Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Arusha

Wamiliki wa vyombo vya habari na wanahabari kwa ujumla hapa nchini, wameshauriwa kuitumia Teknolojia mpya ya kimtandao inayojulina kama Akili bandia (Artificial Intelligence), ili kukabiliana na changamoto ya uchumi na uhaba wa rasrimali watu katika vyombo binafsi vya habari.

Ushauri huo umetolewa leo Oktoba 24, 2023 na mtafiti wa masuala ya habari kutoka Taasisi ya Nukta Africa, Nuzulack Dausen, alipokuwa akiwasilisha mada katika mdahalo uliofanyika katika Wiki ya AZAKI inayoendelea Jijini Arusha.

Dausen amesema kuwa wakati umefika kwa Waandishi wa Habari kuhakiki habari kwa kutumia nyenzo za Teknolojia kama vile akili mnemba (AI), ili kuwa na usahihi wa habari na matukio kwa kutumia google lens kutambua mazingira na picha sahihi.

“Teknolojia hii ni nzuri na inarahisisha utendaji kazi kwa ufasaha, hivyo watu hawapaswi kuogopa matumizi ya AI ” amesema Nuzulack.

Aidha, amewatahadharisha watengenezaji wa Habari za uchunguzi kutoweka habari hizo kabla ya uchunguzi kukamilika katika mfumo wa AI kwa lengo la kuhakiki habari zao kwani kwa kufanya hivyo habari hizo zinaweza kudukuliwa na walishaji au wasimamizi wa programu hiyo na badala yake watumie njia za kawaida.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) Dkt. Rose Reuben, amesema kuwa ukuaji wa Teknolojia umerahisisha utoaji wa Habari na kuwawezesha wananchi kupata taarifa kwa wakati.

Wiki ya AZAKI inaendelea kwa siku ya pili katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (AICC), tangu ilipozinduliwa rasmi Octoba 23, ambapo inatarajiwa kufikia tamati 0ctoba 27, 2023, Jijini Arusha.

By Jamhuri