Mwanamuziki wa Uganda, Moses Ssekibogo ‘Mowzey Radio’ enzi za uhai wake.

MWANAMUZIKI nyota nchini Uganda, Moses Ssekibogo maarufu kama Mowzery Radio, amefariki. Habari zilizothibitishwa na familia yake na mmoja wa mameneja wake aitwaye Balaam Barugahare, kwa vyombo vya habari, zinazema Mowzery amefariki asubuhi ya leo akiwa katika Hospitali ya Case mjini Kampala.

“Ndiyo, Radio amefariki asubuhi hii,” alisema Barugahare katika mahojiano ya simu. Mowzey Radio alilazwa hospitalini wiki iliyopita baada ya kupata majeraha wakati wa mapigano katika baa moja mjini Entebbe ijulikanayo kama De Bar, ambapo Radio alipigwa na kupoteza fahamu.

Kifo hicho kimetokea saa chache baada ya Rais wa Uganda, Yoweri Museveni kutoa mchango wa Sh. milioni 30 za Uganda kwa ajili ya matibabu ya mwanamuziki huyo.

“Uongozi wa Hospitali ya Case unathibitisha kupokea malipo ya UGX 30,000,000 kutoka kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Uganda @KagutaMuseveni. Tunamshukuru kwa mchango wake huo wa kugharamia matibabu kwa mwanamuziki nyota wa Uganda, Radio,” ilisema sehemu ya taarifa kutoka Hospitali ya Case.

Wiki iliyopita, polisi walisema walikuwa wamewakamata watu watano katika uchunguzi kuhusiana na kupigwa kwa Radio. Mowzery Radio aliyekuwa sehemu ya kundi la Radio and Weasel, alitoa vibao vikali kama vile ‘Bread and Butter, ‘Zuena’, ‘Magnetic’, miongoni mwa vingine vingi.

By Jamhuri