Na Mwandishi Wetu,JamhuriMeida

Watanzania wameshauriwa kuchangamkia Shahada za Uzamivu (PhD), zinazotolewa na vyuo vya nje kwa bei rahisi ili kuongeza idadi ya wataalamu na wahadhiri wa vyuo vikuu nchini.

Hayo yamesemwa jana jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Vyuo Vikuu Nje ya Nchi, Global Education Link (GEL), Abdulmalik Mollel, wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.

Alikuwa akizungumzia maonyesho ya vyuo vikuu vya Cyprus, Uingereza, Uturuki, Malasyia na India yaliyoanza jana Jumamosi kwenye hoteli ya Serena Dar es Salaam.

Amesema kuna baadhi ya watu wanaogopa kusoma Shahada za Uzamivu wakidhani kwamba zinagharama kubwa wakati nje ya nchi mafunzo hayo hutolewa kwa bei rahisi.

“Nitoe wito kwa wanafunzi wanaohitaji kusoma PhD mara nyingi wanafikiri vyuo vikuu nje ya nchi ni ghali sana na tunapokuwa na watu wengi wenye elimu ya kiwango hicho watatusaidia sana kujenga nchi yetu kwenye elimu,” amesema

“Sasa kwa mfano hivi vyuo ambavyo nimeleta mfano vyuo vikuu vya India, Cyprus, Uturuki PhD ni Dola 1,000 za Marekani hapo naongelea shilingi milioni mbili mpaka milioni nne kwa mwaka kwa kiwango cha PhD ni nafuu sana kwasababu kuna vyo hapa ndani gharama zinaweza kufikia hadi Sh milioni nane,” alisema Mollel

Amesema kama mwanafunzi anaweza kupata fursa ya kusoma Shahada ya Uzamivu kwa shilingi 2,300,000 mpaka 4,000,000 gharama hiyo kwenye vyuo vikuu mashuhuri duniani ni fursa kubwa.

“Kwa kuwa vyuo hivyo sasa viko nchini naona ni fursa ya sisi kuongeza idadi ya wahadhiri wanaotamani kusoma ngazi ya Uzamivu tusiogope gharama hizi za vyuo vya nje gharama zake ni ndogo na nafasi zipo,” alisema Mollel

Amesema Jumamosi na Jumapili vyuo hivyo vitakuwa na maonyesho makubwa ya elimu kuwapa fursa wanafunzi watanzania wenye mahitaji ya masomo kwenye nchi za nje.

Amesema maonyesho hayo yatafanyika katika ukumbi wa Serena kuanzia asubuhi hadi jioni na kwamba Jumapili yatafanyika kwenye viwanja vya Mapinduzi Square Zanzibar na baada ya maonyesho hayo vitaendelea na udahili wa wanafunzi.

Amesema kuanzia siku ya Jumatatu tarehe 27 vitakuwa vinadahili wanafunzi wanaotaka kusoma nje ya nchi katika ofisi za GEL jijini Dar es Salaam hadi mwezi ujao. “Kuna vyuo vimepunguza ada za masomo ya udaktari wa tiba kutoka shilingi milioni 30 kwa mwaka hadi shilingi milioni 10 kwa mwaka hii tunaona ni furs sana kwa watanzania kuchangamkia na watakaofika watapata udahili siku hiyo hiyo bure,” alisema Mollel

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Vyuo Vikuu Nje ya Nchi  Global Education Link (GEL) Abdulmalick Mollel, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maonyesho ya vyuo vikuu vya Uturuki, Malaysia, Ungingereza, Cyprus na India yanayoanza leo Jumamosi kwenye hoteli ya Serena  jijini Dar es Salaam na siku ya Jumapili yatafanyika kwenye viwanja vya Mapinduzi Square Zanzibar.

Amesema nchini India vyuo ambavyo vimeleta wawakilishi wake ni pamoja na Lovely professional (LPU), ambacho kimebobea kwenye elimu ya uhandisi na biashara, Chuo Kikuu cha MMU ambacho kimebobea kwenye elimu ya tiba na uhandisi na Chuo Kikuu cha Sharda ambacho kimebobea kwenye elimu ya Tiba, Sanaa na Biashara.

Ametaja vyuo vingine kuwa ni vya Cyprus kama Near East University kilichoko Kaskazini mwa nchi hiyo, Chuo Kikuu cha Kyrenia wakati nchi ya Uturuki vyuo vilivyokuja ni Gelism na Ishiki na Malasyia ni Chuo Kikuu cha Segi.

Mwisho

By Jamhuri