Na Byarugaba Innocent,JamhuriMedia, Kibaha

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Dkt.Rogers Shemwelekwa amefanya kikao rasmi na watumishi kwa lengo la kufahamiana, kujitambulisha na kutoa mwelekeo kiutendaji.

Dkt.Shemwelekwa aliyeteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan tarehe 13 Machi, 2024 kuwa Mkurugenzi wa Kibaha Mji amesifu mifumo mizuri iliyowekwa na watangulizi wake akiwemo Bi.Jenifa Omolo ambaye kwa Sasa ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mhandisi Mshamu Munde aliyehamishiwa Halmashauri ya Nanyamba na kwamba kazi yake Sasa ni kutengeneza kemia mpya itakayotumika ili kufikia malengo ya Serikali ya kuwahudumia wananchi.

Dkt.Shemwelekwa amewataka watumishi kutoa huduma Bora kwa wananchi wakiwa na furaha,kuondoa hofu,woga na wasiwasi na kwamba unapokuwa ofisini mwananchi ana matumaini makubwa nawe ya Kusikilizwa na kutatuliwa changamoto zake.

Aidha,Dkt.Shemwelekwa amewaasa watumishi kuwa wanyenyekevu kwa wananchi, kutumia lugha za staha, kuheshimiana, kushirikiana, kupendana na kusaidiana ili kufanya kazi zenye matokeo na zinazoacha alama za kukumbukwa huku akikemea vikali tabia za kufanyakazi kwa mazoea zisizokuwa na tija kwa Taifa letu.

“Watumishi wa Umma tuache kulalamika, tujielekeze kwenye kuondoa malalamiko na kero za wananchi.Tuwasikilize vizuri na kuwahudumia tukiwa na furaha”…amesema Dkt.Shemwelekwa.

Akizungumzia ukusanyaji wa mapato ametoa rai kwa watumishi wote kushiriki na sio kuwaachi Kitengo cha fedha na Divisheni ya Biashara pekee kama ilivyozoeleka huku akitoa rai ya kuongeza uadilifu,uaminifu na kuziba mianya yote inayovujisha ama kuchepusha Mapato na kwamba atakayefanya hivyo hata mvumilia.


“Ndugu zangu tukakusanye Mapato kwa uaminifu na uadilifu ili yatumike kwa Maslahi mapana ya watu wote,atakaye thubutu kwenda kinyume atakumbana na mkono wa sheria” ameongeza.

Dkt.Shemwelekwa amekumbusha watumishi kuwahi Kazini kama sheria,Kanuni na taratibu za Utumishi wa Umma zinavyoelekeza na kwamba hiyo sio hiari ni takwa la Kisheria linalomtaka mtumishi kufanya kazi kwa saa nane kwa siku

Mary Chimoto na Hassan Ngonyani wamesifu utaratibu mpya kiutendaji wa Mkurugenzi Dkt.Shemwelekwa na kwamba kilichobaki ni utekelezaji

Mkuu wa Divisheni na Utumishi na rasilimali watu Dibogo Protas amesema kazi yake kwenda kutafsiri sheria,Kanuni na taratibu kwani watumishi Sasa wamekumbushwa upya wajibu wao.

Dkt.Rogers Shemwelekwa ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kutumiza miaka mitatu Madarakani kwa kuendelea kuwekeza kwenye Miradi mikubwa ya Kimkakati nchini ikiwemo Kibaha Mji ambayo imenufaika na Soko kubwa lenye thamani ya Bilioni nane

By Jamhuri