Kibao chawageukia Al-Shabaab, Boko Haram

INTELIJENSIA ya Serikali za Nigeria na Somalia, zimeshtukia mipango ya makundi ya kigaidi ya Al-Shaabab na Boko Haram yaliyopanga kuungana, lakini mambo yamewawia ugumu.

Kwa takribani wiki mbili zilizopita, makundi hayo, yalipanga kuungana kuimarisha nguvu na kupambana na majeshi ya serikali zao mara baada ya kukosa misaada kutoka nje.

Hali hii imetokea baada ya Serikali za Somalia na Nigeria kuunganisha nguvu kusambaratisha makundi hayo ya kigaidi ambayo yametokea kuangamiza maisha ya watu wengi.

Mara baada ya idara za upelelezi za majeshi hayo kushitukia mipango hiyo, tayari kundi la Al-Shabaab linahaha kusaka msaada kutokana na vipigo na kuporwa miji.

Mkuu wa Majeshi ya Somalia, Mahmoud Muhammad, ametamba akisema kwamba “huo ndio mwisho wa kuvuma kwa kundi la Al-Shaabab.”

Muhammad amesema kuwa, Vikosi vya nchi hiyo vikishirikiana na vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Afrika (AMISOM), vimefanikiwa kuukomboa mji Adala.

Mji huo ulioko Kusini mwa Somalia, ulikuwa ukidhibitiwa na wanamgambo wa Al Shabaab na tayari vikosi vya kijeshi vya Somalia vimeshaanza kutekeleza majukumu ya kuimarisha usalama katika mji huo.

Serikali ya Somalia kwa kushirikiana na vikosi vya AMISOM kuanzia mwezi uliopita ilianza kutekeleza operesheni ya pamoja ya kijeshi dhidi ya Al Shabaab.

Kikosi cha AMISOM ni kikosi maalumu kinachoundwa na wanajeshi 22,000 kutoka nchini Somalia kwa lengo la kukabiliana na kundi la Al Shabaab.

Katika mapigano hayo yaliyojiri kilometa 30 mashariki mwa bandari ya Basaso, watu zaidi ya 20 wameuawa huku kila upande ukidai kushinda.

Hata hivyo, Msemaji wa kundi hilo la Al Shabaab, Abdiweli Hirsi Abdille alisema kuwa mapigano hayo hayawatishi kwa kuwa bado wanadhibiti eneo la Puntland.

Abdille ambaye ni Waziri wa Habari wa eneo la Mashariki la Somalia la Puntland, amesema vikosi vyao vimefanikiwa kudhibiti eneo la milima ya Galgala kupitia mapigano hayo.

Katika mapigano hayo yaliyojiri kilomita 30 mashariki mwa bandari ya Basaso, watu zaidi ya 20 wameuawa huku kila upande ukidai kushinda.

Nguvu iliyotumika kuanza kusambaratisha Somalia, ndiyo hiyo iliyotangazwa na Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria ambaye amesema, “Magaidi hawa hawawezi kuungana.”

Akizungumza mjini Abuja kwenye sherehe za kutimiza miaka 54 ya Uhuru wa Nigeria wiki iliyopita, Rais Jonathan alisema sasa ni wakati mwafaka wa kukabiliana na kundi la Boko Haram la nchini humo.

Rais Jonathan ameongeza kuwa, suala la kulindwa maisha ya wananchi ni miongoni mwa mambo yanayopewa kipaumbele na serikali, “Kundi la Boko Haram linapaswa kupokonywa silaha.”

Kundi hilo tangu mwaka 2009 limekuwa likitekeleza mauaji, utekaji nyara, ulipuaji wa majengo ya serikali na kuharibu miundo mbinu nchini humo na kusababisha zaidi ya watu 2000 kuuawa na maelfu wengine kuwa wakimbizi.