Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Hospitali ya Taifa Muhimbili imefanya upasuaji wa kuondoa mtoto wa jicho kupitia njia ya kisasa ya matundu madogo (Phacoemulsification) ambapo katika hospitali za umma nchini inakua ya kwanza kufanya upasuaji wa ina hii.

Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji, Dkt. Rachel Mhaville amesema upasuaji huu umeenda sambamba na mafunzo ya kuwajengea uwezo wataalamu wa ndani pamoja na hospitali zingine kwa lengo la kuwezesha huduma hii kuwafikia Watanzania wengi zaidi umefanywa na wataalamu wa MNH kwa kushirikiana na wataalamu kutoka Korea na kupitia Taasisi ya Vision Care Tanzania.

Amesema MNH inapambana kutoa huduma za kibingwa na bobezi kwa Watanzania na nchi jirani ili kuhakikisha kama Hospitali ya Rufaa ya Taifa inakua kitovu cha utalii tiba .

‘‘Muhimbili inaendelea kunyoosha njia chini ya uongozi wa Mkurugenzi Mtendaji Prof. Mohamed Janabi na kuishi ndoto ya Mh. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhamasisha utalii tiba nchini na kufikia kile ambacho tunataka kufikia kama nchi’’ amefafanua Dkt. Mhaville

Akielezea kuhusu upasuaji huo, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Macho Muhimbili Joachim Kilemile amesema upasuaji huu ni tofauti na uliokuwa unatumika awali ambapo mgonjwa alikuwa anapasuliwa sehemu kubwa ili kuweza kutoa mtoto wa jicho.

Kwa mujibu wa Dkt. Kilemile upasuaji huu una faida nyingi kwakuwa mgonjwa anapona kwa muda mfupi na kuendelea na shughuli zake kama kawaida ambapo takribani wagonjwa 50 watanufaika na huduma hiyo.
 
‘‘Sababu za mtu kupata mtoto wa jicho ni umri kubwa, magonjwa mbalimbali ikiwemo ugonjwa Kisukari kwa wale wenye umri mdogo hasa pale ugonjwa huo usipodhibitiwa vizuri, magonjwa ya figo na ngozi’’ ameeleza Dkt. Kilemile

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkazi wa Taasisi ya Vision Care Tanzania Bi. Jieun Park amesema Vison Care itaendelea kushirikina na Muhimbili kuwajengea uwezo wataalamu na kusaidia upatikanaji wa vifaa tiba ili kuendelea kuboresha huduma za macho Muhimbili.

By Jamhuri