Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amewakaribisha wawekezaji kutoka nchini China na mataifa mengine kuwekeza nchini Tanzania kutokana na mazingira rafiki ya kijiografia, kimiundombinu, kisiasa, kisera na kisheria yaliyopo.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati akifunga Jukwaa la Uwekezaji kati ya China na Tanzania lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Johari Rotana Jijini Dar es salaam. Amesema Tanzania imedumisha amani tangu kupata uhuru mwaka 1961, imeendelea kufanya mageuzi ya sheria na utekelezaji sera zinazolenga kuimarisha mazingira ya uwekezaji na ufanyaji biashara. Pia amesema faida za kijiogragfia ni pamoja na kuwa na soko la ndani la watu zaidi ya milioni 64 pamoja na soko la watu bilioni 1.4 katika matumizi ya Ukanda Huru wa Biashara Barani Afrika, Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika pamoja na Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Makamu wa Rais ameongeza kwamba, Uwekezaji nchini Tanzania unawezesha kufikia masoko ya Marekani kupitia mpango wa AGOA, soko la Ulaya kupitia mpango wa EBA pamoja na soko la China kupitia mpango wa FOCAC, pia nchi za Japan kupitia TICAD pamoja na soko la India.

Makamu wa Rais amesema uchumi wa Tanzania umeendelea kuimarika mara baada ya athari za Uviko19 ambapo umekua kwa asilimia 5.5 kwa mwaka 2023 na kutarajiwa kukuka kwa asilimia 6 kwa mwaka 2024-2027. Amesema serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imewekeza katika kujenga uchumi imara kupitia R nne zinazolenga Uhimilivu, Ujenzi Mpya, Maridhiano na Mageuzi.

Halikadhalika Makamu wa Rais amesema imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika miundombinu ili kuweka mazingira bora ya ufanyaji biashara na uwekezaji. Ametaja uwekezaji huo ni pamoja na miradi ya nishati ya uhakika, uboreshaji bandari, ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) ambayo itafika hadi Burundi na Kindu Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Pia amesema uwekezaji mwingine ni katika elimu ili kupata rasilimali watu iliyobora zaidi pamoja na sekta ya afya.

Makamu wa Rais amewasihi wawekezaji kutoka China na Mataifa mengine kuwekeza Tanzania katika mazingira na uchumi wa buluu, ambapo amewasisitiza wawekezaji kuja na teknolojia za kisasa zitakazosaidia kuwahamisha wananchi katika matumizi ya nishati chafu na kuokoa uharibifu wa mazingira.

Pia amekaribisha uwekezaji sahihi katika kuendeleza maeneo ya pwani na visiwa ili kuweza kutumia vema uchumi wa buluu na huku mazingira yakilindwa.

Makamu wa Rais amesema kwa muda mrefu Jamhuri ya Watu wa China imekuwa mwekezaji mkuu wa kimkakati na mshirika wa biashara wa Tanzania. Amesema mtiririko wa fedha wa kila mwaka kutoka China uliongezeka kutoka dola milioni 92 mwaka 2019 hadi dola milioni 221 mwaka 2021. Katika kipindi cha Januari 2021 hadi Desemba 2023, miradi 256 ya Kichina iliyosajiliwa na Kituo cha Uwekezaji Tanzania ilikuwa na thamani ya dola za Kimarekani bilioni 2.4, ikikadiriwa kuzalisha ajira 29,122.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akifuatilia mawasilisho mbalimbali wakati wa Jukwaa la Uwekezaji kati ya China na Tanzania lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Johari Rotana Jijini Dar es salaam tarehe 27 Machi 2024.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip akihutubia wakati akifunga Jukwaa la Uwekezaji kati ya China na Tanzania lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Johari Rotana Jijini Dar es salaam tarehe 27 Machi 2024.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip akihutubia wakati akifunga Jukwaa la Uwekezaji kati ya China na Tanzania lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Johari Rotana Jijini Dar es salaam tarehe 27 Machi 2024.
akamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Tanzania pamoja na ujumbe wa wafanyabiashara na wawekezaji kutoka nchini China mara baada ya kuhitimishwa kwa Jukwaa la Uwekezaji kati ya China na Tanzania lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Johari Rotana Jijini Dar es salaam tarehe 27 Machi 2024.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Tanzania pamoja na wafanyabiashara wanawake kutoka nchini China mara baada ya kuhitimishwa kwa Jukwaa la Uwekezaji kati ya China na Tanzania lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Johari Rotana Jijini Dar es salaam tarehe 27 Machi 2024.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiagana na Katibu wa Tume ya Manispaa ya Jinhua wa Chama Cha Kikomonisti cha China (CPC) Bw. Zhu Chonglie mara baada ya kuhitimishwa kwa Jukwaa la Uwekezaji kati ya China na Tanzania lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Johari Rotana Jijini Dar es salaam tarehe 27 Machi 2024.

By Jamhuri