Majaliwa: Tutaendelea kuondoa changamkto sekta ya nishati

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan itaendelea kusimamia kikamilifu sekta ya nishati nchini ili kuondoa changamoto mbalimbali zitokanazo na sekta hiyo.

Amesema hayo leo wakati alipomuwakilisha Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan katika kongamano la nishati lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere.

“Umeme tulionao utaimarika na utakuwa wa gharama nafuu, na sasa tunauhakika wa kupeleka umeme mpaka vijijini na tunaendelea kuhamasisha watanzania kila mmoja aweke umeme”

Amesema kuwa mradi wa bomba la mafuta kutoka nchini Uganda unaendelea vizuri. “Kampuni inayosimamia utekelezaji wa mradi huu imejipanga vizuri kwa pande zote mbili za Tanzania na Uganda.”

Amesema kuwa utekelezaji wa miradi mbalimbali katika sekta ya nishati ikiwemo ya mafuta na gesi itasaidia kwa kiasi kikubwa katika kukuza uchumi wa nchi kutokana na mapato yatakayokuwa yanakusanywa kutoka kwenye miradi hiyo.

Amesema kuwa kongamano hilo litafungua fursa za uwekezaji nchini kutokana na kujumuisha makampuni mbalimbali makubwa ya kimataifa katika sekta ya nishati “Tuna wageni ambao ni wadau katika sekta ya nishati, kongamano hili la kimataifa litafungua fursa zilizopo kwenye sekta ya nishati ikiwemo maji, makaa ya mawe, gesi na umeme wa jua”

Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na washirika wa kimataifa katika kukuza ushirikishwaji na uwezeshaji wa wanawake kiuchumi katika sekta ya nishati.

“Lengo la Serikali ni kutumia fursa za sekta yetu ya nishati ili kuboresha sekta nyingine ikiwemo viwanda na uchumi. Kwa hiyo ni kwa imani yangu kwamba, kongamano hili litawawezesha washiriki kubadilishana uzoefu, mawazo, ujuzi, maarifa, ambayo ni muhimu katika kusimamia rasilimali za mafuta kwa njia endelevu kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho”

Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha inaweka kanuni na taratibu zinazofaa ili kuwezesha ushirikishwaji wa wafanyabiashara wa ndani kunufaika na mnyororo wa thamani katika sekta ya nishati.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Januari Makamba amesema Tanzania ina rais ambaye ana matamanio ya kuifanya sekta ya nishati kuwa chanzo cha ukuaji wa uchumi nchini.

Awali, Mkurugenzi wa Ocean Business Partners ambao ndio waandaaji wa kongamano hilo, Abdulsamad Abdulrahim alisema kongamano hilo litawawezesha wadau kutambua fursa za uwekezaji katika sekta ya nishati nchini.

By Jamhuri