na Isri Mohamed, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Pazia la Ligi Kuu ya NBC Tanzania bara linafungwa rasmi leo Mei 28, 2024 huku kukiwa na vita tatu kubwa za kushindaniwa ikiwa ni pamoja na mbio za nafasi ya pili, mbio za ufungaji bora na mbio za golikipa bora wa Ligi hiyo.

NAFASI YA PILI

Simba Sc yenye pointi (66) inaendelea kuchuana na Azam Fc ambayo nayo ina alama (66) kwenye mbio za nafasi kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao huku Mnyama akiwa nyumbani Benjamin Mkapa kukabiliana na maafande wa JKT Tanzania wakati Wanalambalamba ambao wapo mbele ya Mnyama kwa tofauti ya magoli watakuwa ugenini dhidi ya Geita Gold Fc katika dimba la Nyankumbu, Geita.

MBIO ZA UFUNGAJI BORA:

Stephanie Aziz Ki wa Yanga Sc na Feisal Salum ‘Feitoto’ wa Azam Fc ambao kila mmoja amefunga magoli 18 watautumia mchezo leo kutafuta kuongeza akaunti yao ya magoli.

MBIO ZA GLAVU YA DHAHABU
Nyanda wa Yanga Sc Djigui Diarra na Ley Matampi wa Coastal Union ambao kila mmoja ana ‘clean sheets’ 14 wapo kwenye vita ya kuwania tuzo ya golikipa bora (Golden Glove) wa Ligi Kuu bara

Diarra anatarajiwa kuwa langoni pale Young Africans Sc watakapochuana na Tanzania Prisons katika dimba la Azam Complex, Chamazi huku Ley Matampi akitarajiwa kuwa kibaruani pale Coastal Union watakapoikaribisha KMC Fc katika dimba Mkwakwani, Tanga.

RATIBA

Simba Sc vs JKT Tanzania
Geita Gold Fc vs Azam Fc
Yanga Sc vs Tanzania Prisons
Namungo Fc vs Tabora United
Coastal Union vs KMC Fc
Mashujaa Fc vs Dodoma Jiji Fc
Ihefu Fc vs Mtibwa Sugar
Singida FG Fc vs Kagera Sugar