Msajili Mkuu wa Hazina, Nehemiah Mchechu amelipongeza Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) baada ya uongozi wake kufanikiwa kuleta mageuzi makubwa na kulifanya shirika kuanza kuzalisha faida.

Hatua hiyo inakuja wakati mwaka jana shirika hilo ambalo lilifikisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, kufanikiwa kutoa gawio la zaidi ya Sh bilioni 2.2 kwa Serikali.

Akitoa wasilisho lake mwishoni mwa wiki iliyopita jijini Dar es Salaam katika Mkutano wa Ofisi ya Msajili wa Hazina na wenyeviti wa bodi, wakurugenzi wa taasisi na mashirika mbalimbali ya umma, Mchechu alisema shirika hilo sasa limeitoa kimasomaso Serikali baada ya kuwa moja ya mashirika yanayoingiza faida kubwa kwa Serikali.

Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu akizungumza katika mkutano wa ofisi yake na wakurugenzi, wenyeviti wa bodi na viongozi wa taasisi na mashirika mbalimbali ya umma jijini , Dar es Salaam.

Alisema lengo la Serikali ni kuona mashirika ya umma yanaacha kuwa tegemezi kwa serikali hivyo kuizidishia mzigo wa kuyaendesha.

Kutokana na mafanikio hayo, Shirika hilo ambalo lilitajwa kuwa mfu, mwaka 2019 wabunge walidhibitisha kwamba haliwezi kufutwa tena kutokana na mwenendo wa sasa kuridhisha kutokana na utendaji wake na kubadili mtazamo wa awali.

Hayo yanajiri wakati Machi mwaka huu Shirika hilo lilifanikiwa kusaini mkataba mnono wa kihistoria wa miaka miwili wenye thamani ya Sh bilioni 55.2 na Kampuni ya uchimbaji madini ya dhahabu Geita- Geita Gold Mining Limited (GGML) mahususi kwa ajili ya shughuli za kuchoronga miamba ndani ya mgodi huo.

Mkataba huo mnono, ulifuata baada ya STAMICO kufanikiwa kutekeleza kwa ufanisi mkataba wa awali wenye thamani ya Sh bilioni 5.6 ambao ulisainiwa Julai 2020.

Mkurugenzi Mtendaji wa Stamico, Dk. Venance Mwasse (kushoto) akimkabidhi mkaa mbadala mmoja wa wateja walionunua mkaa huo unaozalishwa na Shirika hilo kwa lengo la kuendelea kuhifadhi mazingira.

Kutokana na halo hiyo Waziri wa Madini, Dk. Dotto Biteko alisema mikataba hiyo ni matunda ya uwekezaji uliofanywa na serikali kuhakikisha kampuni ya Stamico inaimarika na kuweza kujiendesha kwa faida.

Pamoja na mambo mengine shirika hilo linaloongozwa na Mkurugenzi Mtendaji Dk. Venance Mwasse, limefanikiwa kubuni nishati mbadala ya kupikia Rafiki Briquttes ambayo ni rafiki kwa mazingira.

Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Dk. Venance Mwasse (kushoto) pamoja na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mgodi wa GGML, Damon Elder, wakionesha mikataba waliosaini baada (STAMICO), kusaini mkataba wa miaka miwili wenye thamani ya Sh bilioni 55.2 na Kampuni ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML) mahususi kwa ajili ya shughuli za kuchoronga migodi ya GGML.

By Jamhuri