Wiki hii Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi (pichani), amefanya ziara ya siku tatu mkoani Mtwara kuangalia maendeleo ya ujenzi wa bomba la gesi. Nimepata fursa ya kuwamo kwenye ziara hii. Nimeshuhudia mengi.

Ujenzi wa bomba la gesi asilia katika mikoa ya Lindi na Mtwara umeanza kuzaa matunda baada ya mikoa hiyo kuanza kunufaika kiuchumi.

 

Mikoa hiyo iliyokuwa taabani sasa si kama ile ya zamani. Idadi ya watu wanaongia na kutoka katika mikoa hiyo, sasa imeongezeka kwa kiwango kikubwa.


Idadi hiyo imeongeza mzunguko wa fedha tofauti na miaka ya miwili iliyopita.

Sasa wananchi wa miji hiyo wanatembea kifua mbele kutokana na kukua kwa biashara mbambali zinazowaingizia kipato.


Siku za nyuma kabla bomba la gesi halijaanza kujengwa haikuwa rahisi kusikia nyumba za wageni zimejaa, ila kwa sasa kujaa nyumba hizo ni jambo la kawaida.


Pamoja na watu wengi kuwekeza katika biashara hiyo bado nyumba za wageni hazitoshi kuhimili kishindo cha wageni katika miji hiyo.


Mbali na ujenzi wa nyumba hizo viwanja na navyo sasa bei haishikiki. Kiwanja kilichouzwa Sh milioni moja mwaka juzi sasa kinauzwa milioni 10.


Hata bidha mbalimbalia zinazotokana na mazoea kama vyakula, mifugo na mahitaji mengine nazo zimeapta soko.


Hatua hiyo imepunguza vijiwe vya kahawa na uchezaji bao au kukaa katika mabaraza na kupiga soga kwa kuwa sasa kila mtu ana kazi ya kufanya kujiingizia kipato.

Agizo la Serikali, limewezesha ununuzi wa vyakula kutoka kwa wanachi katika maeneo waliko wawekezaji. Sasa wawekezaji Mtwara wanatakiwa kutumia kila kitu kinachopatikana nchini kwa manufaa ya wanachi wa mikoa hiyo.

 

Vijana wengi wamepata ajira. Wapo waliopata bahati ya kupewa mafunzo kutoka katika

kampuni mbalimbali zilizowekeza katika mikoa hiyo.

Huo ni mwanzo tu, kwa kuwa ujenzi wa bomba hilo uko katika hatua za awali. Wananchi wa Lindi na Mtwara wategemee mengi baada ya kukamilika kwa ujenzi huo.


Ujenzi wa bomba hilo lenye urefu wa kilomita 542  umegawanyika katika sehemu kuu tatu nao ni  kuunganisha na kutandika mabomba hayo ardhini, unaotarajiwa kukamilika mwezi Julai mwaka kesho.

 

Sehemu ya pili ni kutengeneza mabomba kwa kuyawekea zege na kuyatandaza katika Bahari ya Hindi kwa urefu wa kilomita 25 hadi 30.


Na tatu ni ujenzi wa kituo cha Mnazi Bay kitakachotumika kusafisha gesi unaotarajiwa kumalizika Desemba, mwaka kesho.

 

Mbali na mikoa hiyo, Mkoa wa Pwani nao utanufaika na ujenzi wa bomba hilo kutokana na mikakati iliyowekwa kuwa kila sehemu kitapaowekwa kituo wanachi wa eneo husika wasikilizwe na kutekelezewa matatizo yanayowakabili jambo ambalo limeanza kufanyiwa kaza na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).


Vituo bomba hilo ni Tuangoma, Vikindu (Dar es Salaam), Mkuranga Camp V, Bungu, Mkuranga Camp IV, Ikwiriri na Nyamwage (Pwani).


Vingine ni Somanga, Kilwa, Kiwawa, Kirangere, Nangurukuru, Kitomanga (Lindi). Vituo vingine ni Msijute na Madimba (Mtwara)

 

Kwa kutambua kuwa vijana wa miji hiyo wasiishie kuuza maji na mihogo kwa wawekezaji, Benki ya Maendeleo ya Afrika tayari imenzisha mradi wa kukipa nguvu Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) katika Mkoa wa Mtwara.


Viongozi wa wa dini, mashirika mbalimbalia na Serikali wamekuwa  mstali mbele kuhamasisha wananchi wa mikoa hiyo kuhakikisha wanakuwa makini kuwekeza katika elimu. Wapo waliosikia na kutekeleza maagizo hayo, lakini pia wapo waliopuuza.


Shime wananchi wa Mtwara, fursa hii imekuja miguuni kwenu, ni utajiri kutoka kwa Mwenyezi Mungua itumieni. Lakini ndugu zangu wa Mtwara na Lindi kumbukekeni kuwa hakuna kitu kinachokuja kwa kusema tu na kukaa katika vijiwe cha kahawa, bali kufanya kazi kwa bidii.


Iwapo hamtazingatia maelekezo na ushauri unaotolewa na viongozi wa dini, mashirika na Serikali kwa kuwapeleka watoto wenu shule na katika vyuo vya ufundi stadi wataambulia kuwa manamba na watu kutoka katika mikoa mingine wakitanua kwa kufurahia fursa hizo.

By Jamhuri