Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Waganga Wafawidhi wa Hospitali za Rufaa za Mikoa ya Temeke, Amana, Mwananyamala na Iringa wamewapongeza watoa huduma wa Hospitali ya Taifa Muhimbili hasa Wauguzi kutokana na huduma nzuri wanazotoa kwa wananchi wanaolazwa katika wodi mbalimbali.

Hayo yamesemwa leo na Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa, Dkt. Alfred Mwakalebela ambaye amelazwa Hospitalini hapa wakati akiwaelezea jinsi anavyoendelea vizuri na matibabu Waganga Wafawidhi wenzake Dkt. Bryceson Kiwelu (RRH-Amana), Dkt. Joseph Kimaro (RRH-Temeke), Muuguzi Mfawidhi (RRH-Temeke) Bi. Nuswe Ambokile pamoja na Dkt. Zavery Benela kutoka (RRH-Mwananyamala).

Dkt. Mwakalebela amewaambia wenzake kuwa tangu amefika hospitalini hapa amehudumiwa vizuri kila mahali alipopita kuanzia idara ya magonjwa ya dharura, kwenye vipimo vya maabara na radiolojia na kuongeza kuwa amefanyiwa vipimo vingi na kupata majibu yake ndani ya muda mfupi.

“Nimekaa hapa nimejifunza mengi hasa kutoka kwa wauguzi, naulizwa na kuelekezwa vizuri kabla ya kupatiwa huduma ikiwemo dawa, nimeiona huduma kwa mteja jinsi inavyotolewa hapa” amesisitiza Dkt. Dkt. Mwakalebela.

Nao, Dkt. Bryceson Kiwelu (RRH-Amana), Dkt. Joseph Kimaro (RRH-Temeke), Muuguzi Mfawidhi (RRH-Temeke) Bi. Nuswe Ambokile pamoja na Dkt. Zavery Benela kutoka (RRH-Mwananyamala) wameipongeza Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa maboresho mengi yaliyofanyika na kuahidi kuja kufanya ziara rasmi ya kujifunza mambo mbalimbali ili waweze kuyatekeleza katika maeneo yao.

By Jamhuri