Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Shirika la Umeme Nchini TANESCO limetakiwa kukamilisha kwa wakati mradi wa ujenzi wa Miundombinu ya umeme wa chini unaoendelea katika mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Hayo yamesemwa leo Tarehe 21 Septemba 2023, na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi alipokuwa katika ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya Ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba.

Dkt. Yonazi amesema kuwa,TANESCO wana jukumu la usimamizi wa karibu na ulazima katika ujenzi wa Miundombinu ya nishati ya umeme katika Mji wa Serikali kwani baada ya muda mfupi ujao mahitaji ya umeme yatakuwa makubwa kutokana na Agizo la Serikali kuzitaka Ofisi zote za Serikali Jijini Dodoma kuhamia Mtumba mapema ifikapo January Mosi mwakani.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulika na Sera, Bunge na Uratibu Dkt, Jim Yonazi akizungumza na Mhandisi wa TANESCO, Richard Kafura Wakati akikagua mfumo wa ujenzi wa miundo mbinu ya Umeme katika Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma.

Sambamba na hilo Dkt. Yonazi amelitaka Shirika hilo kuvipa vipaombele viwanda vya ndani kwakununua bidhaa zinazofaa kununuliwa nchini katika viwanda hivyo.

“Mnafahamu kuwa kuna changamoto ya kiuchumi duniani kote hivyo hatuwezi kununua nje kila kitu; vitu ambavyo vinaweza kununuliwa ndani ya nchi vununuliwe ndani ya nchi, ili kupunguza upelekaki wa fedha za Tanzania nje, ni vizuri kuhusisha viwanda vya ndani ambavyo vinawezekana kutoa huduma vitoe huduma.” Alifafanua Dkt. Yonazi

Akiendelea Kusisitiza kuhusu suala la Ubora na muonekano wa Ujenzi unaendelea katika Mji wa Serikali Dkt. Yonazi alisema ni muhimu kuzingatia maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya huduma nyingine akitolea Mfano Miundombinu ya Umeme, Maji na mawasiliano na kutoa wito kwa kila Mkandarasi katika eneo kufuata Mpangokazi ambao ulikuwa umewekwa, na alisisitiza suala zima la kuzingatia muda wa umaliziaji wa kazi.

“Tunakumbuka Agizo la Serikali linataka watumishi kuhamia Mtumba ifikapo Tarehe 1 Januari 2024, hivyo ni muhimu kuhakikisha kwamba majengo yanakwenda vizuri katika umaliziaji na kuweka huduma ambazo ni muhimu.” amebainisha

Akiongea katika ziara hiyo, Mhandisi Richard Kafura kutoka Shirika la Umeme nchini TANESCO alisema,Ujenzi wa mradi huo unatekelezwa na Serikali kupitia TANESCO kwa kushirikiana na mkandarasi DERMO Contruction Limeted. Ambapo mpaka sasa ujenzi wa mifereji ya kupitishia miundombinu ya umeme na Mfumo wa umeme wa ardhini unaendelea kutekelezwa na Mkandarasi

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulika na Sera, Bunge na Uratibu Dkt, Jim Yonazi akizungumza na Msimamizi Mkuu wa miradi ya Ujenzi kutoka Chuo Kikuu cha Ardhi Mhandisi Anania Saudeni, wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) katika Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma.

By Jamhuri