Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatarajia kuadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake kwa hafla maalum itakayofanyika Julai 1, 2026, sambamba na utoaji wa Tuzo za Rais kwa Walipakodi Bora wa Mwaka wa Fedha 2024/2025.

Akizungumza jijini Dodoma kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Yusuph Juma Mwenda, Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipakodi na Mawasiliano wa TRA, Bw. Richard Kayombo, amesema maadhimisho hayo yatafanyika chini ya kaulimbiu isemayo, “Miongo Mitatu ya TRA, Mlipakodi Shujaa, Tanzania Inayojitegemea.”

Bw. Kayombo amesema maadhimisho hayo yanalenga kuenzi mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 30 tangu TRA ianzishwe mwaka 1996, pamoja na kuendelea kuhamasisha ulipaji kodi kwa hiari na kuimarisha ushirikiano kati ya TRA na walipakodi.

Ameeleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atatoa Tuzo za Walipakodi Bora wa Mwaka wa Fedha 2024/2025 kwa walipakodi walioonyesha uadilifu, uwajibikaji na mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa kupitia ulipaji wa kodi.

Aidha, amesema tuzo hizo ni njia ya kutambua na kuthamini mchango wa walipakodi katika kugharamia huduma za kijamii, utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kukuza uchumi wa nchi katika nyanja mbalimbali. Amebainisha kuwa maendeleo yanayoonekana katika sekta za afya, elimu, miundombinu na huduma nyingine za umma yanategemea kwa kiasi kikubwa mapato yatokanayo na kodi.

TRA imewataka walipakodi na Watanzania kwa ujumla kuendelea kutimiza wajibu wao wa kodi kwa hiari na kwa wakati ili kuendelea kuchochea maendeleo ya Taifa na kujenga Tanzania yenye uchumi imara na endelevu.