CCM Rukwa tunataka serikali tatu

Wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Rukwa wamekwenda kinyume na msimamo wa chama chao na kutaka uwepo wa serikali tatu maana katiba ni kwa maslahi ya Taifa na sio wana CCM.

Inawezekana baadhi ya viongozi wa ngazi za juu wanataka serikali mbili kwa maslahi yao binafsi na sio taifa. Tutaiwekea ubavu katiba hiyo hiyo.

 

Watanzania hatutaki watu wanaosimamia baadhi ya mambo yaliyotunyima maendeleo yaendelee kuwepo kwenye katiba hii mpya.

 

Katika hilo hatuwezi kukubali maana ni muda mwafaka na sisi kuwa na serikali yetu ya Tanganyika ili tushugulikie changamoto zetu.

 

Kusema serikali tatu ni gharama siyo kweli maana vitendo vya ufisadi tu kwa sasa kwa mwaka unaweza kuwa sawa na bajeti ya miaka mitatu.

 

Wana CCM Rukwa wametangaza msimamo huo katika mkutano wao katika kijiji cha Kasanga, Wilaya ya Sumbawanga Vijijini.  Nawasilisha.

Mwanachama wa Jamii Forums

 

Mheshimwa Rais naomba unisaidie

Ndugu Mhariri

Ndugu Mheshemiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete, mimi naitwa Gregory, ni mkazi wa Kaliua, mkoani Tabora, lakini kwa sasa naishi uhamishoni Tabora mijini.

 

Sababu ya kuishi uhamishoni ni kutokana na kufukuzwa katika mji wa Kaliua na kuchomewa nyumba yangu kwa hila za kisiasa. Mheshimiwa Rais, kutokana na kuchomewa nyumba yangu hadi sasa sijui hatima ya maisha yangu kwani familia yangu imesambaratika.

 

Nilifikisha suala hili katika ngazi mbalimbali za Jeshi la Polisi kama kwa Kamanda wa Polisi Mkoa na wale wa wilaya wakiwaeo wakuu wa vitengo vya upelelezi mkoa na wilaya, lakini ninachojibiwa kuwa mimi ni mhalifu hivyo sina haki ya kwenda kushtaki polisi.

 

Viongozi hao wa polisi wamekuwa wakinitishia kunifunga pindi ninapokwenda kutoa taarifa  kuhusu tukio langu.

 

Polisi wanamtetea mhalifu aliyenichomea nyumba na kunifukuza katika katika mji niliozaliwa, ambaye ni diwani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM). Sasa nashindwa ni wapi nitapeleka malalamiko yangu.

 

Mheshimwa Rais, naomba unisaidie kupata haki yangu, kwani mimi pamoja na familia yangu tunateseka mno, sijui hatima ya maisha yangu na ya familia yangu.

Ninaandika barua hii kwa uchungu na majonzi makubwa, kutokana na kuona watu uliowapa majukumu ya kutuangalia sisi wanyonge hawatusikilizi wanasikiliza wenye fedha.

Gregory,

Tabora mjini.

 

By Jamhuri