Na Abel Paul wa Jeshi la Polisi

Askari wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha watakiwa kutojihusisha na ushabiki wa vyama vya siasa.

Hayo yamesemwa leo Januri 9, 2023 na Kamanda wa Polisi Kikosi cha Kuzuia wizi wa mifugo nchini Kamishina Msaidizi wa Polisi ACP Simon Pasua wakati wa hafla fupi ya kuwapongeza askari waliofanya vizuri zaidi mwaka jana mkoani Arusha.

Kamanda Pasua amesema kuwa askari wanapaswa kushabikia maswala mengine ya kijamiii kama vile michezo amewataka askari hao kujikita zaidi katika ulinzi wa raia na mali zao ili kuleta ufanisi na kupunguza manung’uniko ya wananchi.

Ameongeza kuwa waliopata zawadi wanao muda wa kuongeza juhudi ili mwaka mwingine waendele kupata zawadi hizo ikiwa ni pamoja na kupanda vyeo ambapo amewataka kufanya kazi kwa umoja ili kuleta ufanisi wa kazi za Polisi .

Kwa Upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Kamishina msaidizi wa Polisi ACP Justine Masejo amempongeza kamanda wa kikosi hicho kwa kutambua mchango wa askari wanaofanya kazi vizuri zaidi kazini.

Kamanda Masejo amebainisha kuwa Watanzania wanalitegemea sana jehhi hilo ambapo amebainisha kuwa askari waliofanya vizuri wataliwakilisha vyema jeshi ikiwa ni pamoja na wengine ambao wajapata zawadi hizo.

Nae askari wa kikosi hicho kutoka Makao Makuu ya Kikosi cha Kupambana na Kuzuia wizi wa mifugo Copolo wa Polisi CPL Silvester Mang’aha aliyepata zawadi kwa kufanya kazi vizuri mwaka 2022 amewashukuru askari wenzake ambapo amebainisha kuwa kitendo cha kupata zawadi hiyo ni mchango na ushirikiano kutoka kwa askari wenzake.

By Jamhuri