Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Pwani

Tanzania ina kila sababu ya kujivunia namna ambayo imeweza kulinda na kuudumisha Muungano wetu.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani,alhaj Abubakar Kunenge alitoa kauli hiyo wakati akifungua Kongamano la miaka 59 ya Muungano wa Tanzania, lililofanyika katika ukumbi wa Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere,Kwamfipa Kibaha Mkoani Pwani.

Aidha Kunenge alisema kuwa ili kudumisha Muungano suala la Amani na utulivu lipewe kipaumbele.

Alieleza Serikali za awamu zote zimefanya kazi kubwa ya kudumisha Muungano uliopo na namna ambavyo wameweza kutatua changamoto za Muungano.

Mkuu huyo wa Mkoa alieleza yapo mataifa mengi na makubwa ambayo yameshindwa kudumisha Muungano wao lakini Muungano huu umedumu na kuwa wa mfano.
Aliwataka vijana, Wanafunzi na Watumishi kufahamu maana ya Muungano,kulinda amani na umoja tulionao.

“Vijana wa Leo wanapaswa kupata elimu juu ya historia ya kuundwa kwa Muungano, changamoto zilizokuwepo na namna viongozi wa Serikali walivyo na wanavyoendelea kupigania kutatua kero za Muungano kwa kiasi kikubwa”alieleza Kunenge.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliundwa Aprili 26, 1964 ikiwa ni Muungano wa Mataifa mawili huru ya Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar ambayo yaliingia mkataba wa Muungano mnamo mwaka 1964 na kuanzishwa Dola ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mkataba wa Muungano ulitiwa saini na aliyekuwa Rais wa Tanganyika, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, Aprili 22, 1964 huko Zanzibar.

By Jamhuri