Serikali yatangaza mlipuko wa surua,wagonjwa 54 wathibitika

Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Dodoma

Waziri Wa Afya Ummy Mwalimu, amethibitisha kuibuka kwa ugonjwa wa surua lubela nchini na kubainisha kuwa mpaka sasa wataalamu wamebaini wagonjwa 54 kutoka mikoa mbalimbali.

Hayo ameyasema leo Septemba 15,2022 jijini Dodoma, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu ongezeko la wagonjwa wa Surua nchini.

Waziri Ummy amesema kuwa kati ya wagonjwa 54 waliothibitika kuwa na surua kati ya wagonjwa hao 48 ni watoto chini ya miaka 15 huku Halmashauri saba (7) zikiwa na wagonjwa wengi.

” Wizara inaendelea na ufuatiliaji wa Magonjwa na tetesi katika ngazi ya Jamii, kutumia timu kwenda kweny maeneo yaliyoathirika kwa kuwa na Wangonjwa wengi pamoja na kutoa elimu kwa watoa huduma za afya na jamii kwa ujumla kuhusu dalili na jinsi ya kujikinga na ugonjwa huu”, amesema.

“Ugonjwa huu hauna tiba maalum bali matibabu hutolewa kuoingana na dalili zinazojitokeza, na ugonjwa huu usipodhibitiwa mapema huweza kuleta madhara katika masikio au kusababisha homa ya mapafu, upofu wa macho, homa ya Uti wa mgongo na kupelekea kupoteza maisha” amesema Ummy

Aidha amesema ongezeko la wagonjwa wa Surua Nchini Wizara imefanya tathmini ya mwenendo wa utoaji wa Chanjo za Watoto Nchini ili kubaini idadi ya Watoto wanaooata na kukamilisha chanjo kwa kuzingatia ratiba.

“Kwa tathmini iliyofanyika kwa kuchambua takwimu za miaka mitatu mfululizo yaani mwaka 2019, 2020 na 2021, imeonyesha kuwa kiwango cha utoaji wa chanjo za Watoto Nchini kimeshuka na kinaendelea kushuka”

“Kwa kipindi cha kuanzia 2019 hadi Julai 2021 imebainisha kuwa zaidi ya Watoto laki nne wenye umri chini ya miaka mitano hawajapata chanjo kabisa pia lipo kundi kubwa la Watoto hawajakamilisha chanjo na Mikoa yenye Watoto wengi ambao hawanapata chanjo ni Kigoma, Kagera, Mara, Songwe, Manyara, na mbeya na Mikoa yenye Watoto ambao hawajakamilisha chanjo ni Tabora, Dar es salaam, Arusha, Geita, Rukwa, Shinyanga, Manyara, Pwani, Singida, Ruvuma, Dodoma, Kigoma, Morogoro, Lindi, Songwe, Mtwara, Katavi, Iringa na Mbeya”. amesema Ummy

Amesema nchi ipo katika hatari ya kupata milipuko ya magonjwa husani yale yanayozulika kwa chanjo kutokana na uwepo wa idadi kubwa ya Watoti ambao hawajapata chanjo na ambao hawajakamilisha chanjo.

Ameongezea kwa kutoa rai kwa Umma kupeleka Watoto kwenye vituo vya kutolea huduma za afya ili wapatiwe chanjo ya Surua kukingana na umri wao.

“Ni muhimu kwa Wazazi na Walezi kuhakikisha kuwa Watoto wao wanapata dozi zote za chanjo dhidi ya ugonjwa wa surua wanapofikia umri huo
Ninawahimiza wazazi na Walezi kuhakikisha kuwa Mtoto yeyote mwenye dalili ya homa na vipele apelekwe kwenye kituo cha kutolea huduma za Afya”, amesema Ummy.