Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Singida

Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu ameweka wazi kuwa tangu ameanza ziara yake kuna gari inafuatilia msafara wake na wakifika kwenye mkutano Watu hao hujificha.

Lissu ameyasema hayo akiwa kwenye mkutano katika kata ya matumbo Jimbo la Singida Kaskazini, ambapo hali hiyo imekuwa ikimuogopesha na hivyo kuwaomba Polisi kama ni wao basi wampe taarifa ili awe na amani na kama wasiposema atawanyooshea vidole kwenye mkutano.

“Tangu nimeanza ziara yangu kuna gari inatufuatilia halafu wakifika kwenye mikutano wanajificha, nyinyi mnajua mimi nimeshambuliwa sasa nikiona hali kama hiyi ninaogopa, nataka niseme kama ni Polisi mje mniambie kama mmetumwa na Serikali niambieni ili niwe na amani msiposema kesho kwenye mkutano wangu nitawanyooshea kidole ili wananchi wawatambuwe kama ni Wakazi wa sehemu husika maana Vijana wangu wameshawatambua” amesema.

Mwezi Agosti mwaka 2017, Tundu Lissu aliitisha mkutano na waandishi wa habari na kusema kuna vijana wanamfuatilia kila anapokwenda, na baadaye Septemba 17,2017, akashambuliwa kwa risasi akiwa Jijini Dodoma.