Mwalimu mbaroni kwa kumjeruhi kwa fimbo mwanafunzi akimtuhumu kuiba maandazi

Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Mbeya

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linamshikilia mwalimu wa shule ya Sekondari Loiler iliyopo Mji Mdogo wa Mbalizi mkoani Mbeya,Peter Emmanuel (29),kwa tuhuma za kumshambulia fimbo mwanafunzi kwa madai ya kuiba maandazi matano.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga, amesema kuwa tukio hilo limetokea Februari 10,2023 katika Shule ya Sekondari Loiler mkoani Mbeya.

Kamanda amesema kuwa mtuhumiwa huyo pamoja na mlinzi wa shule hiyo Haruna Issa (30),mkazi wa Iwala walimshambulia kwa viboko sehemu mbalimbali za mwili mwanafunzi huyo wa kidato cha IV mwenye umri wa miaka 16,mkazi wa Mwangake na kumsababishia madhara.

Kamanda amesema kuwa watuhumiwa hao walimtuhumu mwanafunzi (jina linahifadhiwa) kuiba maandazi matano ambayo kila andazi ni linauzwa sh.300 hivyo jumla ya maandazi yote ni sh.1,500 katika duka la shule hiyo.

Kamanda amesema kuwa na mwalimu na mlinzi huyi walimshambulia kwa viboko na kumsababishia majeraha sehemu ya paji la uso, mkono wa kushoto na magoti yote mawili.

“Baada ya kumshambulia na kumjeruhi,siku hiyo ya tukio majira ya saa 5:00 usiku walimkimbiza Hospitali Teule ya Ifisi kwa ajili ya matibabu.

“Jeshi la Polisi kupitia wasiri wake lilipata taarifa na kufanya ufuatiliaji na kubaini kutokea kwa tukio hilo na hatimaye kuwakamata watuhumiwa wote wawili,” amesema kamanda.

Kamanda amesema kuwa upelelezi wa shauri hilo unaendelea na mara baada ya kukamilika watuhumiwa watafikishwa mahakamani muda wowote kuanzia sasa.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa wito kwa jamii kuacha mara moja tabia ya kujichukulia sheria mkononi kwani ni kinyume cha sheria.