Brad Gordon

Naomba kuweka wazi kuwa, pamoja na juhudi za mazungumzo kati yetu na Serikali ya Tanzania, hakuna makubaliano yoyote ya kulipa kama vyombo vya habari vinavyoendelea kuripoti. Kile kilichowasilishwa katika ripoti za kamati ya kwanza na ya pili siyo matokeo sahihi, licha ya kile kinachoelezwa na kuaminika na wengi.
Hatujawahi kuiba, hatujawahi kukwepa kodi, hatujawahi kughushi nyaraka kukwepa kulipa mirabaha na hatujawahi kuendesha shughuli zetu kinyume cha sheria. Nitaeleza hapa chini kwanini madai yaliyotolewa jana siyo ya kweli na kwa nini Mheshimiwa Raisi kwa mara nyingine amekabidhiwa taarifa isiyokuwa sahihi na Kamati yake. Tunaendesha shughuli za Acacia kama kampuni ya kimataifa, na kutarajia watu wetu wote kuwa na uadilifu wa hali ya juu. Tuhuma dhidi yetu haziwezi kuwa na ukweli wowote.

Tuziangazie tuhuma hizi kwa ukaribu zaidi: tumetuhumiwa kuendesha shughuli zetu kinyume cha sheria kwa miaka 19 iliyopita kwani kampuni ya Acacia Mining plc haijasajiliwa nchini. Hatuendeshi shughuli zetu kinyume cha sheria. Migodi yetu inamilikiwa na kuendeshwa na kampuni zilizosajiliwa nchini Tanzania na zinazotambulika kwa mujibu wa sheria. Kampuni hizi (Pangea Minerals Limited, Bulyanhulu Gold Mine Limited na North Mara Gold Mine Limited) zinalipa kodi zote stahiki na huwasilisha taarifa zake za mapato kwa TRA. Kampuni hizi kwa ujumla wake humilikiwa na Acacia Mining plc, ambayo ni kampuni mama ya kundi la makampuni ya Acacia. Acacia ni chapa ya kampuni nchini Tanzania. Acacia group inajumuisha makampuni mbalimbali duniani kote, ikiwa ni pamoja na nchi nyingine za Afrika ambapo tuna miradi: Kenya, Burkina Faso na Mali.

Acacia ni kampuni iliyoanzishwa na kusajiliwa nchini Uingereza. Naomba ifahamike kuwa tumekuwa tukijaribu kuielezea TRA kwa miaka kadhaa kwamba Acacia Mining PLC ni kampuni iliyoorodheshwa katika masoko ya hisa ya London na Dar es Salaam na inamilikiwa na mamia ya wanahisa. Muundo huu wa uendeshaji ni sawa na ule uliopo katika makampuni mengi ya kimataifa yanayoendesha shughuli zake nchini Tanzania na haupo kinyume cha sheria wala haujalenga kukwepa kodi kwa njia yoyote ile. Muundo huu pia sio suala la siri. Tumekua tukitoa taarifa juu ya muundo huu kwa umma katika taarifa zetu zilizofanyiwa ukaguzi za mwaka, na kwa TRA na kwa wakala wengine wa serikali. Muundo huu uliunda sehemu ya mafungamano “memorandum” yaliyopitishwa na Mamlaka ya Masoko ya Hisa na Mitaji (CMSA) wakati wa kipindi cha uorodheshwaji katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) mwaka 2011.

Tulituhumiwa pia kwa kutokulipa kodi inayofikia dola bilioni 50 za Marekani (Sh trilioni 110). Hii sio kweli. Hebu tuweke namba hii katika mtazamo. Kama idadi hii ni sahihi, na kwa kutumia kiwango rahisi cha kodi cha 30% ya mauzo (ambayo siyo faida inayokatwa kodi) ingeashiria kuwa tumekuwa na mauzo ya zaidi ya dola bilioni 150 za Marekani (Sh trilioni 330) kwa miaka 15 iliyopita. Kuweka rekodi sawa – kama hii ingekuwa na ukweli, tungekuwa kampuni kubwa ya uchimbaji ulimwenguni (sio madini ya dhahabu tu).
Kampuni kubwa ya uchimbaji madini duniani ni BHP ambayo ina karibu migodi 20 katika nchi 10 na ina thamani ya zaidi ya dola bilioni 90 za Mareksni (Sh trilioni 200). Ni dhahiri kwamba hii haiwezi kufikiwa na migodi yetu mitatu. Thamani ya kampuni yetu kwa ujumla hadi kufikia leo ni karibu dola bilioni 1.2 za Marekani (Sh trilioni 2.6) na tunaombwa kodi inayofikia dola bilioni 50 za Marekani (Sh trilioni 108). Haileti maana.

Taarifa kutokana na matokeo ya Kamati ya Pili
Kwa uhalisia jumla ya mapato tuliyopata kutoka Bulyanhulu na Buzwagi tangu tumeanza uzalishaji ni chini ya dola bilioni 6 za Marekani (Sh trilioni 13.2), hii ikijumuisha tofali za dhahabu. Kama ni makinikia pekee, thamani yake ni dola bilioni 3.3 za Marekani (Sh trilioni 7.2) kwa takribani miaka 15.
Kama mnavyofahamu, tunakaguliwa hapa nchini na kimataifa (na kampuni za ukaguzi zinazotambulika kimataifa zinazokagua kampuni nyingi katika sekta tofauti duniani kote), huku tukiuza tunachozalisha kwa wafanya biashara na wachenjuaji wanaotulipa thamani halisi ya kinachopatikana na kukitangaza kwa uwazi. Tungeweza vipi kukwepa kodi yenye thamani mara kumi ya mauzo yetu? Hili lisingewezekana.

Sitaelezea tuhuma zote hapa, ila nataka kueleweka, tumetangaza kila tunachozalisha na kuuza. Kwa mfano, hatujajaribu kuficha idadi ya makontena tunayouza. Hata hivyo hili lisingewezekana ukichukua idadi kampuni na taasisi za serikali zinazohusika katika usafirishaji, kushughulikia huduma za bandarini, usafirishaji kwa meli na uchenjuaji.
Siku ya jana [iliposomwa ripoti ya pili] ilikuwa ya kufedhehesha na kusikitisha kwa kuwa inatishia uhai wa kampuni yetu. Matokeo ya uchunguzi wa kamati ya pili unaonekana kutegemea matokeo uchunguzi wa kamati ya kwanza ambayo tumerudia kupingana nayo, na hayashabihiani na vipimo vilivyofanywa kwa miaka zaidi ya 20 na vyombo huru vya utafiti vya kitaifa na kimataifa zikiongeza kwa kiasi kikubwa kiasi cha madini katika makontena. Tunapiga matokeo ya uchunguzi wa kamati ya pili, kama tulivyopinga matokeo ya uchunguzi wa kamati ya kwanza.

Tumeomba nakala ya ripoti ya kwanza ya uchunguzi ili kujaribu kuelewa jinsi walivyofikia matokeo yao, lakini kwa bahati mbaya, bado hatujafanikiwa kuona ripoti hiyo. Pia tumeomba kupata nakala ya ripoti ya kamati ya pili ili tuweze kuelewa matokeo yaliyotangazwa jana [Juni 12], huku tukitarajia Serikali itatupatia nakala za ripoti hizi. Tumeomba ukaguzi huru wa makinikia ili kuweza kuondoa dhana iliyojengeka kuwa tunaiba, wakati hatujashiriki katika wizi wowote; ombi hili bado halijatekelezwa.
Kwa mwenendo wa shughuli ya jana [Juni 12] na ripoti katika vyombo vya habari leo [Juni 13], imedhihirika kwamba tunaonekana kama siyo wazalendo, huku tukiiba madini ya watanzania kwa mikataba mibovu. Hii si kweli, sisi ni mashujaa wa uchimbaji madini Tanzania. Miaka ya hivi karibuni tumefanya mabadiliko ya hiari katika mikataba iliyotiliwa sahihi miaka ya nyuma ili kuhakikisha faida zaidi inawafikia watanzania, hata kabla ya wawekezaji waliolipia gharama za migodi hii kujengwa, hawajalipwa gharama zao za uwekezaji. Tumekuwa tukilipa kodi kabla ya muda, huku tukiongeza viwango vya tozo za mrahaba, na tozo za ushuru wa huduma na kuwekeza zaidi katika jamii zinazotuzunguka, kuliko kampuni zozote za madini zikijumuishwa. Tuna Watanzania wengi katika nafasi za juu ndani ya kampuni zetu, huku zaidi ya asilimia 96 ya wafanyakazi katika migodi yetu ni Watanzania. Watumishi hawa wamepatiwa mafunzo ya hali ya juu na kuendelezwa kwa miaka mingi, huku tukiwa tumewezesha wataalamu wanaoongoza katika fani mbalimbali hapa nchini.

Ilivyo sasa, matokeo yasiyo sahihi yaliyochukuliwa kutoka katika sampuli zilizochaguliwa kutoka makontena 44 kati ya maelfu yanatumika kuharibu sifa ya mwekezaji mkubwa wa kimataifa, ambaye pia ni moja ya waajiri wakubwa katika sekta binafsi na mmoja wa walipa kodi wakubwa nchini. Tumewekeza zaidi ya dola bilioni 4 za Marekani (Sh trilioni 8.8) katika nchi hii katika ujenzi na uendelezaji wa migodi yetu, huku tukitumia zaidi ya dola bilioni 3 za Marekani (Sh trilioni 6.6) kwa wafanyabiashara wa Kitanzania kusaidia kuendesha biashara yetu na kulipa zaidi ya dola bilioni 1 za Marekani (Sh trilioni 2.2) kulipia kodi na mrabaha.
Sisi ni washirika wa muda mrefu wa Tanzania na tumekuwa tukifuata sheria. Tunaamini tuna nafasi ya kushirikiana na Serikali katika kufikia lengo moja la kuwezesha Watanzania kufikia malengo ya maendeleo. Tutaendelea kutafuta mwafaka kupitia mazungumzo na Serikali. Kama haitawekezana, itakuwa ishara mbaya kwa wawekezaji waliopo sasa na wanaotazamia kuwekeza nchini. Naamini ukweli utatawala na nitaendelea kujaribu kufanikisha hilo. Mpaka hatua hiyo, naomba muendelee kustahimili na kuwa salama.

Mwandishi wa taarifa hii, Brad Gordon, ni Ofisa Mtendaji Mkuu Acacia

By Jamhuri