KAMISHNA wa Maadili Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Jaji Mstaafu, Harold Nsekela

KAMISHNA wa Maadili Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Jaji Mstaafu, Harold Nsekela, amesema sheria ya maadili ya viongozi wa umma kupitia kifungu cha 9 (1) (b) inamtaka kiongozi wa ummma kila ifikapo mwisho wa mwaka kupeleka kwa kamishna wa maadili tamko la maandishi katika hati rasmi inayoorodhesha mali au rasilimali zake na za mwenza wake, watoto wake wenye umri usiozidi miaka 18 na ambao hawajaoa au kuolewa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Nsekela ameeleza kwamba mwisho wa kupokea fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni mwisho wa kupokelewa ni Desemba 31, 2017 na kwa mtu ambaye bado hajapata fomu hizo anaweza kuingia tovuti ya sekretarieti hiyo ya www.ethicsssecretariat.go.tz.

“Kwa kuzingatia kifungu cha 9(1) (a) na (c) cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, viongozi wapya wanaochaguliwa au kuteuliwa wanatakiwa kujaza fomu hizo na kuzirejesha kwa kamishna wa maadili ndani ya siku thelathini baada ya kupewa wadhifa. Kiongozi anapofika mwisho wa kutumikia wadhifa wake, anatakiwa kujaza fomu za tamko la rasilimali na madeni na kuziwakilisha kwa kamishna,” alisema Nsekela.

Naye Ofisa Sheria Mkuu wa Sekretarieti hiyo, Filotheus Manula, amefafanua kuwa kutokupeleka viongozi katika Baraza la Tume ya Maadili ya Utumishi wa Umma kwa ajili ya kuhojiwa juu tuhuma mbalimbali, kwao ni sifa kuonyesha kwamba katika utumishi wa umma kuna maadili mema.

By Jamhuri