Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula amesema azma ya Serikali ya Tanzania ya kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi iko pale pale ndio maana inaandaa inafanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha changamoto hiyo inapata suluhisho.

Amesema hayo Septemba 2, 2022 jijini Dar esa Salaam wakati akifunga Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi na Maendeleo ulioandaliwa na Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano na Serikali ya Uingereza.

Balozi Mulamula amesema Tanzania imetimiza wajibu wake katika mapambano dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi ambapo miongoni mwa jitihada zilizofanyika na kuzindua Sera ya Taifa ya Mazingira ya mwaka 2021.

Mkuu wa Kitengo cha Mikutano na Mabadiliko ya Tabianchi Uingereza Bw. Matt Toombs akizungumza katika Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi na Maendeleo ulioandaliwa na Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano na Serikali ya Uingereza na kufanyika Septemba 1 hadi 2, 2022 jijini Dar es Salaam.

Amesema katika Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi na Maendeleo mambo mbalimbali yamejadiliwa yakiwemo nchi zinazoendelea kukumbushwa kutimiza ahadi zao za kutoa fedha kwa ajili ya kusaidia katika harakati hizo.

Balozi Mulamula alikumbusha kuhusu ahadi zilizotolewa katika Mkutano wa COP 26 Novemba 2021 nchini Scotland za kusaidia Tanzania na nchi zingine zinazoendelea katika kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kusema ni wakati sasa wa utekelezaji.

“Ninaamini kwamba siku hizi mbili za mkutano zimekuwezesha kutoa mchango mkubwa katika kurahisisha upatikanaji wa fedha za mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi. Ninaamini pia mkutano huu utakuwa ni mwanzo wa ushirikiano bora kwa mataifa mbalimbali,” alisema.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Dkt. Omar Dadi Shajak alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ)katika bajeti ya mwaka 2022/23 imetenga sh. Bilioni 4.1 kwa ajili ya mapambano dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi.

Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Thomas Bwana akiwasilisha Mpango Kabambe wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022-2032) kwa washiriki wa Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi na Maendeleo kutoka mataifa zaidi ya 20 uliofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Septemba 1 hadi 2, 2022.

Alisema kuwa visiwa vya Zanzibar vinakabiliwa na athari hizo katika maeneo yote na hivyo kuathiri shughuli za kilimo ambapo majichumvi yanaingia katika mashamba ya mpunga.

Hivyo Dkt. Shajak alisema kuwa ushiriki wa Tanzania katika Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi na Maendeleo utasaidia katika kuja na suluhu ya changamoto hizo za mabadiliko ya tabianchi kwa upande wa Zanzibar.

Mkutano huo uliofunguliwa Septemba 1, 2022 na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo ni maandalizi ya Mkutano wa 27 wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP27) unaotarajiwa kufanyika nchini Misri Novemba 2022.

By Jamhuri