Nianze kwa kutoa taarifa. Katika toleo lililopita niliandika habari kuhusu Dk. Myles Munroe. Kuanzia Jumapili usiku na zaidi sana Jumatatu asubuhi ya wiki iliyopita, wengi walipata taarifa za kifo cha Dk. Munroe kwa ajali ya ndege. 

Kilichowasumbua wasomaji wa safu hii ni kuona taarifa za Dk. Munroe katika makala yangu siku ya Jumanne huku nikiwa sijaeleza chochote kuhusu kifo chake.

Wengi walinipigia wakiamini kuwa sina taarifa kuhusu kifo chake. Kimsingi ni kwamba taarifa za kifo cha Dk. Munroe zilikuja saa kadhaa baada ya gazeti hili kuwa limeshaingia mitamboni kuchapishwa. Kwa maana hiyo isingekuwa rahisi kuibadilisha makala ile kuendana na ‘breaking news’ hizo.

Mimi nilikuwa mwanafunzi na mfuasi mkubwa wa Dk. Munroe, hivyo unaweza kuelewa namna kifo chake (yeye, mke wake, msaidizi wake na binti yake, jumla yao watu tisa), vilivyonigusa na kuniuma mno. Ninalitukuza jina la Mungu kwa yote. Daima nimekuwa nikiamini kuwa, Mungu anabaki kuwa Mungu hata kama asipotenda kama tunavyotarajia. Sasa tuendelee na mada yetu ya leo.

Bila shaka wafuatiliaji wa safu hii mnatambua kuwa nimekuwa nikiandika safu hii kwa kufuata mpango kazi ninaojiwekea kila mwanzoni mwa mwaka. Mpango kazi wa mwaka huu umekuwa ni kuwajengea mfumo imara wa kifikra na kiuamuzi kwa wafanyabiashara, wajasiriamali na watu wengine katika maeneo ya uongozi wa nafsi zao, usimamizi wa chumi zao na uwezo wa kuona na kutumia fursa. Ukirejea utathibitisha kuwa asilimia 95 ya makala za mwaka huu zimekuwa zikitiririsha maarifa yanayo-‘fit’ kwenye mpango kazi huu.

Kutokana na hilo, leo tunaangalia nguvu ya watu wanaokuzunguka katika kukufanikisha kibiashara na katika maeneo mengine yote. Ninaposema watu wanaokuzunguka ninamaanisha wale watu ambao una ukaribu nao, unaoshirikiana nao katika kazi zako — marafiki, washauri wako, wapambe na hata wale unaowashirikisha mambo yako — iwe ni mara kwa mara ama kila siku.

Upo msemo wa Waingereza usemao, nioneshe marafiki zako nami nitakueleza wewe ni mtu wa aina gani. Pia msemo mwingine wa Kiswahili unasema ndege wanaofanana huruka katika kundi moja. Vile vile mwandishi na mzungumzaji wa kimataifa, Jim Rohn anasema, “Kila mtu ni wastani wa watu watano ambao hutumia muda mwingi pamoja nao”.

Iko hivi: tabia, mwenendo na hali ya mtu huakisiwa kupitia wale anaoshirikiana nao. Machinga utaona marafiki zake wengi ni machinga wenzie. Mfanyabiashara wa nyama naye atakuwa na marafiki na watu wake wanaomfanikishia biashara yake.

Hapa ngoja nikupe mfano wa Mwalimu Yesu Kristo anayefahamika kwa watu wengi. Kwa mujibu wa maandiko matakatifu tunaona kuwa mwalimu huyu alikuwa na watu wengi sana anaofahamiana nao katika miji na maeneo alikokuwa akifanyia shughuli zake.

Alikuwa na urafiki na viongozi wa kiserikali, alikuwa na urafiki na watu wa mitaani lakini pia alikuwa akiambatana na watu wanaotambulishwa kama wanafunzi lakini walikuwapo wafuasi yaani wale ambao walivutiwa na mafundisho yake na kuamua kumfuata. Watu wake wengine wa karibu walikuwa ni matajiri wa miji na wenye ushawishi mkubwa mmoja wapo akiwa Yusufu wa Armataya.

Katika wanafunzi wake huyu Yesu tunaambiwa alikuwa nao “wengine sabini” ambao majina yao hayatajwi ijapokuwa tunaona kuwa nao walitumwa kazini. Nini maana yake? Maana yake ni kwamba hawa sabini hawakuwa karibu sana na mwalimu huyu kama walivyokuwa wale kumi na wawili ambao kimsingi majina yao yanajulikana. Hata katika hawa kumi na mbili rekodi zinaonesha kuwa mwalimu huyu alikuwa na ukaribu zaidi na wanafunzi watatu ambapo kati yao yupo mmoja aitwaye Petro aliyemwachia uongozi alipoondoka.

Yapo mambo nataka ujifunze kutokana na mfumo alioutumia mwalimu huyu kuhusu watu wanaokuzunguka. Rekodi zinatuonesha kuwa alipohitaji msaada kutoka serikali ya ‘Kirumi’ kuna watu walikuwapo kumsaidia. Alipohitaji fedha tunaambiwa watu wake wa karibu walimtumikia kwa fedha na mali zao. Hata alipofariki rafiki yake Yusufu wa Armataya, mtu tajiri na kiongozi katika baraza la mji ndiye aliyegharimia mazishi yake.

Alipohitaji kupeleka bidhaa zake (mafundisho) sehemu mbalimbali wakawapo na “wengine sabini” kwa ajili ya kusaidia kutanua biashara (huduma). Matajiri wa miji walimpenda kwa sababu mafundisho yake yanathibitisha namna alivyowafundisha kwa umakini namna ya kuzalisha fedha na kukuza mitaji yao kiufasaha.

Ninachokueleza hapa ni kwamba hakikisha unakuwa na marafiki ama watu ambao watasaidia kukamilisha malengo na mipango yako. Hakikisha unakuwa na mpango madhubuti wa kutafuta, kujiunganisha na kubanana na marafiki na watu wenye maana kwako. Lazima uhakikishe kwamba katika kila jambo unalolihitaji kuwepo na mtu wa uhakika wa kukusaidia ufanikishe.

Huna sababu ya kung’ang’ana kila siku na watu wanaokurudisha nyuma ama ambao hawana thamani yoyote wanayoongezea kwako. Unakuwaje na marafiki ama watu wanaokuzunguka ambao kwa asilimia 90 wanakunyonya? Huyu anakukopa fedha hakulipi, mwingine hana wazo lolote jipya la kimaendeleo analokushirikisha, yupo yupo tu!

Hawa unadirikije kuwaita marafiki zako? Inabidi ulijue hili, ukiona mahali kuna mtu mmoja anayejiweza katikati ya watu saba, basi uwe na uhakika kuwa baada ya muda utakuja kukutana na watu saba wasiojiweza kabisa! Kwa nini? Mtu mmoja anayewakilisha wengine sita watammalizia kila anachozalisha.

Ndiyo maana ninashauri mambo mawili. Kwa wale watu ambao ni wategemezi kwako (ndugu, wazazi n.k) hutakiwi kuwasaidia bali unatakiwa ufanye bidii kuwawezesha. Pili kwa wale watu ambao wanachagulika (mfano, marafiki), chagua wale ambao mtakuwa mkiinuana na si wale ambao watakuwa wakikuona wewe kama kituo cha kupatia misaada.

Usishirikiane na watu ili kuwaridhisha na wala usiogope kuwatema marafiki na watu wasiokufaa katika safari yako ya mafanikio. Maisha haya peke yake ni mzigo mkubwa kuubeba, sembuse kubeba tena furushi na marafiki mizigo! Kuna wakati inabidi hata uende mbele za Mungu umuombe akutenganishe na marafiki wanaorudi nyuma na kisha akuunganishe na watu na marafiki wanaoenda mbele!

Lakini kuna kitu nataka utambue kuhusu ‘levels’ za marafiki na watu wanaokuzunguka. Kuna watu wa karibu na kuna watu wa ndani. Watu wa karibu wanaweza kuwa ‘wowote’ kutegemea na jambo unalotaka wakufanikishie lakini watu wa ndani ni lazima (nasisitiza ni lazima) wawe wale wenye mtazamo, moyo, ari na utayari wa kuhakikisha mnainuana. Mwalimu Yesu Kristo alikuwa na ukaribu na wanafunzi wote (wale 12 na wengine 70) lakini lilipokuja suala la kukabidhi uongozi wa biashara yake alikuwa na “vichwa” vitatu tu, alivyoviamini zaidi.

Kufanikiwa kibiashara na katika maeneo mbalimbali huhitaji kuwa na ukaribu wa ndani na watu wengi. Unahitaji watu wachache tu na wakati mwingine hata mtu mmoja tu ambaye ‘mmeshibana’ kweli kweli na mioyo yenu imeambatana kwa dhati katika kusaidiana. Kuna mambo yako ambayo si wote wa karibu yako wanapaswa kuyajua, isipokuwa wale wa ndani.

Jambo kubwa linalomfanya mtu kuwa na ukaribu ama urafiki na watu wa aina fulani ni mtazamo wake, ‘unaoendana’ na mtazamo wa watu wa aina hiyo.  Kitakachokuwezesha ukubaliwe katika kundi fulani la watu si ulichonacho bali ni mtazamo unaokuwa nao. Kwa maana hii, unaweza kuwa na ukaribu ama urafiki na mtu yeyote kuanzia Ikulu hadi mtaani ikiwa ‘uta-tune’ mtazamo wako kuendana na ule wa unaotaka kuambatana nao.

Mathalani, kitakachokuunganisha na kundi la matajiri si kiasi cha mali unachomiliki isipokuwa ni mtazamo unaokuwa nao kuhusu utajiri. Kitakachokuwezesha kukaa kundi moja na wasomi si wewe kuwa na digrii nyingi kichwani, isipokuwa ni ule moyo wa kujifunza unaowezesha wasomi hao kukugawia maarifa.

Unawaza nini kuhusu utajiri? Unazungumza nini kuhusu matajiri? Namna unavyowaza kuhusu utajiri ndiko kunakoweza kuuvuta utajiri kukujia ama kuusukuma utajiri mbali na wewe. Nimekuwa nikiwasikia baadhi ya watu wakisema maneno haya, “Utajiri mkubwa ni mateso”, “Matajiri hawana amani” na wengine husema, “Bora niwe na fedha kiasi, zisiwe nyingi wala zisiwe chache, ziwe wastani”.

Huwezi kuwaza kuwa utajiri ni mateso halafu utazamie kuwapata marafiki walio matajiri. Huwezi kunena maneno hasi dhidi ya matajiri, halafu utazamie kuwa na ukaribu na matajiri. Hapo juu nimekupa baadhi ya kauli ambazo huwa nazisikia kutoka kwa watu mbalimbali kuhusiana na utajiri na matajiri.

Uhalisia ni kwamba ukichunguza maisha ya watu wenye imani kama hizi, utagundua kuwa watu waliowazunguka nao wana imani kama hizi hizi. Na kwa kuwa wanaamini kuwa fedha ya wastani ndiyo inayofaa, basi huendelea kufanya mambo yao, ajira zao, biashara zao kwa vipimo vya wastani. Kufikia viwango vya juu ni lazima ukutane na watu wanaofikiria viwango vya juu. Kukutana na kuambatana na watu wanaofikiria viwango vya juu ni lazima ubadilishe mtazamo wako, uachane na kufikiria ukawaida uanze kufikiria “u-juu”.

Kagua marafiki na watu wako wa karibu kisha hakikisha ‘una-pruni’ wasioenda unakoenda. Mtu anaweza kuwa mwema na mzuri, lakini kama haendi unakoenda jitenganishe naye kwa sababu ukikomaa kwenda naye, ujue yeye atafika lakini wewe utakuwa umepotea!

Kitabu changu “Ni wakati wako wa kung’aa” kipo nchi nzima, piga (0788 155 010) kwa maelekezo ya kukipata. Wasalaam!

[email protected] 0719127901

By Jamhuri