Mtuhumiwa Malele anaweza kuishitaki Polisi

 

. Ni kwa kumtangaza mgonjwa wa akili

Kijana aliyejitangaza kung’atuka ushirika wa mtandao uliohusika kumuua aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow, anaweza kulishitaki jeshi hilo kwa kumtangaza kuwa ni mgonjwa wa akili.

Jeshi la Polisi Tanzania kupitia kwa Msemaji wake, SSP Advera Senso, Mei 28, mwaka huu, lilimtangaza kijana huyo, Mohamed Malele kupitia vyombo vya habari kuwa ni mgonjwa wa akili bila kuonesha vielelezo vya daktari.

 

Kwa mujibu wa wanataaluma ya sheria waliozungumza na JAMHURI kwa nyakati tofauti hivi karibuni, Malele anayo haki ya kisheria ya kufungua kesi ya madai dhidi ya jeshi hilo, akililalamikia kumkashifu na kumdhalilisha mbele ya jamii.

 

“Kisheria ni kosa la jinai kwa mtu wa asiye na taaluma ya utabibu kumtangaza mwingine kuwa ni mgonjwa wa akili bila kuwa na uthibitisho au kielelezo kutoka kwa daktari husika,” ameeleza mwanasheria mmoja (jina lipo).

 

Anaongeza; “Unajua kila mtu ana haki ya kulindiwa heshima yake. Huwezi kumtangaza mtu kuwa ni kichaa, au mgonjwa wa ukimwi bila kuegemea kwenye ‘quotation’ ya daktari. Kufanya hivyo ni kukiuka law of tort (sheria ya kosa la daawa/madhara).”

 

Mwanasheria mwingine amesema, “Kama mtu (asiye daktari) hana uthibitisho wa daktari, hana nguvu ya kisheria kukwepa shitaka la kumdhalilisha mtu kwa kumtangaza katika jamii kuwa ana ugonjwa fulani.

 

“Ninasema hivi kwa sababu hata madaktari wenyewe huwa makini sana katika kutangaza ugonjwa wa mtu. Vinginevyo unaweza kujikuta unapandishwa kizimbani kujibu ama shitaka la kukashifu, au kudhalilisha utu wa mtu,” ameongeza mwanasheria huyo.

 

Juhudi za kumpata dakatari anayemhudumia Malele katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alikolazwa, hazikuzaa matunda baada ya daktari huyo kukwepa kukutana na JAMHURI, huku ofisa uhusiano wa hospitali hiyo naye akidaiwa kuwa likizo.