Na Albano Midelo

ENEO la Masonya lililopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma lina utajiri wa utalii wa malikale na utambulisho wa Taifa kimataifa.

Nyumba aliyokuwa anafikia na kulala Rais wa zamani wa Msumbiji hayati Samora Machel katika eneo la Masonya wilayani Tunduru kuanzia mwaka 1966 hadi 1975 wakati wa harakati za ukmbozi wa nchi ya Msumbiji

Eneo hilo lenye ukubwa wa ekari 100 lina vivutio adimu vya utalii wa malikale ikiwemo nyumba yenye namba A 10 ambayo walikuwa wanafikia na kuishi Marais Hayati Julius Nyerere wa Tanzania na Hayati Samaro Machel wa Msumbiji kuanzia 1966 wakati wa harakati za ukombozi Kusini mwa Afrika.

Mkurugenzi wa Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Bartazar Nyamusya anasema viongozi hao pia wakiwa katika nyumba hiyo walitumia kibanda maalum kilichopo jirani ya nyumba hiyo kama chumba cha mawasiliano na nchi zilizokuwa katika harakati za ukombozi kusini mwa Afrika.

Masonya ni eneo la hifadhi ya Makumbusho ya kihistoria ya watu wa Msumbij,ambalo limesheni utajiri mkubwa wa historia ya Tanzania na namna Tanzania ilivyoshiriki katika harakati za ukombozi wa bara la Afrika.

Nyumba aliyokuwa anafikia na kulala baba wa Taifa Mwl.Julius Nyerere eneo la Masonya wilayani Tunduru wakati wa harakati za kuikomboa nchi ya Msumbiji kuanzia mwaka 1966 hadi 1975 Msumbiji ilipopata Uhuru

Jambo la kufurahisha zaidi eneo hili lina nyumba iliyotumiwa na Rais wa zamani wa Msumbiji hayati Samora Machel kuanzia mwaka 1966 hadi nchi hiyo ilipopata uhuru mwaka 1975.

Mkurugenzi wa Makumbusho ya Taifa ya Majimaji anasema mwaka 1966 Tanzania iliwapokea  wapigania uhuru wa Msumbiji na kuwakabidhi eneo la Masonya lililopo kilometa nane toka Tunduru mjini.

Hata hivyo anasema eneo hili limebaki kama eneo la makumbusho ambapo ametaja urithi unaopatikana katika eneo hilo kuwa ni nyumba mbili za viongozi wa kitaifa hayati Samora Machel Rais wa kwanza wa Msumbiji na Nyumba aliyokuwa anafikia baba wa Taifa hayati Julius Nyerere.

Nyamusya ameutaja urithi mwingine kuwa ni jengo moja la mawasiliano alilokuwa anatumia Rais Samora Machael,ukumbi wa semina aliokuwa anatumia Samora Machel kutoa mafunzo mbalimbali na majengo 11 ambayo kwa sasa ni madarasa ya wanafunzi wa sekondari ya wasichana Masonya.

“Maeneo mengine ya urithi ni mahandaki yaliyotumiwa na wapigania uhuru wa Msumbiji,eneo la bendera ya FRELIMO na eneo la mnara ulipofanyika mkutano wa wanawake wa Msumbiji tarehe 17/3/1973 ‘’, anasema Mkurugenzi wa Makumbusho ya Majimaji.

Kulingana na Nyamusya mwaka 1975 baada ya nchi ya Msumbiji kupata uhuru wapigania uhuru hao walirudi katika nchi kwao na kuanzia mwaka  1990 Halmashauri ya Tunduru iliamua kuanzisha shule ya sekondari ya wasichana Masonya ambayo hadi kufikia mwaka 2014 inachukua wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha sita.

Tito Mboma ni Mwalimu wa sekondari ya wasichana Masonya na Mtaalam wa Makumbusho ya Masonya,amesema Rais wa sasa wa Msumbiji Philip Nyusi amesoma shule ya msingi FRELIMO katika eneo la Masonya na kwamba alifika hapo mwaka 1970 akiwa na umri wa miaka nane.

Serikali hivi sasa inalitumia eneo la malikale la Masonya kwa shughuli za kielimu ambapo katika eneo hilo imejenga shule ya sekondari ya Masonya kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita.

Nyumba maalum iliyokuwa inatumika kama nyumba ya mawasiliano katika harakati za ukombozi kusini mwa Afrika,Baba wa Taifa Mwl.Nyerere na Samora Machel walikuwa wanatumia nyumba hii katika eneo la Masonya kwa kufanya mawasiliano yote muhimu kuanzia mwaka 1966 hadi 1975

Historia inaonesha kuwa kabla ya mwaka 1966,eneo la malikale la Masonya lilikuwa ni msitu ambapo katika mwaka huo ndipo serikali iliwapokea watu kutoka nchini Msumbiji na kuwakabidhi eneo hilo  katika kipindi chote cha kupigania uhuru nchini Msumbiji toka katika utawala wa Mreno.

Erick Soko ni Afisa Elimu Msaidizi Makumbusho ya Taifa ya Majimaji anasema tangu tangu wakabidhiwe eneo hilo la Masonya watu wa Msumbiji mwaka 1966,wamewahi kutembelea na kuishi kadhaa viongozi mashuhuri akiwemo Hayati Samora Machel ambaye alifika mara kadhaa wakati wa harakati za kupigania uhuru.

Soko anabainisha zaidi kuwa katika kipindi cha miaka kumi kuanzia 1966 hadi wanawake toka nchini Msumbiji wameishi katika eneo la Masonya na kwamba Umoja wa Wanawake wa Msumbiji uliojulikana kwa OMM ulianzia Masonya mwaka 1973.

Mwaka 1975 baada ya  uhuru wa Msumbiji kutangazwa ndipo kambi ya Masonya ilivunjwa na wanamsumbiji walirejea katika nchi yao,tangu mwaka 1975 hadi mwaka 1989 eneo hili lilibaki bila matumizi hadi mwaka 1990 ilipoanzishwa sekondari ya wasichana Masonya.

salia ya ukumbi aliyokuwa anautumia hayati Samaro Machel kutoa semina na  mafunzo ya kijeshi  uliopo eneo la Masonya Tunduru

By Jamhuri