#Awaasa kusaidia miradi ya uwekezaji nchini hususan sekta ya umeme

# NMB yaipongeza Serikali kwa kuwa na Uchumi imara

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati,Dkt. Doto Biteko leo tarehe 24 Novemba, 2023 amekutana na kufanya mazungumzo na Menejimenti ya Benki ya NMB jijini Dar es Salaam.

Pamoja na mambo mengine Dkt. Biteko ameipongeza benki hiyo kwa kuwa wabunifu kwenye utoaji huduma pamoja na kuwekeza kwenye teknolojia.

Aidha, Dkt. Biteko ameiasa NMB kuangalia uwezekano wa kusaidia uwekezaji wa miradi mbalimbali ya umeme hususan ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji wa umeme, ili kuwezesha upatikanaji umeme wa uhakika.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna amesema kuwa, lengo la ziara hiyo ni kumpongeza Dkt. Biteko kwa kuteuliwa na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati.

Amesema kuwa, kwa sasa uchumi wa nchi umeimarika na unakua kwa asilimia 5.3 ambapo Tanzania ni moja ya nchi bora kwenye uwekezaji kwa Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla.

NMB ni moja Kati ya benki zinazofanya vizuri kwenye soko la benki ambapo ina jumla ya matawi 230 na wakala elfu 24 nchini.