📍NIRC: Arusha.

Katika jitihada za kumkomboa mkulima mdogo kutokana na utegemezi wa mvua, Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) inaendelea na mpango wa kuchimba visima 67,000 nchi nzima, mradi utakaozalisha maelfu ya ajira kwa vijana na kuleta uhakika wa chakula.

Akiwasilisha mikakati hiyo katika Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma Mwaka 2026 jijini Arusha, Mkurugenzi Mkuu wa Tume hiyo, Bw. Raymond Mndolwa, amebainisha kuwa mpango huo ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mara alipozindua mradi wa uchimbaji wa visima kwa wakulima wadogo katika maonesho ya kilimo Nanenane yaliyofanyika jijini Mbeya Mwaka 2023

Bw. Mndolwa ameeleza kuwa lengo kuu la mpango huo ni kuwawezesha wakulima wadogo kupata uhakika wa maji kwa ajili ya uzalishaji wa mwaka mzima. Amebainisha pia kuwa mradi huu unalenga kufikisha huduma za Umwagiliaji kwa makundi ambayo hayapo katika mfumo rasmi wa skimu za Umwagiliaji, hatua itakayoongeza uzalishaji, ajira na kipato cha wakulima na nchi kwa ujumla.

“Kupitia utekelezaji wa mpango wa uchimbaji wa visima na usambazaji wa pampu, Tume inatarajia kutengeneza ajira kwa vijana kati ya 2,000 hadi 4,000,” imeeleza sehemu ya wasilisho hilo. Pia, mpango utajenga uwezo wa vijana katika kutekeleza na kusimamia miradi ya Umwagiliaji.

Ili kufanikisha azma hiyo, Serikali inatoa ruzuku katika hatua mbili muhimu ambazo ni uchimbaji wa visima na ununuzi wa pampu za kusukuma maji. Ufungaji wa mifumo hii utahusisha vijana wanaosoma fani zinazohusiana na uandaaji wa mifumo hiyo. Kila kisima kimoja kinachochimbwa kina uwezo wa kuhudumia takribani wakulima 16 na kina uwezo wa kumwagilia hadi ekari 40 ambapo utambuzi wa maeneo yanayonufaika unafanyika kwa ushirikiano wa karibu kati ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji na Halmashauri za Wilaya.

Akifafanua kuhusu mafanikio ya utekelezaji wa mpango huo hadi sasa, Bw. Mndolwa amebainisha kuwa visima 390 tayari vimechimbwa katika mikoa 15 nchini. Katika hatua nyingine, Serikali imenunua jumla ya pampu 2,000, ambapo pampu 1,000 tayari zimepokelewa na kusambazwa huku mikoa iliyonufaika na usambazaji wa pampu hizo hadi sasa ikiwa ni Mwanza, Mara, Kagera, Kigoma, Simiyu, Geita, na Katavi.

Ameongeza kuwa kupitia hatua hii, wakulima 15,022 wamenufaika, wakijumuisha wanawake 6,335 na wanaume 8,702 kutoka katika vikundi 769, huku eneo ambalo linatarajiwa kumwagiliwa katika hatua ya awali likiwa ni ekari 13,518.75.

Aidha tume inatekeleza hayo ikiwa ni katika sehemu ya majukumu yake ya msingi ya kuratibu, kuendeleza na kusimamia maendeleo ya sekta ya Umwagiliaji nchini, huku jumla ya miradi 146 ya ujenzi na miradi 634 ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa skimu na mabwawa ya Umwagiliaji pia yakiendelea nchi nzima

Tume inaendelea kushukuru wadau kwa ushirikiano wakiwemo Halmashauri zote 184 pamoja na taasisi mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) na vyuo vingine vya ufundi nchini.