BAADA ya Simba kumtimua Kocha Mkuu, Mfaransa, Pierre Lechantre, mabosi wa timu hiyo wamefikia uamuzi wa kuikabidhi timu hiyo kwa Mrundi, Masoud Djuma Irambona ambaye atasaidiwa na mkongwe, Selemani Matola.

 

Djuma ambaye ndiye kocha msaidizi wa Simba kwa sasa, yupo na kikosi hicho mjini hapa Nakuru ambapo Simba inajiandaa kucheza mchezo wa fainali ya michuano ya SportPesa Super Cup dhidi ya Gor Mahia, kesho Jumapili.

 

Juzi Alhamisi, mabosi wa Simba walimpiga chini Mfaransa huyo baada ya kushinikiza kupewa mkataba mpya licha ya kuambiwa asubiri mpaka timu itakaporudi Dar.

 

Lechantre alitofautiana na vigogo wa Simba baada ya kushinikiza mabadiliko makubwa kwenye mkataba wake ikiwemo mshahara wa Sh 90milioni kwa mwezi pamoja na kupandishiwa posho zote na hata ndege asafiri kwenye daraja la kwanza.

 

Chanzo chetu kilidokezwa na kiongozi mkubwa wa Simba kwamba baada ya timu hiyo kuwasili jijini Dar ikitokea Kenya, Djuma atatangazwa kama kocha mkuu huku msaidizi wake akiwa Matola ambaye msimu uliopita alikuwa kocha msaidizi wa Lipuli ya Iringa.

 

Matola ndiye nahodha wa mwisho kuipeleka Simba kwenye robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu wa 2003.

“Tumeamua kumuongeza Matola kwenye kikosi chetu kwa kuw atuna imani naye hivyo atakuwa msaidizi chini ya Djuma, tumepanga kumtambulisha mara tu tutakaporejea Tanzania.

 

“Kwa sasa tumeamua kufanya hivyo kwani tumeona ni bora kuwatumia makocha wa Kiafrika zaidi hasa wa ukanda wetu huu ambao wanajua vizuri staili ya soka letu kuliko Wazungu,” kilisema chanzo.

 

Alipotafutwa Matola alisema: “Bado sijapata taarifa kuhusiana na hilo lakini tungoje kwanza nitaweka wazi baadaye.”

Hakuna kiongozi wa Simba aliyekuwa tayari kuzungumzia ishu hiyo jana kwa kutajwa jina, huku wengi wakidai watatoa ufafanuzi baadaye.

By Jamhuri