NA BASHIR YAKUB

1. Nini maana ya hisa?

Hisa ni masilahi ya kila mwanachama
aliyonayo katika kampuni fulani. Yaani
wewe kama ni mwanahisa katika kampuni
fulani, basi yale masilahi yako au kiwango
chako cha uwekezaji ulichowekeza katika
ile kampuni ndizo hisa zako.
Kama mko watu kumi katika kampuni, basi
kila mtu ana masilahi au kiwango kadhaa
cha uwekezaji, ambapo ukikusanya
uwekezaji huo kwa pamoja ndio utaitwa
hisa za kampuni.
Uwekezaji au masilahi katika kampuni
hutofautiana kutokana na uwezo wa kila

mwanahisa.
Tofauti hutokana na kiwango cha kila mtu
alichowekeza. Kuna mwenye hisa kumi,
kuna mwenye ishirini, kuna mwenye hisa
mia n.k.
Hisa siku zote hupimwa kwa kiwango cha
pesa. Yawezekana uwekezaji wa mtu
kwenye kampuni ni magari, yaani amepata
hisa kwa kuchangia magari. Mwingine
amepata hisa kwa kuchangia ofisi na
mwingine amepata hisa kwa kuchangia
vifaa vyote vya ofisi.
Katika kuhesabu hisa, michango hii yote
itawekwa katika viwango vya pesa na
itasemwa kuwa fulani ana hisa za shilingi
kadhaa na si ana hisa za magari au vifaa
kadhaa.
Kwa hiyo hisa huhesabiwa kwa
mtindo/viwango vya fedha.

2. Aina za hisa

Hisa si hisa kama wengi tunavyojua,

isipokuwa hisa zina aina zake. Si kila
mwenye hisa ana hisa, isipokuwa ana hisa
gani au za aina gani.
Aina za hisa za mtu katika kampuni ndizo
humwezesha kujua ana haki gani katika
kampuni, wajibu gani na anawajibikaje
likitokea tatizo.
Kwa hiyo haki, wajibu (duty) na uwajibikaji
(liability) katika kampuni hutofautiana kutoka
mwanahisa mmoja hadi mwingine kutokana
na aina za hisa anazomiliki. Wanahisa wote
hawana haki sawa, hawana wajibu sawa na
hawawajibiki sawa pamoja na kuwa katika
kampuni moja.

Aina za hisa:
(a) Hisa za wamiliki (Equity shares)
Hizi ni aina za hisa ambazo huwa ndizo
nyingi katika kampuni. Wale wanaomiliki
hisa nyingi katika kampuni hisa zao huitwa
hisa za wamiliki.
Huitwa hisa za wamiliki kwakuwa hawa
huhesabika kama ndio kampuni yenyewe,

hivyo wenye hisa hizo ndio wamiliki wa
kampuni.
Nimesema hapo juu kuwa wanahisa
hawana haki sawa, wajibu, pamoja na
uwajibikaji. Wenye hisa hizi wana haki
kubwa ya kimaamuzi katika shughuli zote
za uendeshaji wa kampuni, kwa kuwa wao
kila hisa moja huwa ni kura moja, kwa hiyo
kila kitu hupitishwa kwa kura zao.
Pia wana haki ya kupata mgao mkubwa
kuliko wengine, hata hivyo wanawajibika
zaidi linapotokea tatizo, kwa mfano
inapotokea hasara wao ndio hupoteza zaidi.
Kwa jina jingine, hisa za hawa huitwa hisa
za simba (Lion’s share). Hii ni kwa sababu
huko mwituni simba hupata mgao mkubwa
wa nyama miongoni mwa wanyama wote.

(b) Hisa za kawaida

Hizi ni zile hisa ambazo humilikiwa na watu
wengine wa kawaida katika kampuni. Mara
nyingi hawa ndio huwa wengi japo kila mtu

huwa na hisa kidogo kidogo.
Mgao wao wa faida hutokana na asilimia ya
kile mtu anachomiliki. Maamuzi yao katika
kampuni huwa ni madogo ukilinganisha na
wenye zile hisa za umiliki (equity shares).
Hata hivyo uwajibikaji wao nao ni mdogo
pia, kwani hupata hasara kidogo pale
kampuni inapopata hasara. Pamoja na
hayo, sheria imewapa kipaumbele cha
kupewa mgao wa faida kabla ya kundi
jingine lolote.

(c) Hisa za waanzilishi (Deferred shares)

Hizi ni hisa ambazo hutolewa kama zawadi
kwa waanzilishi wa kampuni. Mgao wa faida
wa hisa hizi huwa si wa moja kwa moja
isipokuwa hutegemea faida inayozidi.
Kawaida mgao wa faida kwa wanahisa
wengine hutoka katika faida ya kawaida,
lakini hawa hawapewi mgao kutoka faida ya
kawaida, isipokuwa hupata pale faida
inapozidi au kuvuka kiwango
kilichotegemewa.

(d) Hisa za kampuni (Corporate shares)

Zote nilizotaja juu ni hisa za kampuni, lakini
bado jina hili hupewa hisa hizi kutokana na
kuwa ni hisa maalumu ambazo hutolewa
kwa waajiriwa/wafanyakazi katika kampuni
husika.
Waajiriwa hutengewa hisa zao na mwenye
uwezo huweza kuchukua hisa hizo kwa
kiwango cha uwezo wake. Mwajiriwa
huendelea kuwa na hisa hizo hata baada ya
utumishi wake kukoma.
Kwa ufupi sana, niseme tu kuwa hisa si
hisa, ila hisa ni una hisa za aina gani.

Kuhusu sheria za ardhi, mirathi,
makampuni, ndoa n.k, tembelea SHERIA
YAKUB BLOG.

Mwisho

By Jamhuri