Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Mkuranga

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru, Godfrey Mzava, Mei 4 Mwaka 2024 ,ameweka jiwe la msingi mradi wa maji Kimanzichana, wilayani Mkuranga, uliogharimu sh.bilioni 5.2 ambao utanufaisha zaidi ya watu 20,000 na kusimamiwa na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA).

Akizungumza baada ya kukagua na kuridhishwa na mradi huo, wakati Mwenge ulipokuwa wilayani Mkuranga kutokea Kisarawe,Mzava alieleza mradi huo utakuwa mkombozi kwa jamii.

Hata hivyo, ameiagiza mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira vijijini (RUWASA) kuweka ulinzi shirikishi kwa pamoja na wananchi wanaozunguka miradi ya maji dhidi ya hujuma za baadhi ya watu wasiokuwa na nia njema na miradi inayotekelezwa.

Anaeleza, ili miradi ilete tija kwa wananchi inayoendana na thamani ya fedha zilizotolewa na Serikali ni lazima ilindwe na kutunzwa.

Aidha ameziasa, Halmashauri nchini kuacha kujisifu kwa idadi ya miti waliyopanda bali wajikite kwenye usimamizi na uendelezaji wa miti kufikia adhma ya kuwa Tanzania ya Kijani, ili kukabiliana athari za mabadiliko ya tabia nchi inayosababishwa na uharibifu wa mazingira.

Nae Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge, ameshiriki Mbio za Mwenge wilayani Mkuranga, na kueleza kwa sasa mkoa huo unapata maji safi na salama kwa asilimia 86.

Anasema ,kwa maeneo ya mjini asilimia 93 na Vijijini 79.6 lengo ni kufikia asilimia 95 mijini na Vijijini asilimia 85.

“Tunafahamu kuwa Rais Samia Suluhu Hassan ndie mwanzilishi wa kampeni ya kumtua ndoo mama kichwani na anaendelea na jitihada ya kampeni hiyo ambapo kwa mkoa wa Pwani ameshatoa fedha nyingi kwa upande wa RUWASA na DAWASA.

Meneja wa RUWASA Wilayani Mkuranga ,Mhandisi Maria Malale akitoa taarifa ya mradi amesema, mradi wa maji Kimanzichana
ni sehemu ya mkataba mkubwa wenye thamani ya sh.bilioni 5.273,377,000.5 ambao umehusisha ,miradi mingine minne kwenye vijiji vya Mwarusembe,Dondo ,Sotele na Lukanga .

Ameeleza, gharama kwa Kimanzichana ni milioni 516,309,960 ambazo zimetolewa na Serikali Kuu kupitia program ya lipa kwa matokeo (PforR).

Malale amefafanua, mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi Serengeti Ltd ukijumuisha ujenzi wa nyumba ya pampu,uvutaji umeme,ufungaji pampu na utandazaji wa mabomba km.19.4 ,ambapo unasimamiwa na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini RUWASA wilayani Mkuranga.

“Mradi umefikia asilimia 90 ya utekelezaji, baada ya maji kufika kwenye tenki kazi inayoendelea ni kuwaungia wateja maji majumbani kutoka kwenye bomba kuu, lengo likiwa kuwafikishia maji wateja 20,000” anasema Malale .

Akipokea Mwenge wa Uhuru kutoka wilayani Kisarawe, Mkuu wa wilaya ya Mkuranga, Hadija Nasir alisema jumla ya miradi 13 yenye thamani ya sh. bilioni 10.2 .

By Jamhuri