na Mwandishi Wetu, JamburiMedia, Arusha

Watanzania wametakiwa kubadilika kulingana na kasi ya mabadiliko ya sayansi na teknolojia, ili kuongeza ufanisi katika utendaji kazi na utoaji huduma, ikiwa ni pamoja na kujua aina bora ya matumizi ya yeknolojia na kukabiliana na athari zake.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Foundation For Civil Society (FCS), Katika ufunguzi wa Wiki ya Asasi za Kiraia (AZAKI), iliyozinduliwa rasmi leo Oktoba 23,2023 katika kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha AICC Jijini Arusha.

Kiwanga amesema kuwa matumizi sahihi ya aina ya Teknolojia pasi na kuathiri ustawi wa jamii, yataongeza kasi ya maendeleo katika jamii na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Mrajisi wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali Zanzibar Ahmed Abdullah ametoa rai kwa asasi za kiraia kuwa mstari wa mbele katika kubeba maono ya jamii kwa kuwa na matumizi bora ya Teknolojia.

Amesema kuwa Tanzania imeendelea kushika kasi kimaendeleo kutokana na mabadiliko ya kiteknolojia, na kwamba Teknolojia hiyo imewezesha kuwa na mifumo mizuri yenye kurahisha utoaji wa huduma bora.

“Wakati umefika kwa vijana kuona umuhumu wa matumizi bora na yenye tija katika mitandao ya kijamii, kwa lengo la kujiingizia kipato” amesema Abdullah.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Umma Benki ya Stanbic, Doreen Dominic amesema benki hiyo inashika nafasi ya nne kwa ukubwa nchini, katika utoaji wa huduma za kidigitali.

“Benki katika kuendana na masuala ya kijamii tunatoa mada juu ya kuboresha upatikanaji wa huduma za kifedha, kwa kutumia teknolojia za Kidigitali, na kutoa elimu kwa watu ambao bado hawajafikiwa, na huduma za kidijitali.

“Kwa pamoja tunaweza katika kutumia teknolojia ili kujenga Tanzania yenye umoja na mafanikio zaidi katika jamii na Taifa kwa ujumla” amesema Doreen.

By Jamhuri