Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule amesema kuwa moja kati kitu ambacho Rais Samia anatamani kukiona anapotembele katika kata ni kukutana na kero ambazo zipo nje ya uwezo wa afisa tarafa na mtendaji wa kata na sio zile ambazo wanauwezo wa kuzitafutia ufumbuzi.

RC Senyemule ameyasema hayo leo Novemba 20,2023 Jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo maafisa tarafa na watendaji wa kata ambapo amesema kuwa jambo hilo linawaumiza sana viongozi kutokana na mamlaka waliopewa watumishi hao.

“Jambo hili sio sawa mnajua serikali yetu imeisha elekeza vyema namna ya kufanya kila mtu kuanzia mtendaji wa kijiji, kata, tarafa kila mtu awe na nafasi ya kusikiliza kero na kuzitatua,” amesema Senyamule.

Pia amewataka watumishi hao kuwa na utaratibu wakufunga faili la kero kwani wengi wao wamekuwa na changamoto ya kutofunga na kupelekea kuwa na mrundikano wa kero hivyo kupitia mafunzo hayo watakuja na jawabu la namna ya kufanya ili kuweza kutatua hilo suala.

Sanjari na hayo ameongeza kuwa moja kati ya changamoto ambazo watumishi hao wanazo ni kukosa ubunifu wa kiuongozi katika usimamizi na uibuaji wa fursa za kiuchumi na kijamii zinazopatikana kwenye ngazi za msingi pamoja na ushirikishwaji wa wananchi na wadau wa maendeleo.

“Siku hizi ndiyo imekuwa mbaya zaidi kwasababu wale watendaji walikuwa wanajua wajibu wa kujenga shule ni kwenye kata ni wajibu wa kwao, baada ya serikali kuongeza uwezo kidogo wa kiuchumi na kuanza kupeleka katika baadhi ya maeneo huduma kila mtu amepumzika kazi kusema namimi nahitaji shule,” amesema Senyemule.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara za serikali za mitaa kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Bi.Angelista Kihaga amesema kuwa moja kati ya mada zitakazo tolewa katika mafunzo hayo ya siku mbili ni kuhusiana na utunzaji wa siri za serikali kwa watumishi hao wa umma.

“Tumeandaa mafunzo haya kwaajili ya watendaji wa kata, na maafisa tarafa wote nchi nzima yalikwishaanza na yalizinduliwa awamu ya kwanza yalifanyika katika Mikoa ya Mbeya na Mikoa mingine ya kanda ya Magharibi lakini sasa tunaendelea kwenye kanda ya kati lakini na kanda ya Mashariki kwahiyo zipo timu mbili,”amesema.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule,akisisitiza jambo kwa washiriki  wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo Maafisa Tarafa na Watendaji wa kata yanayofanyika jijini Dodoma.

Sehemu ya washiriki wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule, wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo Maafisa Tarafa na Watendaji wa kata yanayofanyika jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara za serikali za mitaa kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Bi.Angelista Kihaga,akielezea umuhimu wa mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo Maafisa Tarafa na Watendaji wa kata yanayofanyika jijini Dodoma