Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara lina mshikilia mwanaume mmoja jina limehifadhiwa (56), Muislamu na mkazi wa Kijiji cha Makong’onda Wilaya ya Masasi Kwa tuhuma za kumjeruhi mke wake Kwa kumuingizia panga sehemu ya haja kubwa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara Kamishina msaidizi wa Polisi (ACP) Nicodemus Katembo, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo Agosti 8, 2023 majira ya saa 1 usiku,Kijiji na kata ya Makong’onda Wilaya ya Masasi Mkoa wa Mtwara.

Amesema kwamba mtuhumiwa jina (limehifadhiwa) pamoja na mhanga baada ya kutoka kwenye mihangaiko yao ya kuokota korosho mhanga alikwenda kwa binamu yake kutwanga kisamvu ambapo ni eneo jirani na wanapoishi”

Baada ya kukaa huko kwa muda mumewe alihisi kuwa amekwenda kwa mwanaume mwingine na baada ya kurejea alianza kumshambulia hadi kupoteza fahamu.

Kamanda amesema kuwa baada ya hapo mtuhumiwa (Jina limehifadhiwa) alichukua panga na kumuingizia muhanga sehemu ya haja kubwa na kumsababishia majeraha”.

Mhanga wa tukio hili anaendelea na matibabu katika hospitali ya Newala na hali yake inaendelea vizuri na mtuhumiwa anatarajia kufika mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili.

Aidha kamanda Katembo ametoa rai Kwa wananchi Kwa ujumla kuacha kushiriki vitendo vya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia unao husisha wivu wa mapenzi na hatua Kali za kisheria zitaendelea kuchukuliwa dhidi ya wahalifu dhidi ya vitendo hivi vya kikatili Kwa Jamii zetu