Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Hospitali ya Taifa Muhimbili na Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Amana Amana zimesema upatikanaji wa dawa na vifaa tiba kwa sasa ni asilimia 97.

Akizungumza jijini Dar es Salaam Mfamasia wa Hospitali ya Muhimbili Nelson Faustine amesema hali ya upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika taasisi hiyo imeimarika na wameshuhudia mabadiliko makubwa yaliyofanyiwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

“Tumetoka asilimia 30 hadi zaidi ya asilimia 97 upatikanaji wa dawa katika hospitali yetu ya Muhimbili Upanga na Mloganzila ni hatua kubwa idadi ya wagonjwa imeongezeka kulingana na bajeti.Kwa sasa manunuzi yetu ya dawa kwa MSD ni zaidi ya Sh.bilioni 6 kwa mwezi na kwa mwaka ni zaidi ya Sh. bilioni 24,”alisema.

Ametoa mwito kwa Serikali kuhakikisha inaiongezea mtaji MSD kama ambavyo iliahidi na kufuta madeni ya nyuma, lengo ni kuwezesha taasisi hiyo kujiendesha.

Nelson aliitaka taasisi hiyo ikiwa ni kati ya wateja wakubwa kwa MSD wanapata huduma kwa kipaumbele cha pekee.

Pamoja na hali hiyo wameitaka MSD kuhakikisha maboresho ya huduma Muhimbili hususani huduma za kibobezi yanaendana na mahitaji ya dawa na vifaa tiba vyake kama vya kupandikiza figo, uboho na uroto ambapo chupa moja ndogo ya dawa hizo ni hadi sh milioni 3.

Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa Amana Dk.Brayson Kiwelu alisema mafanikio makubwa yaliyopo yamechagizwa na Rais Dk. Samia kutokana na maboresho aliyoyafanya sekta ya afya.

“Amana imeweza kupata zaidi ya sh bilioni 5 ambazo zimewekezwa katika jengo la kisasa la Ct Scan, X ray, jengo la dharula, ukarabati wa jengo la wagonjwa mahututi na maboresho kitengo cha usafishaji damu kwa wagonjwa wa figo.

“ Ukarabati huu umeendana na uwekezaji wa vifaa ambapo asilimia 70 ni kutoka MSD, tunajivunia hali ya utoaji huduma ambapo upatikanaji wa dawa ni zaidi ya asilimia 97 changamoto ni dawa za wagonjwa wa saratani ambapo hata hivyo tuna kifungu cha bajeti ya dharula tunazonunua dawa ambazo hazipo.

By Jamhuri