Na WMJJWM- Dar es Salaam

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima amekutana na kuzungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Adam Mihayo kwa lengo la kujadili fursa za maendeleo ya wananchi hasa makundi maalum kupitia benki hiyo.

Katika kikao hicho kilichofanyika jijini Dar Es Salaam Desemba 28, 2023 Waziri Dkt. Gwajima ameishukuru benki hiyo kwa kuwezesha kufanikisha Tamasha la Maendeleo la Zijue Fursa, Imarisha Uchumi, Kataa Ukatili, Kazi Iendelee (ZIFIUKUKI) lililofanyika Dar es Salaam na Geita na kuwafikia zaidi ya wananchi 30,000.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB Adam Mihayo amesema benki hiyo itendelea kushirikiana na Wizara kuhakikisha wananchi hasa wa makundi maalum wanawezeshwa na kuendelezwa kiuchumi kwa maendeleo ya Taifa.

Wakati huo huo Waziri Dkt. Gwajima amekutana na wadau wengine akiwemo Mkurugenzi wa Taasisi ya C Sema Kiiya Joel, Mkurugenzi wa Taasisi ya AMO Amina Said na Mwakilishi wa Kampuni ya michezo ya kubahatisha ya Meridian Bet Amani Maeda ambapo wamezungumzia ushirikiano katika kuzitambulisha fursa mbalimbali kwa wananchi.

Katika vikao hivyo Mkurugenzi wa Taasisi ya FAGDI inayoratibu Tamasha la Maendeleo ZIFIUKUKI na Balozi wa kupinga Ukatili Simon Mwapagata amehudhuria.