Bassirou Diomaye Faye, rais wa tano wa Senegal, ameapishwa kuwa rais katika hafla iliyofanyika katika mji mkuu, Dakar.

Mapema mwezi huu, Bw Faye mwenye umri wa miaka 44 alishinda uchaguzi uliocheleweshwa, na kupata 54% ya kura zilizopigwa, mbele ya mpinzani wake mkuu Amadou Ba.

Siku ya Ijumaa, Baraza la Kikatiba la nchi hiyo lilimthibitisha Bw Faye kuwa mshindi.

Wakuu wa nchi kutoka bara zima walihudhuria sherehe za kuapishwa, akiwemo Bola Tinubu, rais wa Nigeria na mwenyekiti wa kambi ya kikanda, Ecowas.