhama. Uchunguzi ukifanyika, na taarifa ikatolewa narejea kwenye Kamati.

“Bunge la 10 wabunge walituhumiwa juu ya suala la rushwa na yakaachwa hivi hivi bila investigation. Inaharibu credibility ya Bunge. Katika hili, msimamo wangu, najua wengi hawatanielewa ndani ya CCM, hasa waliokuwa na kitu kinachoitwa ‘nidhamu ya woga’. Na mimi sijutiii maamuzi niliyochukua ya kumwandikia Spika na nashukuru amechukua hatua na Takukuru imechukua hatua,” amesema Bashe.

 

Mary Mwanjelwa

Mery Mwanjelwa, mbunge mwingine anayetuhumiwa kuomba rushwa ya Sh milioni 100 kutoka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), amezungumza na JAMHURI na kusema: “Hamna kitu kama hicho wewe, labda hayo ni maexagration. Ndiyo nayasikia kwako. Kwa sababu, kule hawakusema hata kiasi, wenyewe walisema tu Shirika la Nyumba… maneno yatakuwa mengi sana.

“Mimi yote namwachia Mungu kwa sababu hapa nilipo sijui kinachoendelea… nimejitahidi kujenga uadilifu wangu kwa muda mrefu. Kwa hiyo hayo yanayotokea sasa hivi ambayo na mimi sielewi chanzo chake, ninamwamini sana Mungu, namwachia Mungu. Mungu atathibitika katika haki. Hilo tu ndilo ninaloweza kusema.

“Na bahati nzuri, wewe unanijua A mpaka Z kwa uadilifu na jinsi gani ninavyoweza kuchapa kazi. Sasa kwenye hilo, kwa sababu namwamini Mungu, naamini Mungu atajidhihirisha tu. Kwa jinsi nilivyo innocent, ninamwachia Mungu athibitishe. And I tell you this Balile from the bottom of my heart (nakwambia haya Balile kutoka kwenye sakafu ya moyo wangu). Mungu ninayemwamini, kama mimi kweli ni innocent, wote wanaojaribu kufanya ya kufanya, Mungu atashughulika nao.

“Kama kuna uadilifu nimeujenga kwa muda mrefu na uchapakazi, halafu mtu anakuja kunidamage kwa sababu anazozijua yeye, labda Mungu tunayemwamini siyo Mungu,” anasema Mwanjelwa.

 

Dk. Kashilillah awaasa wabunge

 Kwa upande wake, Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashilillah, ameiambia JAMHURI kuwa Spika amechukua hatua si kwa sababu ya magazeti kuchapisha taarifa hizo juu ya wabunge, bali kutokana na uchunguzi ulioanza muda mrefu kufuatilia nyendo za wabunge.

Aliwataka wabunge kuweka maslahi ya aifa kwanza, na kwamba

taarifa za kutuhumiwa kupokea au kuomba rushwa zimepatikana

kutoka miongoni mwa wabunge wenyewe na vyombo vya dola

vikazifanyia kazi.

Anasema uchunguzi unaoendelea unaweza usiwe na matokeo mazuri kwa baadhi ya wabunge. 

“Sheria iko wazi. Hawa ikithibitika, wengi wanaweza kuishia gerezani na kupoteza ubunge,” anaonya.

Kifungu cha 28 cha Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge ya Mwaka 1988 kinasema Mbunge akipatikana na kosa la kuomba rushwa, anaweza kutozwa faini ya Sh 20,000 au kifungo cha miaka mitatu jela.

Ibara ya 67 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) inasema bayana kuwa Mbunge anaweza kupoteza sifa ya kuendelea kuwa mbunge iwapo atafungwa jela kwa kipindi kinachozidi miezi sita kutokana na kosa lolote.

Spika wa Bunge, Job Ndugai, baada ya tuhuma hizo kutokea amevunja Kamati za tano za Bunge na kuhamisha wajumbe 27,  na akaelekeza uchaguzi ufanyike upya kwa Kamati zilizopoteza Mwenyekiti na Makamu wake au mmoja wa viongozi hao.

Zipo taarifa kuwa wabunge katika kamati walikopelekwa wabunge wanaotuhumiwa kwa rushwa, wajumbe wake wameanza kuwakataa kwa maelezo kuwa kamati zao si ‘kijiwe’ cha wala rushwa.

 

Ewura wajibu 

Meneja wa Mawasiliano wa Ewura, Titus Kaguo, ameiambia JAMHURI; “Kumekuwa na tuhuma za kupatikana kwa vinasaba mtaani, kwa bei nafuu kabisa, lakini Ewura tumekuwa tukiwaomba wenzetu watuletee angalau tupate pa kuanzia, lakini hakuna hata mmoja aliyeleta.

“Suala la pili, kama vinapatikana hovyo hovyo tu, Ewura ikienda kupima mafuta isingewakamata wafanyabiashara kwani kila mtu angekuwa anaweka na Ewura ikipima inakuta vinasaba viko sawa, ambapo bado transit fuel nyingi sana inauzwa hapa nchini,” amesema Kaguo.

Amesema wanachoomba kwa wafanyabiashara wa mafuta ni kufuata sheria na taratibu za biashra hiyo kwa kuuza mafuta yaliyolipiwa kodi tu na hakuna chombo chochote kitakachowafuata.

Amekiri kuwa maafisa wa Ewura wanatembea na mafuta ya sampuli kwa ajili ya kuwathibitishia wenye vituo ukitokea ubishi na akaitetea kampuni ya Global Fluid International (GFI) ya Israel, kuwa inaheshimika na imebana mianya ya uvujaji wa vinasaba hivyo huenda hilo likawa chimbuko la malalamiko.

Mchambuzi wa masuala kisheria, alisema hoja ya Shabby na wenzake haina mashiko. 

“Kama vinasaba vinauzwa Sh milioni 2, kwa nini Shabby na wenzake wasinunue hivyo vinasaba vya milioni 2 wakaweka kwenye mafuta yao wasubiri kupigwa faini ya Sh milioni 25?” anahoji mchambuzi huyo.

Anasema wauza mafuta hawavitaki vinasaba na wananchi wa kawaida hawana matumizi navyo, hivyo kwa akili ya kawaida havina soko na wauza mafuta wanataka viondolewe waweze kumwaga mafuta yasiyolipiwa kodi kwenye vituo vyao.

By Jamhuri