Mashabiki wa klabu ya Simba waliokuwa katika basi dogo la abiria aina ya Coaster wamepata ajali eneo la Vigwaza mkoani Pwani na mtu mmoja amefariki.

Taarifa ya Idara ya Habari na Mawasiliano ya Simba imeeleza kuwa ajali hiyo imetokea alfajiri ya leo, wakati mashabiki hao wakiwa njiani kuelekea jijini Dar es Salaam, ambapo usiku Simba itacheza na Al Ahly ya Misri mchezo wa Robo Fainali Ligi ya Mabingwa Afrika, Uwanja wa Benjamin Mkapa.

Taarifa hiyo imesema uongozi wa Simba umepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za ajali mbili za mashabiki wa Simba ya kwanza ikiwa ya Vigwaza na nyingine iliyotokea Doma mkoani Morogoro na kwamba mashabiki hao walikuwa wakitokea mkoani Mbeya.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo ajali ya Vigwaza imehusisha mashabiki wa Tawi la Kiwira Rungwe la mkoani Mbeya, ambapo taarifa za awali za Polisi zinaeleza mtu mmoja amepoteza maisha.

Ajali ya pili imetokea mkoani Morogoro ikihusisha mashabiki wa tawi la Wekundu wa Boader Tunduma iliyotokea Doma mkoani Morogoro, taarifa za awali zinaeleza mtu mmoja ameumia na hakuna madhara makubwa, ambapo taarifa inaeleza viongozi wa Simba wanaelekea Vigwaza ili kutoa msaada zaidi kwa waathirika.

By Jamhuri