Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

BENKI ya NMB imewahakikishia Wafanyabiashara wakubwa Kanda ya Dar es Salaam wanaohudumiwa na taasisi hiyo, kuwa iko imara kipesa kukopesha mteja mmoja zaidi ya Sh.Bil. 300 na hii ni kutokana na kukua kwa mtaji wa benki hiyo unaokaribia kufika Sh. Trilioni 11.

Hayo yalibainishwa na Mkuu wa Idara ya Biashara wa NMB, Alex Mgeni, wakati wa Jukwaa la Wafanyabiashara hao ‘NMB Business Executive Network’, lililofanyika Dar es Salaam chini ya kaulimbiu ya; Mtandao Thabiti kwa Ukuaji Endelevu wa Biashara, likishirikisha zaidi ya wateja 100.

Jukwaa hilo la kila mwaka, limetumika kunadi bidhaa mpya za benki hiyo sokoni (ikiwemo Hati Fungani ya Jamii), kupokea maoni ya wateja hao, huku mada mbalimbali zikitolewa kwa washiriki, waliohakikishiwa kuwa, ufanisi wa NMB ni uthibitisho kuwa pesa za wateja wote ziko salama.

Akizungumza mbele ya mgeni rasmi wa jukwaa hilo, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, Mgeni alisema benki hiyo imeendelea kukua vema sio tu kimtaji, bali pia mtandao mpana wa matawi, Mashine za ATM na Mawakala kote nchini, tangu walipokutana na mtandao huo mwaka jana.

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo (kushoto), akipongezwa na Mkuu wa Idara ya Biashara wa Benki ya NMB, Alex Mgeni (katikati), baada ya kutoa hotuba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, wakati wa Jukwaa la Wafanyabiashara Wakubwa Kanda ya Dar es Salaam wanaohudumiwa na benki hiyo ‘NMB Business Executive Network’, lililofanyika jijini Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki. Kulia ni Meneja wa Benki ya NMB Tawi la Kariakoo, William Nkuna. (Na Mpiga Picha Wetu).

“NMB inafanya vizuri sokoni, na hii maana yake ni kuwa ufanisi wetu ni uthibitisho tosha kuwa pesa zenu, zikiwemo za wateja wengine wadogo na wa kati ziko salama. Tumeimarisha pia ushirikiano wetu na Serikali kwa kutoa kupitia Programu ya Uwekezaji kwa Jamii (CSI).

“Mwaka jana tulikutana hapa tukiwa na mtaji – kwa maana ya mali za benki zilikuwa na thamani ya zaidi Sh. Trilioni 9, leo tunakutana tena huku mtaji wetu ukiwa ni zaidi ya Sh. Trilioni 10 na tunakaribia 11,” alisema Mgeni mbele ya Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Omar Kumbilamoto.

Alibainisha kuwa faida moja wapo benki inapokuza mtaji, inaweza kuyahudumia makampuni makubwa yanayofanya biashara kubwa Tanzania, ambako kwa vigezo vya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), na kwa mtaji iliyonao NMB inaweza kukopesha hadi Sh. Bil. 300 hadi 350 kwa mteja mmoja.

“Kwa kanuni za BoT, tunaruhusiwa kukopesha chini ya asilimia 25 ya mtaji wetu, ambapo faida moja kubwa ukikopa ndani, gharama inakuwa ndogo na uzalishaji unakuwa mkubwa na bidhaa zitapatikana sokoni kwa bei nafuu, kulinganisha na mikopo inaypochukuliwa nje ya nchi na kampuni zenu.

“Kwa hiyo ni vema tunapokuza mtaji na kutanua wigo wa ukopeshaji wafanyabiashara wakubwa kwa ustawi wa biashara zao na unafuu wa bei za bidhaa, tunayafanya haya yote huku tukiendelea kutanua mtandao wa matawi yetu kufikia 230, huku tukipanga kufungua matawi sita zaidi.

“Hivi karibuni tutaongeza tawi Kariakoo, ambako tumegundua kuwa matawi yaliyopo pale yameelemewa. Tutafungua pia matawi zaidi jijini Dar es Salaam, ikiwemo Chanika, huku tukitanua mtandao wa mawakala wetu kutoka 21,000 tulionao sasa hadi kufikia 30,000 kabla ya mwisho wa mwaka.

Kwa upande wake, DC Mpogolo aliwashukuru Wafanyabiashara Wakubwa na wateja wote wa NMB kwa ujumla na kwamba mafanikio Chanya ya benki hiyo yametokana na mahusiano mema baina ya pande tatu – yani wateja, Serikali na NMB.

“NMB na wateja wakubwa ni miongoni mwa wawezeshaji wa Serikali, gawio kubwa la benki hii kwa Serikali la kiasi cha Sh. Bilioni 45, limetokana nanyi wafanyabiashara wakubwa, ambazo zimeenda katika usambazaji huduma mijini na vijijini, ikiwemo umeme, Barabara, maji na mengineyo.

“Hii ni benki salama kwenu, niwaombe muendelee kukopa na kufanya biashara na NMB, ikiwemo kuchangamkia Hati Fungani iliyo sokoni hivi sasa (NMB Jamii Bond), ili kuiwezesha kupata pesa za kukidhi mahitaji ya miradi ya maendelo ya jamii,” alisema DC Mpogolo.

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo (katikati), akiagana na  Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Dar es Salaam, Dismas Prosper (kushoto), wakati wa Jukwaa la Wafanyabiashara Wakubwa Kanda ya Dar es Salaam wanaohudumiwa na benki hiyo ‘NMB Business Executive Network’, lililofanyika jijini Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki. Kulia ni Mkuu wa Idara ya Biashara wa Benki ya NMB, Alex Mgeni. (Na Mpiga Picha Wetu).
 

Aliongeza kuwa, NMB ni kinara wa mahusiano mema na Serikali, ndio maana imekuwa msaidizi mkuu utatuzi wa changamoto za kijamii na kwamba mahusiano hayo yanamhakikishia mteja mkubwa uhuru wa kufanya biashara na benki hiyo iliyoimarisha ushirikiano hata na Jumuiya za Kimataifa.

Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, DC Mpogolo alikiri kuwa wafanyabiashara hao wanafanya kazi kubwa kuiunga mkono Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, aliyemtaja kama kinara wa kuifungua nchi kiuchumi kwa kujenga mahusiano mema na mataifa ya nje.

“Juzi Rais Samia ameenda India na Jopo la Wafanyabiashara wengi, ameenda na Taasisi za Fedha, nia kujenga mtandao sahihi wa ukuaji kiuchumi, ndio maana nasisitiza kuwa tuna kila sababu ya kumuunga mkono,” alibainisha huku akiwataka kuweka rekodi sa
fi za ulipaji kodi Serikalini.