Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Pwani

Mufti wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir, anatarajia kuzindua rasmi kitabu chake ambacho kinahusu masuala mazima ya maadili, kitabia ndani ya jamii hususan kwa kundi la vijana, ifikapo mfungo Mosi.

Aidha amewaasa watanzania kujenga tabia ya kusaidia makundi maalum pamoja na watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu (yatima) kwa nyakati zote isiishie mwezi mtukufu wa Ramadan pekee.

Sheikh Zubeir alisema hayo katika iftari iliyoandaliwa na Rais dkt Samia Suluhu Hassan na kusimamiwa na Serikali mkoa wa Pwani, ambapo watu 500 wakiwemo watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu 300 ,wazazi wao , viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa , Taasisi na waalikwa wengine walijumuika katika futari hiyo.

Alieleza ,suala la maadili ni pana hivyo ni lazima kushirikiana ili kuwa na kizazi chenye maadili mema.

Sheikh Zubeir alitoa rai kwa jamii hususan kundi la vijana kutengeneza misimamo katika maadili na tabia njema ,ili kuwa na Taifa lenye maadili na mfano wa kuigwa Duniani.

“Ili Taifa lisimame vizuri na kuwa Taifa bora lazima kuwa na maadili kwani Hakuna Taifa bora ambalo linasimama pasipo watu wake kuwa na maadili bora” alisisitiza.

Vilevile alieleza kitendo cha Mkuu wa Mkoa wa Pwani Alhaj Abubakar Kunenge kufuturisha futari kwa kula pamoja na watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu ni jambo jema lakuigwa.

“Watoto hawa wanahitaji faraja ,wasiojiweza wasaidie na isiwe mwezi mtukufu wa Ramadan hata nyakati nyingine ,na tukijenga tabia hii ya kusaidia tutajikuta tunafikia kundi kubwa” aliongeza Sheikh Zubeir.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Pwani Alhaj Abubakar Kunenge alieleza, mwaka 2023 alitoa futari Mkoani Pwani, Machi 27 Dodoma na Machi 28 mwaka huu mkoa umesimamia watu 500 Kati yao watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu 300 wamejumuika kufuturu .

Kunenge alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kujali makundi maalum.

Mkuu huyo wa mkoa, aliziasa Taasisi zinazojihusisha kulea watoto ambazo zinakwenda kinyume na mikataba kwa kujinufaisha matumbo yao waache mara moja ,na wanachotakiwa ni kutekeleza malengo yao kwa watoto hao.

Nae Sheikh wa Mkoa wa Pwani, Khamis Mtupa amesema waumini wa kiislam waendeleze kufanya yaliyo mema katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadan.

Alieleza,kutoa ni imani Hata kama ni kidogo na kwa kutambua hilo Wana kamati maalum ambayo wanafikia wasiojiweza, gerezani ,mashuleni ili nao waweze kupata futari.

Mtupa aliomba watanzania kuendelea kuliombea Taifa Amani na kumuombea Rais dkt Samia kufanya majukumu yake kwa afya bora.

By Jamhuri