Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Kibaha

HALI ya mahudhurio kwa wanafunzi wa kidato cha kwanza na darasa la kwanza mkoani Pwani ni nzuri na inaridhisha ikiwa ni siku ya kwanza Januari 8 mwaka huu wakiripoti mashuleni.

Mkuu wa mkoa wa Pwani,Abubakar Kunenge ameridhishwa na mapokezi ya wanafunzi hao katika baadhi ya shule za sekondari na msingi halmashauri ya Mji wa Kibaha, mkoani hapo.

Akikagua hali ya mahudhurio kwenye shule ya sekondari ya wavulana ya Kibaha, shule ya sekondari Tumbi pamoja na shule ya msingi Amani iliyopo Miembesaba ,Kunenge alitoa maelekezo ya Serikali, kwamba mwanafunzi yeyote asisumbuliwe kuripoti kwasababu ya kukosa vifaa ama sare za shule.

Aidha aliwaasa watoto wa kike wasome na wapewe kipaombele.

Akiwa shule ya sekondari Kibaha, alieleza ni shule kimbilio la wazazi kwani wengi wanatamani watoto wao wasome katika shule hiyo.

” Na hii ni kutokana na ufaulu mzuri na mazingira bora ya kielimu yaliyopo ,Shule hii imetoa viongozi wakubwa akiwemo Rais mstaafu awamu ya nne dkt.Jakaya Kikwete “

Aliwataka wanafunzi wawe na nidhamu na maadili mema ,nawaasa fanyeni vizuri,someni ili kuwezesha kuja kujiajiri ama kuajiliriwa kwa manufaa yenu ya baadae.

Nae Mwalimu mkuu sekondari ya Tumbi, Fidelis Haule alieleza mwamko ni mkubwa, wanafunzi wa kidato cha kwanza wanaotakiwa kuripoti ni 279 ambapo hadi sasa wameripoti 241 .

Hata hivyo akielezea ufaulu ,anasema umeongezeka shuleni humo kutoka asilimia 50 hadi kufikia asilimia 80.

Alisema ,wanataka iwe shule ya mfano hivyo wamejiwekea kuwa na daraja la kwanza,A za kutosha.

Akielezea changamoto aliomba kuongezwa viti na madarasa mawili ili kukidhi mahitaji.

Akijibu baadhi ya changamoto ikiwemo upungufu wa walimu ,kuongezwa madaraja walimu Ofisa elimu mkoa wa Pwani, Sara Mlaki alieleza , Serikali inaendelea kushughulikia changamoto mbalimbali ikiwemo kupandisha madaraja walimu .

Mlaki alisema Serikali inatarajia kutangaza ajira kwa watumishi 23,000 nchini ambapo kati ya watumishi hao ni sanjali na walimu .

Kwa upande wake, mkurugenzi wa halmashauri ya mji wa Kibaha, Mshamu Munde alieleza, darasa moja limeshaongezwa na kuhusu kuongeza viti,baada ya wiki mbili vitapelekwa.

Mwanafunzi wa shule ya sekondari ya sekondari Kibaha, Moses Damas Canisio alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kujenga mazingira bora ya elimu ,kuongeza madarasa ,kuboresha miundombinu ,kuondoa ada na ujenzi wa mabweni na maabara .

By Jamhuri