Ruvuma yafanikiwa kutoa chanjo ya Polio kwa asilimia 122.2

MKOA wa Ruvuma umefanikiwa kutoa chanjo ya polio kwa Watoto 398,029 sawa na asilimia 122.2.

Katibu Tawala Msaidizi ,Huduma za Afya,Lishe na Ustawi wa Jamii Mkoani Ruvuma Dr.Lous Chomboko amesema Mkoa ulilenga kuchanja Watoto 325,746 katika awamu ya tatu ya kampeni dhidi ya chanjo ya polio iliyoanza Septemba Mosi hadi Septemba nne 2022.

“Utekelezaji wa kampeni ya utoaji chanjo ya polio ya matone awamu ya tatu kwa Watoto chini ya miaka mitano umefanyika kwa mafanikio makubwa,mikakati yetu ni kuongeza wigo wa ufuatiliaji toka ngazi ya Mkoa hadi Halmashauri ili kudhibiti kabisa polio’’,alisisitiza Dr.Chomboko.

Amesema serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Shirika la Afya Ulimwenguni WHO lilitangaza uwepo wa mlipuko wa ugonjwa wa polio Februari 17,2022 katika jiji la Lilongwe nchini Malawi,hivyo Tanzania iliamua kufanya kampeni ya utoaji chanjo dhidi ya polio kwa Watoto chini ya miaka mitano ili kuudhibiti.

Mkoa wa Ruvuma ulikuwa kinara kitaifa katika utoaji chanjo ya polio kati ya mikoa minne ya awamu ya kwanza iliyotekeleza kampeni ya polio,mwaka 2021 kwa kufanikiwa kutoa chanjo ya polio kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano kwa asilimia 122 .

Mgonjwa wa mwisho wa polio aligundulika nchini Tanzania katika Mkoa wa Mtwara mwaka 1996.

Imeandikwa na Albano Midelo ambaye ni Afisa Habari Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Ruvuma