Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya(MZRH), imepokea Madaktari bingwa wanne kutoka Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China ambao wanatarajiwa kutoa huduma mbalimbali za kibobezi, ikiwemo za upasuaji kwa kushirikiana na Madaktari wa Hospitali hiyo.

Akizungumza ofisini kwake mapema leo Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya Dkt. Godlove Mbwanji amewashukuru na kuwakaribisha wataalamu hao na kuishukuru Serikali ya China kwa kuendelea kuimarisha ushirikiano wa Tanzania na China katika sekta ya afya.

“Tunaishukuru Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Wizara ya Afya kwa kuwezesha kutuletea Madaktari hawa bingwa,

Madaktari hawa watatoa huduma mbalimbali za kitabibu kwa wagonjwa mahututi, utoaji salama wa dawa za usingizi na ganzi pamoja matibabu ya Upasuaji wa watoto na upasuaji wa mifupa.” alisema Dkt.Godlove Mbwanji

Ambapo aliongeza kuwa, kwa kushirikiana na Madaktari wa MZRH watatoa huduma mbalimbali za kibingwa kwa wakazi wa Nyanda za Juu Kusini na Mikoa ya Jirani.

Kwa upande wake kiongozi wa kundi hilo la Madaktari kutoka China, Dkt.Dubinbing ameushukuru Uongozi wa Hospitali ya MZRH kwa mapokezi mazuri na kuahidi kutoa ushirikiano mzuri kwa wataalam wa Hospitali katika kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi wa Tanzania.

By Jamhuri