Wananchi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Morogoro wamehimizwa kufanya maandalizi ya kupokea huduma ya umeme kwa kutandaza nyaya kwenye nyumba zao (wiring) ili kujitayarisha na miradi inayoendela ya umeme kwenye vitongoji.

Wito huo umetolewa leo Mei 19, 2026 na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi Meja Jenerali (Mstaafu), Jacob Kingu wakati wa ziara ya kutembelea miradi ya kufikisha umeme inayosimamiwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika Mkoa wa Morogoro.

Katika ziara hiyo, Mwenyekiti Kingu alitembelea Vijiji vya Ulundo pamoja na Mtego wa Simba ambako miradi ya REA ya kufikisha umeme kwenye vitongoji inaendelea kutekelezwa. Akiwa huko, aliwahimiza wananchi kuhakikisha wanafanya wiring mapema ili miundombinu ya umeme kwenye vitongoji itakapokamilika waweze kuunganisha umeme.

“Umeme kwa sasa ni hitaji la msingi. Unabadilisha maisha ya watu, unaongeza uzalishaji na kuboresha huduma muhimu za kijamii kama afya na elimu,” amesema Balozi Kingu huku akitoa wito pia kwa taasisi za serikali kama shule na vituo vya afya kuhakikisha wanavuta umeme kwenye taasisi zao ili kuendelea kuboresha huduma kwa jamii.

Balozi Kingu alieleza kuwa serikali imeendelea kuwekeza katika kuboresha huduma za afya vijijini kwa kujenga vituo vya afya na zahanati pamoja na kupeleka vifaa tiba vya kisasa, lakini changamoto ya ukosefu wa umeme imekuwa ikikwamisha utoaji wa huduma bora.

Awalia, akitoa taarifa kuhusu utekelezaji wa miradi ya umeme Mkoa wa Morogoro, Msimamizi wa Miradi ya REA Kanda ya Kati, Mhandisi Aneth Malingumu amesema jumla ya Vitongoji 1,821 kati ya 3,391 tayari vimepatiwa umeme huku vitongoji 1,255 vikiwa kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji wa miradi ya kufikishiwa umeme katika Mkoa wa Morogoro.

Akiongea kwa niaba ya wananchi, Mwenyekiti wa Kijiji cha Mtego wa Simba Shomari Jaeka ameshukuru na kuipongeza serikali kwa kuweza kufikisha umeme katika kijiji chao na kuahidi kutumia msimu wa mavuno kuhamasisha wananchi katika kijiji chake kufanya wiring katika nyumba zao.

Kwa upande wake Mkandarasi anaetekeleza mradi wa HEP 2A kwa Mkoa wa Morogoro kupitia kampuni ya Sinotec, Kris Sun ameahidi watakamilisha mradi huo ndani ya muda wa mkataba.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma ya umeme kwa lengo la kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kuboresha maisha yao.