Kurasa za Ndani
MOROGORO
Na Aziza Nangwa
Taasisi ya Tretem Network of Schools Limited imemuomba Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angelina Mabula, kuingilia kati kitendo cha Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Morogoro, Frank Minzikuntwe, kutaka kumega eneo lao kisha apewe mtu mwingine.
Akizungumza na JAMHURI hivi karibuni, Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Julius Chami, amesema eneo hilo wanalimiliki kihalali lakini Frank amewaandikia barua ya siku saba kutaka hati ibadilishwe na limegwe kipande.
Amesema kitendo cha kumwachia mvamizi eneo lao wamekipinga hadi wakaenda mahakamani na ulitolewa uamuzi waendelee na ujenzi na wavamizi waondoke na wakaondoka, lakini mmoja anayekingiwa kifua na Frank amebaki ndiye anawashinikiza waachie eneo hilo.
Pia amesema eneo hilo walilipata kihalali kupitia Manispaa ya Morogoro baada ya kubadilishana nao kiwanja chao kilichokuwa Kata ya Kilakala, eneo la Kigurunyembe lenye ekari tano ili wapewe mbadala kwa ajili ya kupisha ujenzi wa shule ya sekondari ambayo kwa sasa inafanya kazi.
Amesema kiwanja hicho kilitolewa kwa serikali kwa matumizi ya umma na wao walikinunua mwaka 1995 na mwaka 1997 walianzisha Chuo cha Uandishi wa Habari Morogoro (MSJ) kikiwa chini ya mwavuli wa Tretem.
Vilevile amesema baada ya kujenga vyumba vitatu na wakati wanaendelea na ujenzi alikuja Diwani wa zamani wa Kata ya Kilakala, Anthonia Sanga, ambaye aliwaomba eneo hilo kwa ajili ya kujenga shule ya sekondari ya kata na wakafanya mazungumzo wakiwamo watu wa manispaa.
Amesema baada ya mjadala wa muda mrefu walikubali kupewa eneo mbadala lililopo Tungi.
“Tuliamua kukubali kwenda mbali ya mji kwa sababu ya kuzingatia masilahi ya umma, hasa watoto wasiende mbali.
“Sababu kubwa ni eneo lao halisi lililokuwa lijengwe sekondari, lilikuwa kata nyingine, kwa hiyo tuliona hoja yao ina mashiko, tulikubali kuwaachia kwa makubaliano maalumu ya kisheria yaliyosimamiwa na maofisa ardhi wa manispaa,” amesema.
Aidha, amesema baada ya hapo viwanja hivyo vilibadilishwa kisheria na wao wakapewa hati ya ofa na Manispaa ya Morogoro inayosomeka Plot 477, Kitalu E, Tubuyu, Postcode 67122 Tungi Morogoro na kiwanja kina ukubwa wa hekta za mraba 2.697, kimewekwa vigingi namba BAJ321-329 na kilikuwa na hati ya umiliki wa miaka 99.
Amesema baada ya kupewa kiwanja mbadala katika eneo jipya la Tungi hawakufanya ujenzi kwa kipindi hicho.
“Wakati tumeacha bila kujenga tukitafuta fedha, maofisa ardhi wa manispaa wakaanza kuingiwa tamaa na kukimega kipande cha eneo letu na kuuza. Sisi hatukuwa na taarifa, tukakuta watu wamejenga katika eneo letu, tulichukua hatua ya kuwakamata na kuwapeleka mahakamani.
“Mahakama ya Mwanzo nao wakatushusha katika Baraza la Ardhi la Wilaya, huko mwenyekiti akatoa uamuzi kiwanja kipimwe upya, sisi tulikataa na kukata rufaa kwenda Mahakama Kuu Kitengo ya Ardhi kupinga kiwanja chetu kumegwa.
“Na tulitaka kiwe vilevile kama awali, kwa sababu tuliamua kuacha kiwanja chetu cha mjini, tulikwenda kijijini Tungi kuanza upya, pia tukaacha jengo na vifaa vya ujenzi katika eneo hilo kwa manufaa ya umma,” amesema.
Katika hatua nyingine, amesema Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi – Morogoro iliamuru kiwanja chao wapewe vilevile na wavamizi wahame na kuwalipa fidia ya Sh milioni 10.
Amesema baada ya muda waliporudi kuendeleza eneo hilo, wakatokea watu wa kanisa nao wakadai kuuziwa eneo hilo na maofisa ardhi wa Manispaa ya Morogoro kabla yao.
“Kanisa hilo lilitupeleka mahakamani na sisi lengo letu tulitaka manispaa ishirikishwe katika kesi ili itoe kauli kiwanja ni cha nani, lakini haikuwa hivyo, badala yake manispaa iliomba wote watatu tuzungumze nje ya mahakama.
“Mwisho, manispaa walikiri kufanya uovu huo na wakatuamuru sisi tuendelee na ujenzi na shirika hilo walipewa kiwanja mbadala, hivyo manispaa ikalazimika kuandaa hati mbili,” amesema.
Pia amesema wakiendelea kuwatoa watu katika kiwanja chao, manispaa ilikata sehemu ya eneo lao na kumpatia mvamizi mmoja ambaye hadi sasa bado yupo akidai amri ya mahakama si halali.
“Baada ya mvamizi kuendelea kukaa katika eneo letu huku tukiendelea na ujenzi, tulikwenda mahakamani kukazia hukumu ili aondoke, lakini yeye alikwenda kwa Frank ambaye naye ametuandika barua ya amri, inayotutaka kwenda manispaa kubadilisha hati yenye kasoro ya hekta za mraba 2.166 ili kiasi kinachobaki tumwachie mvamizi.
“Kwa kweli amri hiyo hatukuridhika nayo, tukaandika barua kwa waziri mwenye dhamana ili atusaidie kutatua mgogoro wa kudhulumiwa kiwanja chetu na kamishna akishirikiana na maofisa ardhi wa manispaa,” amesema.
Aidha, amesema Ofisa Ardhi wa Manispaa, Valency Huruma, amesema ni kweli manispaa ilitoa kiwanja kwa Tretem lakini suala la kupunguza eneo wao hawana mamlaka ila mwenye uwezo ni kamishna wa ardhi wa mkoa.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Tungi, Ibrahim Chombo, amesema awali eneo hilo walipewa Tretem ili kujenga chuo na kuhusu wavamizi amesema hawakufuata sheria na wameuziwa na madalali.
Naye Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Tungi, Ramadhani Kambi, amesema eneo hilo ni la Tretem na lina vigingi na wanalimiliki kihalali na wavamizi waliuziwa na matapeli.
Majirani
Mwanaidi Rajabu amesema eneo hilo ni la MSJ kwa miaka mingi na linatambulika. Anahoji, waliovamia wamepata wapi ruhusa?
Naye Joseph John amesema anafahamu muda mrefu eneo hilo ni la Tretem na si la mwingine.
Kwa upande wake, msimamizi wa eneo hilo, Mohamed Juma, amesema amekuwa akipelekwa polisi na mvamizi kwa sababu anataka aendelee kukaa katika eneo hilo wakati si lake.
Kamishna ajibu
Frank amekiri kutoa barua ya kuitaka Tretem kubadilisha hati ndani ya siku saba lakini amedai ameshaagiza manispaa kuhakiki upya na kama wana haki wapewe, na amesema shauri hilo limekwenda wizarani na wanasubiri uamuzi.
Diwani wa zamani
Sanga amesema eneo hilo ni la Tretem na wana haki ya kuachiwa kiwanja chao cha awali kwa sababu wamewasaidia watu wa Kilakala.
“Tulikuwa hatuna eneo la kujenga shule, kwa jitihada zangu nilikwenda kuwabembeleza Tretem wahame mjini na kwenda Tungi.
“Mwisho, walivyokubali tuliwapeleka kule kisheria na wakapewa hati halali na wameacha kiwanja cha thamani kwenda kijijini, naomba waachwe kwa sababu wametusaidia watoto walikuwa waende mbali kusoma, lakini wao wametusaidia,” amesema.
Mombasa
Na Dukule Injeni
Hakuna ubishi, urais Kenya ni mbio za farasi wawili licha ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kupitisha majina manne ya wanaosaka kumrithi Rais Uhuru Kenyatta kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Agosti 9, mwaka huu.
Naibu Rais, William Ruto wa muungano wa Kenya Kwanza na aliyewahi kuwa Waziri Mkuu, Raila Odinga, wa muungano wa Azimio la Umoja One Kenya Alliance ndio wanaochuana vikali.
Wengine wawili ambao wanatamba kuwapa wakati mgumu Odinga na Ruto debeni ni Profesa George Wajackoyah wa Chama cha Roots na David Wahiga wa Chama cha Agano.
Hata hivyo ni Wajackoyah ambaye amegonga vichwa vya habari tangu aweke wazi nia ya kuwania urais kisha kuchukua fomu na kuidhinishwa na IEBC.
Mgombea huyo wa Chama cha Roots amejizolea umaarufu hususan kwa kutetea ulimaji wa bangi na kusema endapo atachaguliwa Agosti 9 atatumia zao la bangi kuiingizia Kenya fedha nyingi za kigeni atakazozitumia kulipa madeni.
Lakini cha kushangaza ni kauli aliyoitoa hivi karibuni akiwa Kisumu ambayo ni ngome ya Odinga na kuibua maswali kama kweli Wajackoyah ana nia ya dhati kuwania urais au ni mradi wa Odinga?
Akiwa kwenye kampeni zake eneo la Kondele jijini Kisumu, Profesa Wajackoyah alidokeza mpango wa siri alioingia na Odinga ambapo miongoni mwa mambo mengi ni kuwa yeyote atakayeshinda atafungua milango ya serikali yake kwa mwingine.
Je, kuna uwezekano wa uwepo wa makubaliano kabla na baada ya uchaguzi kati ya mgombea urais wa Azimio la Umoja One Kenya, Odinga, na mwenzake wa Chama cha Roots, Wajackoyah?
Ukiacha umaarufu walionao Ruto na Odinga, uwepo wa Wajackoyah na hususan kauli zake zimewachanganya wengi wasijue kama yeye ni mradi wa Odinga au mwanasiasa aliyekuja kuvuruga na kuwaharibia vinara wawili kwenye uchaguzi hivyo kuwanyima ushindi raundi ya kwanza.
Kauli ya Wajackoyah tena akiwa katika ngome ya Odinga imetafsiriwa ni ya kisiasa, yenye nia ya kuwashawishi wapiga kura wamsikize, ukizingatia alidai anamsafishia njia Odinga kutinga Ikulu.
Alikwenda mbali na kusema ametumwa na Odinga kuwasilisha ujumbe kwa wafuasi wake na kudokeza kuhusu uhusiano wake na waziri mkuu huyo wa zamani, ikiwamo uwezekano wa wawili hao kufanya kazi pamoja katika siku za usoni.
Kiongozi huyo wa Chama cha Roots pia alisema ushindi uwe wake au wa Odinga utakuwa ni ushindi kwa watu wa Magharibi mwa Kenya.
Wajackoyah ambaye ni wakili kitaaluma, alidai alikuwa muonja chakula mkuu wa Makamu wa Rais wa Kwanza, marehemu Jaramogi Oginga Odinga.
“Nitakaposhinda urais, nitakaa na Odinga katika chumba cha mkutano nikiwa na lengo la kufanya kazi naye baada ya uchaguzi,” amesema kiongozi huyo wa Roots Party ambaye mgombea mweza wake ni mwanamke Justina Wamae.
Wajackoyah katika mkutano huo kwenye kambi ya Odinga, alimtetea waziri mkuu huyo wa zamani, akiwataka wale wanaoendekeza kumshambulia kiongozi huyo wa Chama cha ODM kuacha.
Aliyekuwa analengwa na Wajackoyah ni Naibu Rais, Ruto, na imekuwa kawaida kwa kiongozi huyo wa Roots Party katika mikutano yake ya kampeni kumkosoa Ruto zaidi ya Odinga.
“Nimekuja nyumbani kwa baba na nikiwa njiani kuja hapa, niliambiwa kuwa kama utakwenda Kisumu, usimtukane Raila kwa sababu nitapata wakati mgumu. Kuna huyu kijana mmoja kutoka Sugoi (akimaanisha Ruto), ambaye imekuwa kawaida yake kumtukana baba akija hapa. Mpigieni kelele, mumwambie aachane na baba anapokuja hapa,” amesema.
Wajackoyah amesema aliamua kuwa mgombea urais katika uchaguzi wa Agosti 9, mwaka huu kupitia Chama cha Roots baada ya juhudi zake kujiunga na vyama vikuu kama vile ODM, ANC na Ford-Kenya kukataliwa.
*Nyampala auawa akidaiwa ‘kuiba’ mahindi ya Mkuu wa Gereza
*Mpambe wake anusurika kifo kwa kipigo, alazwa ICU Muhimbili
*RPC agoma kuzungumza, aukana mkoa wake akidai yeye ni RPC Mtwara
Dar es Salaam
Na Alex Kazenga
Wakati taifa likifikiria namna sahihi ya kukomesha mauaji ya mara kwa mara yanayotokea nchini, hali si shwari hata ndani ya kuta za majengo yanayolindwa na vyombo vya dola.
Kwa takriban miezi tisa sasa, kumekuwa kukiripotiwa matukio ya watu kuuana; wakati mwingine wana ndoa, watu wenye uhusiano wa karibu na hata ndugu wa familia moja kiasi cha viongozi wa dini na wa serikali kuwataka watu kurejea kwenye mafundisho ya dini na kuwa wacha Mungu.
Na sasa, askari wa Jeshi la Megereza wa Liwale mkoani Lindi wamejikuta katikati ya tuhuma nzito, ikiwamo kusababisha kifo cha mfungwa mmoja.
JAMHURI linafahamu kwamba kifo cha mfungwa huyo Na. 70/2020 aliyekuwa nyampala, Abdalah Ngatumbara, kilitokea Juni 8, mwaka huu, baada ya yeye na mpambe wake kutembezewa kipigo na askari magereza, wakilazimishwa kuwataja watu walioiba mahindi ya Mkuu wa Gereza.
Kwa bahati nzuri, mpambe wa Ngatumbara, Siaba Mbonjola (Na. 76/2021), alinusurika kifo na sasa amelazwa katika chumba kinachohitaji uangalizi maalumu (ICU), Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI).
Awali, wafungwa hawa wawili walipelekwa Hospitali ya Wilaya ya Liwale ambapo wataalamu walithibitisha kifo cha Ngatumbara, baadaye Mbonjola akahamishiwa Hospitali ya Mkoa ya Sokoine na kisha kupelekwa MOI.
“Ukweli wa tukio hili unafichwa. Lakini kwa kifupi Mkuu wa Gereza la Liwale anahusika. Yeye ndiye aliyeamuru Ngatumbara na mwenzake wateswe hadi watakapotaja wezi wa mahindi,” amesema mtoa taarifa wetu kutoka ndani ya Gereza la Liwale (jina linahifadhiwa).
Inadaiwa kuwa wizi wa mahindi ya Mkuu wa Gereza, Gilbert Sindani, ulitokea wakati wafungwa wakivuna mahindi kutoka katika shamba la magereza.
“Mahindi yaliyoibwa yalikuwa yamekusanywa barabarani tayari kusombwa na magari kupelekwa ghalani na mengine kwa Afande Sindani ambaye siku hiyo alikuwa safarini Dar es Salaam.
“Akatumiwa taarifa za kuibwa kwa mahindi yake yaliyovunwa. Aliporejea Liwale, akamuita msaidizi wake na kuhoji juu ya taarifa za wizi. Akajibiwa kuwa zipo lakini hazikuwa zimefanyiwa uchunguzi,” amesema mtoa taarifa.
Anasema hadi wakati huo hakukuwa na yeyote anayetuhumiwa kwa sababu hakuna aliyebainika kupelekewa au kukutwa na mzigo wa mahindi.
Taarifa hizo hazikumridhisha Sindani, ambaye kesho yake, Juni 8, mwaka huu, akawaita nyampala wa gereza na mpambe wake na kuwataka wampe taarifa kamili. Wakamjibu kuwa hawajui chochote.
“Palepale akaanza kuwapiga akiwataka wamtaje aliyechukua mahindi na amechukua kiasi gani. Alipochoka, akaona haitoshi, akawaita askari wawili; Sajenti Yusuph Selemani na Koplo Fadhili Mafowadi, wamsaidie kuwapiga hadi watakapotaja wezi,” amesema.
Kipigo hicho hakikuwafurahisha askari wengine ambao waliwazuia Sajenti Yusuph na Koplo Fadhili wasiendelee kuwapiga, wakihoji iwapo wana uhakika kweli kuna wizi umetokea; wengi wakiamini kuwa uchache wa mavuno ya mwaka huu ndiyo sababu ya kudhani kwamba wizi umefanyika.
Baada ya Sindani kubaini kuwa Ngatumbara na Mbonjola wameumizwa sana, akaondoka. Muda mfupi baadaye akarudi na kuwapakia kwenye gari kuwapeleka hospitalini ambako madaktari walibaini kuwa tayari Ngatumbara alikuwa amekwisha kufariki dunia, na hata matumaini ya kupona kwa Mbonjola ni madogo.
Madaktari wakashauri tukio liripotiwe polisi na kupewa ‘PF3’ ili taratibu za matibabu kwa Mbonjola zifanyike.
Ngatumbara alikuwa anatumikia kifungo cha miaka mitano jela kwa kosa la kukutwa na nyama ya nguruwe pori.
Taarifa za tukio zavuja
Jitihada za Sindani kuficha tukio hilo zilishindikana baada ya wasamaria wema ndani ya Gereza la Liwale kuwapa taarifa ndugu wa Ngatumbara, akiwamo Diwani wa Mbaya, kata anakotokea.
Baada ya kupata taarifa walifika hospitalini na kuutambua mwili wa ndugu yao; lakini hawakuridhishwa na sababu walizopewa za kifo chake, wakaenda kwa Mkuu wa Wilaya kutafuta ufafanuzi.
Diwani, askari wanena
Diwani wa Mbaya, Ali Nassoro, analithibitishia JAMHURI kuwa Ngatumbara amefia mikononi mwa Mkuu wa Gereza na kwamba ana shaka kuwa ni kutokana na kipigo.
Anasema baada ya kupata taarifa aliwasiliana na vyombo vingine vya usalama kisha yeye na ndugu waliushuhudia mwili wa Ngatumbara ukiwa umewekwa chumba cha kuhifadhia maiti ukiwa umevunjwa miguu huku ukiwa umeathirika sana mgongoni.
“Hata daktari aliyekuwapo alithibitisha hilo,” anasema Nassoro.
Mmoja wa askari wa Gereza la Liwale (jina tunalihifadhi), anasema kisasi ndicho chanzo cha kifo cha Ngatumbara.
“Kuna watu ambao Mkuu wa Gereza hapatani nao. Kuna askari anawatafutia sababu awafukuzishe kazi. Ni bahati mbaya kuwa askari hao hawakutajwa na Ngatumbara na mwenzake,” amesema na kuongeza kuwa kuendelea kuwa huru kwa Sindani kunaharibu uchunguzi.
Tayari polisi inawashikilia Sajenti Yusuph na Koplo Fadhili ambao wapo mahabusu ya Mkoa wa Lindi wakati uchunguzi ukiendelea.
Simulizi ya ndugu
Mkazi wa Mbaya, Said Mohamed, anasema Ngatumbara alizikwa Juni 10, mwaka huu na kwamba ameacha mjane na mtoto mmoja.
Anasema awali taarifa kuwa Ngatumbara ana hali mbaya walizipata kutoka kwa mtu wasiyemfahamu, aliyewaeleza kuwa amemuona Hospitali ya Wilaya ya Liwale.
“Muda mfupi baadaye tukapigiwa simu na Diwani (Nassoro) akatueleza kuhusu tukio hilo. Siku ile afya yangu haikuwa nzuri, hivyo nikampigia simu Kassim Arafi (ambaye ni ndugu yake) nikamwambia aende hospitalini kuhakiki taarifa,” amesema.
Anasema alipofika hospitalini, Arafi alizuiwa kumuona Ngatumbara kwa maelezo kuwa akatafute kibali kutoka kwa Mkuu wa Gereza.
Kutokana na kizingiti hicho, Arafi aliamua kuulizia taarifa za ndugu yake kutoka kwa watu wengine, ndipo akaelezwa kuwa alifikishwa hospitalini akiwa na mfungwa mwingine, lakini yeye amefariki dunia.
Kutokana na utata wa taarifa na kwa kushauriana na diwani, Mohamed na ndugu zake wakaona ni vema kuwasiliana na Mkuu wa Wilaya aliyewataka wafike ofisini kwake siku inayofuata.
“Tukaenda kuzungumza naye. Akakiri kuwa anazo taarifa za tukio na kuwa amewasiliana na Mkuu wa Mkoa wa Lindi atume vyombo vya dola kufanya uchunguzi.
“Siku iliyofuata tukaitwa na Mkuu wa Gereza akisema tunahitajika kwenda Kipule liliko gereza tukapate maelekezo. Sisi tukamwambia hatuna usafiri. Akatutumia gari. Mimi, Arafi na Omari Mchite tukaenda gerezani ambako tuliwakuta maofisa wa vyombo vya ulinzi na usalama,” amesema.
Miongoni mwa maofisa waliokuwapo ni Mkuu wa Magereza wa Mkoa wa Lindi. Sindani akawaeleza ndugu wa Ngatumbara kuwa kifo cha ndugu yao kimetokana na shinikizo la damu (pressure).
Mohamed anasema walipohoji zaidi, wakaelezwa kuwa katika gereza hilo kuna kawaida ya kutokea wizi wa mahindi na mara nyingi wafungwa wanapoyasomba kutoka shambani hupotea.
“Sindani akadai kuwa askari wasimamizi ndio watekelezaji wa aina hiyo ya wizi. Akatuambia kuwa siku ya tukio yeye alikuwa amesafiri, akamuacha msaidizi wake afuatilie wizi wa mahindi unaofanywa na askari magereza kwa kushirikiana na wafungwa,” amesema.
Mkuu wa Gereza, mbele ya maofisa wengine kutoka mkoani, akawaambia kuwa aliporudi alipewa orodha ya askari wanaohusika, lakini hakutaja majina yao.
Sindani akaendelea kusema kuwa kesho yake aliitisha gwaride rasmi likijumuisha wafungwa wote na askari magereza, na kutamka kuwa wezi wa mahindi wamekwisha kufahamika, akiwataka kutorudia tabia hiyo.
Baada ya onyo hilo, Sindani anasema alipanda gari lake na kuelekea mjini na wakati akiwa njiani ndipo akapigiwa simu na msaidizi wake kumpa taarifa za Ngatumbara kuzidiwa, kupelekwa zahanati, na kwamba walikuwa wanaomba kibali apelekwe Hospitali ya Wilaya.
“Akasema kuwa msaidizi wake alitoa kibali, Ngatumbara akapelekwa hospitalini. Nako hali ikazidi kuwa mbaya hadi akafariki dunia,” amesema Mohamed.
Mohamed na ndugu zake wakayapokea maelezo ya Sindani, wakisema bado hawajaridhika kuwa kifo cha Ngatumbara kilisababishwa na shinikizo la damu.
Baadaye walipata kibali cha Mahakama cha kuufanyia uchunguzi mwili wa ndugu yao; uchunguzi uliofanywa na daktari akiambatana na maofisa wa vyombo vingine vya usalama.
“Ikagundulika kuwa mguu mmoja umevunjwa, mshipa wa nyuma wa mguu mwingine umechanika huku damu ikiwa imeganda maeneo ya mikononi,” amesema.
Taarifa ya daktari, kwa mujibu wa Mohamed, inathibitisha kuwa hakufariki dunia kutokana na shinikizo la damu.
“Daktari alihoji iwapo wakati Ngatumbara na mwenzake wakipelekwa hospitalini walipata ajali ya gari. Mkuu wa Gereza akajibu kuwa hakukuwa na ajali yoyote. Familia tukajua moja kwa moja ndugu yetu kafa kutokana na kupigwa,” amesema Mohamed.
Baada ya hapo wakaombwa kuchukua mwili wa ndugu yao kwenda kuusitiri, wakiahidiwa kuwa hatua zaidi za kisheria zitachukuliwa kwa wote waliohusika.
JAMHURI, limemtafuta Mkuu wa Gereza la Liwale, Sindani, kupata ukweli wa tukio hilo, lakini kwa nyakati tofauti amekwepa kwa makusudi kuzungumza.
Mkuu wa Magereza Mkoa (RPO) wa Lindi, Felscheme Massawe, naye amekataa kuzungumzia tukio hilo.
“Taasisi unayotaka nizungumzie ni taasisi ya usalama, siwezi kuzungumza na wewe wakati sikujui, juzi tu nimetapeliwa kwa njia ya simu, naogopa usije kuwa utapeli kama niliofanyiwa,” amesema Massawe.
Kwa upande mwingine, Mkuu wa Wilaya ya Liwale, Judith Nguli, anakiri kupokea taarifa za kifo cha mfungwa lakini naye hayupo tayari kutolea ufafanuzi wa kina akidai suala hili limo katika uchunguzi.
“Yanasemwa mengi, siwezi kusema kafanywa nini hadi akafariki dunia. Serikali inazidi kufanya uchunguzi kwa kina, kwa vile vyombo vya usalama vinachunguza, tuvipe muda vitakuja na ripoti yenye taarifa za uhakika,” amesema DC Judith.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa (RPC) wa Lindi, Mtatiro Kitinkwi, hakutaka kulizungumzia tukio hilo akidai yeye si RPC wa Lindi ni RPC wa Mkoa wa Mtwara.
“Unataka nikupe taarifa za mkoa usionihusu! Labda nikusaidie kukupa namba za simu za RPC wa Lindi, huyo atakupa ufafanuzi,” amesema Kitinkwi.
Hata hivyo, RPC Kitinkwi hakutuma namba ya simu ya ‘RPC wa Lindi’. JAMHURI linafahamu kuwa hadi mwishoni mwa wiki iliyopita, yeye alikuwa bado ni RPC Mkoa wa Lindi.
DAR ES SALAAM
Na Andrew Peter
Mabingwa mara 28 wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga, sasa wanahitaji kushinda mechi nne ili kumaliza msimu na rekodi ya kutokufungwa.
Yanga ilitangaza ubingwa wa ligi wiki iliyopita baada ya kuifunga Coastal Union mabao 3-0 na kufikisha pointi 67 ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote.
Ila Yanga wanapaswa kushinda mechi tatu zilizobaki pamoja na ile ya fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam dhidi ya Coastal Union ili kuivunja rekodi ya Simba (2009) na Azam (2014) walipotwaa ubingwa wa ligi bila kufungwa.
Hakuna shaka Yanga msimu huu ilijipanga vizuri tangu mwanzo wa msimu na kuweka mikakati imara kuhakikisha wanamaliza utawala wa Simba wa misimu minne ya kunyakua mataji yote ya ndani.
Yanga chini ya Mwenyekiti, Dk. Mshindo Msolla na wadhamini GSM, waliamua kuziba masikio kwa mambo ya nje ya uwanja, hasa kelele za mashabiki na kumpa nafasi Kocha raia wa Tunisia, Nasreddine Nabi na benchi lake kutimiza majukumu yao kwa uhuru.
Nabi amefanya mabadiliko makubwa kwa uchezaji wa Yanga katika msimu huu wakionekana kucheza pasi nyingi na kujiamini huku akitoa nafasi kwa nyota wengi kuonyesha uwezo wao.
Siri kubwa ya mafanikio ya Yanga ni ubora wa safu yake ya ulinzi. Ngome hiyo chini ya uongozi wa kipa kutoka Mali, Djigui Diarra na nahodha Bakari Mwamnyeto, imeruhusu mabao saba tu katika michezo 27, ikifuatiwa na safu ya ulinzi ya Simba iliyoruhusu mabao 12 katika mechi 26 walizocheza.
Uimara wa safu ya ulinzi umeifanya Yanga kuwa na uwezo wa kulinda ushindi wake wa aina yoyote ilipoupata, jambo lililoleta amani hata kwa wanachama na mashabiki waliokuwa wakijitokeza kwa wingi viwanjani kuishuhudia timu yao.
Mbali na safu ya ulinzi, pia kiungo mkongwe, Khalid Aucho (Dokta wa Mpira) na mshambuliaji Fiston Mayele wamekuwa na mchango mkubwa katika mafanikio ya mabingwa hao wa kihistoria.
Aucho ni injini muhimu katikati akiwa na uwezo wa kuituliza timu na kuchezesha vizuri wenzake. Alipokuwa akikosekana raia huyu wa Uganda, ni wazi ulikuwa unaiona safu ya kiungo ya Yanga inayumba.
Mshambuliaji Mayele ametimiza jukumu lake kwa asilimia 100 akiwa amefunga mabao 16. Hadi sasa ndiye kinara wa ufungaji, mbali ya kufunga pia ametengeneza mabao manne.
Mayele katika mechi tatu zilizosalia atakuwa na kazi moja tu; kuhakikisha anafunga kila mechi ili kunyakua kiatu cha dhahabu anachogombea na mshambuliaji wa Geita Gold, George Mpole, mwenye mabao 15 hadi sasa.
Simba, Azam zaibeba
Waswahili wanasema: “Unamsifu ana mbio… anayemkimbiza ni nani?”
Ndilo swali tunalopaswa kujiuliza kwa sasa. Wakati Yanga wanapata sifa hizo, washindani wao wakubwa katika mbio za ubingwa Simba na Azam walikuwa na hali gani?
Hakuna ubishi kwamba Yanga imenufaika sana na udhaifu wa wapinzani wao msimu huu. Simba waliokuwa mabingwa watetezi tangu mwanzo wa msimu baada ya mdhamini na aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini atangaze kujiweka kando, hali ya timu ilipoteza mwelekeo.
Uamuzi wa Mohamed Dewji ‘Mo’ kujiweka kando ilikuwa ni habari njema kwa Yanga, maana ndiye mtu aliyewasumbua kwa miaka minne ya kukaa bila taji, huku timu yake ya Simba ikipoteza dira kidogo kidogo uwanjani na kushuhudia mabingwa wakimaliza msimu mzima bila kukaa kileleni mwa ligi.
Wakati Simba ikipotea hivyo, matajiri wa Chamazi, Azam FC, nao walianza vizuri ligi, lakini majeraha ya nyota wake Mzimbabwe Prince Dude pamoja na uamuzi wa kumtimua kocha ni wazi kulionekana kuiyumbisha timu.
Azam pamoja na kuwa na wachezaji wengi nyota, ni moja ya timu zilizofungwa mabao mengi, 27, hadi sasa, huku ikipoteza mechi tisa za ligi. Pigo kubwa kwao ni kuondolewa katika nusu fainali ya Kombe la ASFC na Coastal Union.
Udhaifu wa Simba na Azam umeisaidia Yanga kukusanya pointi nane kutoka kwao, wakitoka suluhu mara mbili dhidi ya watani wao wa jadi huku wakishinda mara mbili dhidi ya Wanalambalamba.
Nabi ajipanga upya
Rekodi za Yanga katika mashindano ya kimataifa ni wazi ndicho kitu pekee kinachomtesa Kocha wao Nadi, pamoja na mashabiki wa mabingwa hao wapya wakati msimu ukielekea mwishoni.
Tayari mashabiki wa Simba wanawakebehi kwa kusema Yanga itakwenda kutia aibu taifa katika mashindano ya kimataifa msimu ujao.
Ni wazi Kocha Nabi anapaswa kubadilisha aina ya uchezaji wa timu yake ili kuendana na kasi ya mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, la sivyo aibu ya kuondolewa mapema itawakuta.
Yanga pamoja na kuchukua ubingwa bila kupoteza mchezo, ni timu inayocheza kwa kasi ndogo, hasa inapofanya mashambulizi yake, jambo ambalo litawapa wakati mgumu katika kufanikisha ndoto yao ya kucheza hatua ya makundi kutokana na aina ya ushindani.
Kocha Nabi anasema: “Tutakapokuwa na timu bora ya mashindano ya CAF, moja kwa moja tutakuwa na timu nzuri ya kucheza Ligi Kuu. Ndoto yangu haitofautiani sana na uongozi wa klabu, wote tunataka mafanikio makubwa msimu ujao.”
Hiyo itafikiwa iwapo watafanya usajili kwa kuongeza wachezaji wengi wenye kasi, pia kuitengeneza safu bora ya ushambuliaji itakayoweza kufunga mabao mengi nyumbani na ugenini.
Pia, ili kufanikiwa katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa ni lazima Yanga wakubali kuiga mazuri ya Simba ya kuhakikisha hawapoteza kizembe kwenye uwanja wa nyumbani, kwani ushindi wa nyumbani umekuwa ni nguzo muhimu ya kufanya vizuri katika mashindano ya kimataifa.
0655 413 101
KATAVI
Na Walter Mguluchuma
Chama cha NCCR-Mageuzi mkoani hapa kimeunga mkono maazimio ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho kumsimamisha uenyekiti James Mbatia na makamu wake, Angelina Mtahiwa.
Akitoa tamko la chama la mkoa, Kamishna wa NCCR Mkoa wa Katavi, Rajabu Makana, amelaani kundi linalomuunga mkono Mbatia lililojaribu kuwashawishi viongozi wa mikoa mbalimbali kupinga uamuzi uliotolewa na Halmashauri Kuu.
Akizungumza baada ya kikao cha Halmashauri Kuu ya NCCR Mkoa wa Katavi kilichohudhuriwa na viongozi wa majimbo matano mkoani hapa, Makana amesema Mbatia, aliyesimamishwa uongozi Mei 21, mwaka huu, amekuwa akituhumiwa kutumia vibaya mali za chama.
“Mbali na tuhuma nyingine, pia amekuwa akishindwa kufanya kazi na viongozi wenzake na wamesimamishwa mpaka Mkutano Mkuu utakaposikiliza utetezi wao,” amesema.
Amesema kuna watu wanazunguka mikoani wakiwafuata wajumbe walioshiriki kupitisha uamuzi ngazi ya taifa ili wasaini nyaraka za kukana ushiriki wao.
“Kitendo hiki si sahihi. Kama viongozi hawa ni wasafi, wasubiri Mkutano Mkuu! Kuanza kushawishi wajumbe ni kuongeza makosa na kudharau vikao halali vilivyotoa uamuzi,” amesema.
Mwenyekiti wa NCCR Jimbo la Mpanda Mjini, Abdul Sigela, amesema akiwa kiongozi wa chama wa muda mrefu, anaunga mkono uamuzi wa Halmashauri Kuu ya Taifa, akiomba Mkutano Mkuu uitishwe haraka kumuidhinisha mwenyekiti mpya.
“Iwe hivyo ili kutoa nafasi kwa chama kuendelea kufanya kazi na kujiandaa kwa uchaguzi ujao wa Serikali za Mitaa na Uchuguzi Mkuu wa 2025,” amesema Sigela.
Kauli hiyo inaungwa mkono na Mwenyekiti wa chama hicho Wilaya ya Tanganyika, Muliton Mvilabo, akiwapongeza wajumbe walioshiriki kumwondoa Mbatia madarakani.