Rais Uhuru Kenyatta ametangaza neema kwa wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kuruhusu kuingia nchini humo kwa kutumia kitambulisho cha taifa tu na kupewa haki zingine kama raia wa Kenya.

Taarifa hiyo imetolewa leo na Rais Uhuru Kenyatta alipokuwa akilihutubia taifa mara baada ya kuapishwa , na kusema kwamba raia wa Afrika Mashariki watahudumiwa kama raia wa Kenya na kupewa haki zote za msingi ikiwemo kufanya kazi nchini humo, huku wale wa nchi zingine za Afrika watapewa viza akifika katika kiingilio chochote mpakani au viwanja vya ndege Kenya.

Pamoja na hayo Uhuru Kenyatta amesema hataweka masharti kwamba lazima mataifa mengine yafanye hivyo kwa wakenya watakaotaka kuingia kwenye nchi zao.

Uhuru Kenyatta ameapishwa leo katika uwanja wa Taifa wa Moi Kasarani jijini Nairobi, na kuhudhuriwa na maelfu ya watu na viongozi mbali mbali wa nchi za Afrika.

 

By Jamhuri