Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara Abdulrahman Kinana ameelezea kutoridhishwa kwake na kasi ya ujenzi wa barabara inayounganisha mikoa ya Kigoma na Kagera.

Akizungumza mjini Biharamulo mara baada ya kuwasili kuanza ziara ya siku mbili mkoani Kagera akitokea Kigoma Kinana amesema kasi ya ujenzi wa barabara hiyo ya Kasulu- Nyakanazi si ya kuridhisha.

“ Nimeona kazi inayoendelea ya ujenzi kuna wakandarasi watano na Mungu akipenda itakamilika lakini kuna kuchelewa chelewa kidogo kwahiyo naomba viongozi wa Kagera, Kigoma na wizara ya ujenzi kuwasimamia” amesema.

Akizungumzia baada ya Kinana kuwasili Mkoa wa Kagera, Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoa Costancia Muhiye amesema viongozi wa ngazi mbalimbali wa Wilaya,Mkkoa pamoja na wananchi wamejitokeza kwa wingi kumpokea Makamu Mwenyekiti.

Muheye ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa wananchi wa Mkoa wa Kagera wanampongeza Kinana kwa kuteuliwa na Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kumteua nafasi hiyo.”Makamu Mwenyekiti wewe ni mwenzetu, unakijua Chama chetu vizuri, tunamshukuru Mwenyekiti wetu kwa kujiamini na kukuteua kwenye nafasi hiyo.

“Wananchi wa Mkoa wa Kagera tunakumbuka ukiwa Katibu Mkuu wa Chama chetu ulikuja kwetu na tukaa na wewe,tulipita kila mahali, hivyo tunakukaribisha,”amesema Mwenyekiti huyo wa Mkoa wa Kagera.

Kinana ameambatana na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa ( NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Itikadi na Uenezi Shaka Hamdu Shaka pamoja na maofisa wengine wa Chama hicho

By Jamhuri